Showing posts with label Minnesota. Show all posts
Showing posts with label Minnesota. Show all posts

Monday, August 10, 2015

Bendera ya Tanzania Itapepea Faribault, Minnesota, 22 Agosti

Tarehe 22 Agosti, nitashiriki tamasha la kimataifa mjini Faribault, Minnesota. Nimeshalipia gharama. Nitakuwa na meza ambapo nitaweka vitabu vyangu na machapisho mengine.

Hapo nitaongea na watu siku nzima kuhusu shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, uandishi, na utoaji ushauri kuhusu athari za tofauti za tamadauni, ushauri ambao ninautoa kwa wanafunzi na waalimu wa vyuo vya Marekani na watu wengine waendao Afrika, taasisi na jumuia zenye mahusiano na wa-Afrika, na kadhalika.

Nitaweka pia mabango ya filamu ya "Papa's Shadow." Filamu hiyo, ambayo ni ya maelezo ("documentary"), kwa kiasi kikubwa ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliyebaki. Tunajadili maisha na maandishi ya Ernest Hemingway, hasa yale yanayohusu Afrika. Filamu hii itaanza kuonyeshwa hivi karibuni katika majumba ya sinema na itakuwa inapatikana katika DVD na kadhalika. Kwa taarifa zaidi tembelea tovuti ya Ramble Pictures.

Jambo jingine la pekee ni kuwa, kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa tamasha la kimataifa mjini Faribault, bendera ya Tanzania itapepea, sambamba na bendera za mataifa mengine. Siku chache zilizopita, nilipeperusha bendera hii katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Ninapokuwa Tanzania, ninaweza kuiangalia bendera ya Tanzania nikawa ninaguswa kwa namna fulani, lakini hisia hizo huwa za pekee zaidi huku ughaibuni. Ingekuwa natoka Dar es Salaam kwenda kushiriki tamasha Mtwara, Chake Chake au Mbeya nisingeona sababu ya kubeba bendera ya Tanzania, labda kama tamasha ni la kimataifa. Na hata ningebeba, watu hawangekuwa na duku duku nayo au mshangao. Ni kitu walichozoea.

Lakini mambo ni tofauti huku ughaibuni. Sina namna ya kuelezea vizuri ninachomaanisha. Labda kwa kuwa niko mbali, nina hisia za pekee kuhusu kijiji changu cha Lituru, kata yangu ya Litembo, wilaya yangu ya Mbinga, mkoa wangu wa Ruvuma, na nchi yangu ya Tanzania.

Isipokuwa, jambo moja ni wazi, na linaelezeka: watu watakaohudhuria tamasha mjini Faribault wataiona bendera ya Tanzania. Bendera hii itatokea katika picha mbali mbali watakazopiga siku hiyo na kuzihifadhi, kuwapelekea marafiki au kuziweka mitandaoni.

Tuesday, April 7, 2015

Mhadhara Ujao, Lands Lutheran Church

Siku zimekwenda kasi. Wiki kadhaa zimepita tangu nilipopata mwaliko wa kwenda kutoa mhadhara katika mkutano wa Sinodi ya Kusini Mashariki ya Minnesota. Mkutano ulipangwa kufanyika mjini Zumbrota, kwenye Kanisa la Lands Lutheran, tarehe 11 Aprili.

Mama aliyenialika, kwa niaba ya kamati ya maandalizi, alisema kuwa wangependa niongelee masuala ambayo yameanza kujitokeza katika sharika mbali mbali za sinodi kutokana na kuingia kwa watu kutoka tamaduni mbali mbali. Aliniambia kuwa aliwahi kunisikiliza miaka kadhaa iliyopita katika kanisa lake la First English Lutheran Church, mjini Farbault, nikiongelea masuala hayo, akanunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Wiki zilizofuata, mama huyu nami tuliwasiliana ili kupanga mada ya mhadhara wangu. Nilitoa mapendekezo, naye aliyawasilisha kwenye kamati yao. Pendekezo walilolichagua ni "The Dilemma of Cultural Differences: Challenges and Opportunities."

Niliandika taarifa ya mwaliko katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Sasa siku imekarbia, nami nangojea kwa hamu kwenda kujumuika na waumini hao kutoka makanisa mbali mbali, na kuwapa mawazo na mawaidha yangu kuhusu hali wanayoikabili ya kujikuta wana watu wa tamaduni mbali mbali. Azma yao ya kutaka kujua nini cha kufanya ni mfano wa kuigwa.

Kadiri dunia inavyoendelea kubadilika kutokana na utandawazi wa leo, jamii zote zitalazimika kutafuta njia za kuishi pamoja na watu wa tamaduni tofauti. Hili ni suala ambalo nimelitafiti, kulitafakari, na kuliongelea kwa miaka mingi.

Kama ilivyo kawaida hapa Marekani, niliulizwa malipo yangu ni kiasi gani. Nilijibu kama nilivyozoea, kwamba waamue wenyewe, kufuatana na uwezo wao. Nasukumwa na dhamiri yangu, kutumia vipaji alivyonipa Mungu kwa manufaa ya wanadamu. Pesa si msingi.

Ningekuwa na uchu wa pesa, kama fisadi, ningesema ngoja niwakamue. Lakini mtu unayemtegemea Mungu unajiuliza: Je, tunabarikiwa kwa kutanguliza pesa mbele badala ya ubinadamu? Ninashukuru ninavyofanikiwa kuwagusa wanadamu.

Monday, December 22, 2014

Mkutano na Wanachuo wa Gustavus Adolphus Unakaribia

Siku zinakwenda haraka. Tarehe 5 Januari, ambayo imekaribia, ndio siku nitakayokutana na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus, kama nilivyoandika hapa. Hao ni wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya Tanzania, kujiongezea elimu kuhusu masuala ya afya na matibabu katika mazingira tofauti na ya Marekani, hasa kwa upande wa utamaduni.

Profesa wao aliniomba nikaongee nao kuhusu masuala ya aina hiyo kwa mapana kufuatia yale niliyoandika katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho watakuwa wamekisoma kabla ya mimi kukutana nao.

Kutokana na kusoma hiki kitabu, wanachuo hao watakuwa wameandaa masuali. Kama ilivyotokea siku zilizopita, masuali mengine yatazuka hapo hapo.

Jukumu hili linanifanya nikipitie tena kitabu changu, angalau kijuujuu, kwani sina mazoea ya kusoma sana yale ambayo nimeshayaandika na kuyachapisha. Napendelea kutumia muda wangu na akili yangu katika kutafiti, kutafakari na kuandika mambo mapya. Ingawa yale yaliyomo kitabuni sijayabadili, na sijaona sababu ya kuyabadili, ninafahamu mengi zaidi na naendelea kujifunza, kwani elimu haina mwisho.

Kutokana na ukweli huu, mazungumzo yangu na hao wanachuo wa safari hii hayawezi kuwa sawa na yale ya miaka iliyopita. Hata kama kutakuwa na masuali yanayofanana na yale ambayo nimeshaulizwa kabla, majibu yangu yatajengeka katika upeo mpana zaidi. Fursa za aina hii zinachangia kupanua upeo huo.

Tutakutana, kama siku zilizopita, Mount Olivet Conference & Retreat Center, pembeni mwa mji wa Lakeville, Minnesota. Nangojea kwa hamu kuonana tena na Profesa Zust, na kuonana na hao wanachuo wapya. Panapo majaliwa, nitaweka ripoti katika blogu hii, kama nilivyozoea.

Saturday, April 13, 2013

Maonesho ya Elimu na Huduma za Jamii, Brooklyn Park

Leo nimeshiriki maonesho ya elimu na huduma za jamii yaliyoandaliwa na African Career, Education & Resource, Inc (ACER). Maonesho haya yalifanyika katika shule ya Park Center, Brooklyn Park, Minnesota. Wadau wa huduma kama afya, ajira, elimu, na malezi ya vijana, walikuwepo, kutoa elimu na ushauri, na hasa kuifahamisha jamii kuhusu huduma wanazotoa.
Nilipata fursa ya kukutana na watu ambao tunafahamiana, na wengine ambao hatukuwa tunafahamiana.








Huyu dada anayeonekana kwenye picha ya juu kabisa na hapa kushoto alikuwa mwanafunzi wangu hapa Chuoni St. Olaf, miaka 13 iliyopita. Asili yake ni Ethiopia. Ni shabiki mkubwa wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences




Kati ya hao tunaofahamiana, ambao tumekutana leo, ni Dr. Alvine Siaka kutoka Cameroon, ambaye ni mratibu wa African Health Action. Mwingine ni Rita Apaloo, kutoka Liberia, ambaye ni mratibu wa jumuia iitwayo African Women Connect. Rita naye ni shabiki wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences

Kati ya watu ambao tumefahamiana leo ni dada Iqbal Duale, m-Somali, ambaye ni mtaalam wa elimu ya jamii.  Tulielezana shughuli zetu kwa jamii, tukaona zinahusiana. Taasisi anayofanyia kazi inaitwa Planned Parenthood.  Tutawasiliana zaidi, Insh' Allah.

 Kama kawaida, kwenye mikusanyiko kama hii, tulipata fursa ya kubadilishana mawazo. Tuliongelea shughuli tunazofanya, changamoto zake na malengo yake, na umuhimu wake kwa jamii. Kitu kimoja cha kuvutia na kutia moyo ni kuwa pamoja na changamoto zote na magumu, kila moja wetu ana msimamo thabiti kuwa hakuna kulegea, kurudi nyuma, wala kukata tamaa. Changamoto hizi ni kama chachu kwetu.

Taasisi iliyoandaa maonesho ya leo, yaani ACER, niliitaja siku chache zilizopita, katika ujumbe wangu kuhusu mkutano wa bodi ya taasisi ya Afrifest. ACER na Afrifest tumeamua kushirikiana, nami niliamua kuhudhuria maonesho ya leo kama njia ya kujenga uhusiano huo.

Mimi ni mwenyekiti wa bodi ya taasisi ya Afrifest. Papo hapo, nilienda nikiwa nimejisajili kwa jina la kampuni ya Africonexion. Nilikuwa na meza, kama inavyoonekana hapa kushoto, ambapo niliweka vitabu na machapisho yangu mengine, nikapata fursa ya kuongea na wadau waliofika hapo. Wengine wana wadhifa katika taasisi zinazoshughulikia masuala ninayoshughulikia, yaani ya elimu kuhusu tofauti za tamaduni. Uzuri wa kukutana namna hiyo ni kuwa tunajenga msingi wa kushirikiana siku zijazo.

Monday, December 10, 2012

Baridi Kali Minnesota

Jimbo la Minnesota ni moja ya sehemu zinazopata baridi kali kuliko zote Marekani, wakati wa miezi ya baridi. Jana imeanguka theluji nyingi, kama inavyoonekana pichani, katika eneo la Chuo cha St. Olaf.

Wakati kama huo ni hatari kuendesha magari, na ajali huwa nyingi, yaani magari kugongana barabarani, au kuteleza na kutumbukia mitaroni.













Baridi hii haizoeleki hata kama mtu umepambana nayo miaka na miaka. Inapokuja, ni bora kubaki nyumbani, kama huna sababu ya lazima ya kwenda nje, na kama unakwenda nje, ni lazima kujizatiti kwa mavazi yatakiwayo. Vinginevyo, baridi hii itakuletea madhara. Kuna watu wanaokufa kutokana na kuwa nje kwenye baridi hii.

Katikati ya picha hapa kushoto linaonekana gari maalum ambalo kazi yake ni kusafisha njia na barabara kutokana na kufunikwa na theluji.

Sunday, December 19, 2010

Kitabu Kimetua St. Cloud, Minnesota

Wasomaji wa blogu zangu, hii na ile ya ki-Ingereza, wanafahamu ninavyopenda kujishughulisha na masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake katika ulimwengu wa leo.

Nafanya shughuli hizi si kwa ajili ya kutafuta umaarufu, bali naamini ni wajibu kwa wanadamu kusaidiana katika maisha na kuifanya dunia iwe bora kuliko ilivyo.

Miezi ya karibuni nimejishughulisha sana na matatizo yanayowapata wahamiaji wa ki-Somali katika jimbo la Minnesota, ambalo linaongoza kwa idadi ya wahamiaji wa ki-Somali. Wasomaji wa blogu zangu watakumbuka taarifa za shughuli zangu katika mji wa Faribault.

Matatizo kama haya ya Faribault yako pia katika miji mingine, kama vile St. Cloud. Kutokana uzoefu nilioupata Faribault, nimeanzisha mawasiliano na ndugu Mohamoud Mohamed, mkurugenzi wa SASSO, jumuia inayoshughulikia masuala ya wa-Somali mjini St. Cloud.

Nilimpelekea nakala ya kitabu cha Africans and Americans, kama mchango wangu na changamoto. Jana ameniambia kuwa kitabu amekipata, anaendelea kukisoma, na anakipenda. Atawaonyesha wadau wa St. Cloud: halmashauri ya mji, shule na vyuo, idara ya polisi, mahospitali, na kadhalika. Nami nilimhakikishia kuwa ni jambo bora. Badala ya watu kununiana tu au kugombana, ni vema wakaanza utaratibu wa kuzungumzia matatizo kama ilivyofanyika Faribault, na ikapokelewa vizuri.

Kama ninavyosema katika mihadhara, blogu na maandishi mengine, matatizo ya aina hii yanayoikumba miji ya Faribault na St. Cloud yanajitokeza katika miji na jamii nyingine duniani: Afrika, Asia, Australia, Marekani, Ulaya, na kwingineko, na yataongezeka, kutokana na mwenendo wa utandawazi wa leo. Ninapokuwa Dar es Salaam, kwa mfano, nasikiliza na kutafakari minong'ono na majungu kuhusu wa-China, ambao wanaendelea kuja katika mji ule. Niliwahi pia kuongelea tafrani iliyotokea Zanzibar. Kinachobaki ni sisi kujizatiti kwa kuelimishana kuhusu tofauti zetu na kutafuta namna ya kuishi bila matatizo.

Najiandaa kushiriki katika masuala ya St. Cloud. Mbali ya umuhimu wake kwa jinsi hali ilivyo, ni fursa ya mimi kujiongezea ujuzi na uzoefu nitakaoutumia katika kuwasaidia wengine.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...