Thursday, September 22, 2016

David Robinson Ahutubia Chuo Kikuu cha Minnesota

Leo mchana nilikwenda Chuo Kikuu cha Minnesota, Minneapolis, kumsikiliza David Robinson, m-Marekani Mweusi anayeishi Mbeya, Tanzania, ambako ni mkulima wa kahawa. Huyu ni mtoto wa mwisho wa mwanariadha maarufu sana wa Marekani, Jackie Robinson, ambaye alikuwa pia mpinzani shujaa wa ubaguzi na mtetezi wa haki za wa-Marekani Weusi.

David Robinson aliamua kwenda kuishi Tanzania, kwenye kijiji cha Bara wilaya ya Mbozi. Alijitambulisha kwa wanakijiji akajieleza kuwa ni mtoto wa Afrika aliyepotezewa ughaibuni kwa karne kadhaa, katika utumwa, na sasa ameamua kurudi nyumbani. Wanakijiji walimpa shamba akaanza kulima kahawa. Aliungana na wanakijiji wengine, wakaanzisha chama cha ushirika kiitwacho Sweet Unity Farms

Aliongelea shughuli za chama chao cha ushirika, wanavyoshughulikia matatizo na changamoto na kujifunza. Alielezea mahusiano yao na wateja wa nchi mbali mbali, ikiwemo Marekani. Ingawa wao wako kijijini, wanashiriki katika uchumi wa ulimwengu, na ndio hali halisi ya utandawazi. Daima wanatafuta namna ya kujiweka kibiashara, pamoja na uwezo wao mdogo, katika ulimwengu ambao umetawaliwa na makampuni makubwa ya kimataifa.

Pichani hapa kushoto anaonekana David Robinson, Limi Simbakalia, mwanafunzi m-Tanzania wa Chuo cha St. Olaf ambapo ninafundisha, na mimi.

Kuna taarifa nyingi mtandaoni juu ya David Robinson na Sweet Unity Farms, yakiwemo mahojiano naye. Taarifa moja nzuri kabisa ni hii hapa. Aidha, kuna taarifa nyingi juu ya baba yake, mwanariadha Jackie Robinson. Mfano mmoja ni filamu hii hapa chini, inayoonyesha magumu aliyopitia na alivyopambana kishujaa katika mazingira ambayo yalikuwa mabaya sana kwa wa-Marekani Weusi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...