Showing posts with label Tanga. Show all posts
Showing posts with label Tanga. Show all posts

Saturday, June 5, 2010

Warsha Zangu Hazina Posho

Tangu mwaka juzi, nimeendesha warsha Tanzania, kuhusu masuala ya utamaduni, utandawazi, na maendeleo. Nina malengo kadhaa katika kufanya hivyo.

Lengo moja ni kuwapa wa-Tanzania ujuzi ambao ninaendelea kuupata huku ughaibuni, kutokana na kusoma vitabu, kuongea na watu, na kuendesha warsha kuhusu masuala niliyotaja hapo juu. Natambua umuhimu wa kutoa fursa kwa wa-Tanzania kuyaelewa masuala hayo, waweze kujizatiti kwa ushindani wa dunia ya leo. Hakuna msingi bora na imara kuliko elimu.

Lengo la pili la kuendesha warsha hizi Tanzania ni kuleta mwamko mpya katika mfumo na uendeshaji wa warsha. Kwanza, kuna mtindo wa kutegemea wafadhili. Watu wamezoea kuona warsha zikifanyika kwa kutegemea fedha kutoka kwa wafadhili au taasisi fulani. Wahudhuriaji wa warsha wanategemea kulipiwa gharama za ushiriki, pamoja na posho. Vibahasha vya posho ni sehemu ya utamaduni wa warsha katika Tanzania.

Ninapinga utamaduni huu. Sitafuti wafadhili wa kulipia warsha zangu, na warsha zangu hazina posho. Badala yake, wanaohudhuria wanalipia.

Kwa mtazamo wangu, warsha ni fursa ya kujielimisha. Elimu ni mtaji mkubwa, pengine muhimu kuliko mitaji yote. Kama mtu analipia trekta limzalishie mazao shambani, kwa nini asilipie mtaji huu mkubwa kuliko yote, yaani elimu?

Huku Marekani, ninaona utaratibu huu wa kulipia warsha. Mimi mwenyewe nimeshalipia hela nyingi kuhudhuria warsha hizi. Ninajua umuhimu wake. Niligusia kidogo jambo hili katika blogu hii, nilipoongelea suala la kununua vitabu.

Ninanunua pia vitabu na kuvisoma. Kati ya vitabu nilivyonunua hivi karibuni ni Global Literacies. Kwa kusoma vitabu na kuhudhuria warsha, ninajiongezea mtaji wa elimu. Ufanisi wangu kama mtoa mada na mwendesha warsha unaendelea kuongezeka.

Katika kuendesha warsha zangu Tanzania, nataka kujenga utamaduni wa kuthamini elimu. Msimamo huu unanipa wajibu mkubwa. Nawajibika kujielimisha kwa uwezo wangu wote, ili niweze kuwa mwelimishaji bora. Ndio maana ninafanya bidii kuhudhuria warsha, kununua vitabu na kuvisoma, na pia kuendesha warsha. Ninaelimika hata ninapoendesha warsha.

Nawakaribisheni kwenye warsha zangu za mwaka huu:

Juni 12, "Culture, Globalization and Development," Meeting Point Tanga.

Julai 3, "Culture and Globalization," Arusha Community Church.

Julai 10, "Cultural Tourism," Arusha Community Church.

Natarajia kupanga warsha nyingine moja au mbili. Wasiliana nami: info@africonexion.com

Thursday, June 3, 2010

Umuhimu wa Warsha Zangu

Sijui kama kuna jambo ninaloongelea mara nyingi zaidi katika blogu hii kuliko suala la tofauti za tamaduni duniani, athari zake, na umuhimu wa kuzielewa. Ni suala muhimu sana, hasa katika dunia hii ya utandawazi.

Nimekuwa nikiendesha warsha kuhusu masuala haya huku Marekani, na miaka ya karibuni nimeanza kufanya hivyo Tanzania. Masuala haya yanaendelea kufahamika vizuri katika makampuni, mashirika,taasisi, vyuo na jumuia mbali mbali huku Marekani na sehemu zingine za ughaibuni.

Lakini haya si mambo ya ughaibuni tu, na wala pasiwe na mtu akadhani ni mambo ya ughaibuni tu. Ndio maana naendesha warsha Tanzania. Kama kuna asiyeamini hayo, napenda kuleta tangazo la ajira lilitolewa na World Food Program la Umoja wa Mataifa hapa Tanzania, kama lilivyoripotiwa katika blogu ya Michuzi. Bofya hapa.

Kigezo cha ufahamu wa tamaduni tofauti, ufahamu wa namna ya kushughulika na watu wa tamaduni mbali mbali, kimesisitizwa kama sifa mojawapo ambayo mwomba ajira anatakiwa awe nayo. Watu waliohudhuria warsha zangu wanafahamu kuwa hapo ndipo kwenye msisitizo wa warsha zangu. Warsha zangu hazina mbwembwe wala madoido. Ni darasa, kama inavyoonekana hapa, hapa, na hapa.

Nimefurahi kuona tangazo hili la World Food Program, hasa kwa kuwa zimebaki siku chache tu kabla sijasafiri kuelekea Tanzania, ambako nitaendesha tena warsha. Kitu kimoja kinachotajirisha warsha hizi na kuzipa umuhimu wa pekee ni kuwa washiriki wanachangia uzoefu wao katika kuhusiana na watu wa tamaduni mbali mbali, sehemu zao za kazi au katika shughuli zingine. Hapo najifunza mengi, na natambua umuhimu wake. Warsha yangu ya kwanza ni tarehe 12 Juni, mjini Tanga, kama nilivyoeleza hapa.

Kwa taarifa zaidi, wasiliana nami: info@africonexion.com

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...