Showing posts with label ushindani. Show all posts
Showing posts with label ushindani. Show all posts

Wednesday, January 14, 2015

"Leading Beyond the Walls:" Kitabu Murua

Kwa siku kadhaa sasa, nimekuwa nikisoma Leading Beyond the Walls: How High-Performing Organizations Collaborate for Shared Success, kitabu kilichohaririwa na Frances Hesselbein, Marshall Goldsmith, na Iain Somerville. Ni mkusanyo wa makala 23 zilizoandikwa na wataalam mbali mbali katika tasnia ya uongozi, wakizingatia hali halisi ya utandawazi wa leo, na umuhimu wa kwenda na wakati.

Kwenda na wakati kunahitaji wepesi wa kubadilika kifikra, kimwenendo, kimfumo na hali zingine, ili kumudu mahitaji na hali halisi ya mabadiliko yanayotokea ulimwenguni, ambayo hayakwepeki. Mafanikio ya shirika, taasisi, au kampuni
yanategemea utayari wa kujibadili. Mazoea ni kipingamizi kikubwa cha mafanikio; ni kama kuta ambazo tumejizungushia. Jukumu letu, ambalo halikwepeki, ni kuvunja hizo kuta, tuwe na uwanja na upeo usio na mipaka.

Wengi wa watunzi wa makala zilizomo kitabuni humu nilikuwa sijawahi hata kuwasikia, isipokuwa Joseph S. Nye, Jr., Stephen R. Covey, na Peter F. Drucker, ambaye niliwahi kusoma andiko lake mojawapo. Kati ya makala ambazo nilivutiwa nazo hata kabla ya kuzisoma ni "And the Walls Came Tumbling Down" (Jim Collins), "Dissolving Boundaries in the Era of Knowledge and Custom Work" (Sally Helgesen), "Culture is the Key" (Regina Herzlinger, "New Competencies for Tomorrow's Global Leader" (Marshall Goldsmith, Cathy Walt), na "Creating Success for Others" (Jim Belasco).

Kila makala ambayo nimesoma katika kitabu hiki imenipanua mawazo. Nimegundua mambo ya maana ambayo yataboresha mihadhara ninayotoa kwa jumuia, taasisi na makampuni. Nawazia, kwa mfano, mihadhara niliyotoa kwenye kampuni ya RBC Wealth Management.

Ninashukuru kuwa nilinunua kitabu hiki, ingawa sikumbuki ilikuwa lini. Nina ari kubwa ya kumaliza kusoma insha zote zilizomo, na nina hakika kuwa, Mungu akinijalia uzima, nitazisoma tena na tena.

Saturday, June 5, 2010

Warsha Zangu Hazina Posho

Tangu mwaka juzi, nimeendesha warsha Tanzania, kuhusu masuala ya utamaduni, utandawazi, na maendeleo. Nina malengo kadhaa katika kufanya hivyo.

Lengo moja ni kuwapa wa-Tanzania ujuzi ambao ninaendelea kuupata huku ughaibuni, kutokana na kusoma vitabu, kuongea na watu, na kuendesha warsha kuhusu masuala niliyotaja hapo juu. Natambua umuhimu wa kutoa fursa kwa wa-Tanzania kuyaelewa masuala hayo, waweze kujizatiti kwa ushindani wa dunia ya leo. Hakuna msingi bora na imara kuliko elimu.

Lengo la pili la kuendesha warsha hizi Tanzania ni kuleta mwamko mpya katika mfumo na uendeshaji wa warsha. Kwanza, kuna mtindo wa kutegemea wafadhili. Watu wamezoea kuona warsha zikifanyika kwa kutegemea fedha kutoka kwa wafadhili au taasisi fulani. Wahudhuriaji wa warsha wanategemea kulipiwa gharama za ushiriki, pamoja na posho. Vibahasha vya posho ni sehemu ya utamaduni wa warsha katika Tanzania.

Ninapinga utamaduni huu. Sitafuti wafadhili wa kulipia warsha zangu, na warsha zangu hazina posho. Badala yake, wanaohudhuria wanalipia.

Kwa mtazamo wangu, warsha ni fursa ya kujielimisha. Elimu ni mtaji mkubwa, pengine muhimu kuliko mitaji yote. Kama mtu analipia trekta limzalishie mazao shambani, kwa nini asilipie mtaji huu mkubwa kuliko yote, yaani elimu?

Huku Marekani, ninaona utaratibu huu wa kulipia warsha. Mimi mwenyewe nimeshalipia hela nyingi kuhudhuria warsha hizi. Ninajua umuhimu wake. Niligusia kidogo jambo hili katika blogu hii, nilipoongelea suala la kununua vitabu.

Ninanunua pia vitabu na kuvisoma. Kati ya vitabu nilivyonunua hivi karibuni ni Global Literacies. Kwa kusoma vitabu na kuhudhuria warsha, ninajiongezea mtaji wa elimu. Ufanisi wangu kama mtoa mada na mwendesha warsha unaendelea kuongezeka.

Katika kuendesha warsha zangu Tanzania, nataka kujenga utamaduni wa kuthamini elimu. Msimamo huu unanipa wajibu mkubwa. Nawajibika kujielimisha kwa uwezo wangu wote, ili niweze kuwa mwelimishaji bora. Ndio maana ninafanya bidii kuhudhuria warsha, kununua vitabu na kuvisoma, na pia kuendesha warsha. Ninaelimika hata ninapoendesha warsha.

Nawakaribisheni kwenye warsha zangu za mwaka huu:

Juni 12, "Culture, Globalization and Development," Meeting Point Tanga.

Julai 3, "Culture and Globalization," Arusha Community Church.

Julai 10, "Cultural Tourism," Arusha Community Church.

Natarajia kupanga warsha nyingine moja au mbili. Wasiliana nami: info@africonexion.com

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...