Showing posts with label bendera ya Tanzania. Show all posts
Showing posts with label bendera ya Tanzania. Show all posts

Thursday, April 27, 2017

Bendera ya Tanzania Kupepea Rochester, Minnesota

Kwa mara ya kwanza bendera ya Tanzania itapeperushwa katika tamasha la kimataifa mjini Rochester, Minnesota, tarehe 29 mwezi huu. Hili ni tamasha linaloandaliwa na Rochester International Association (RIA) kila mwaka. Nimewahi kuelezea kuhusu tamasha hili katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Napenda kuelezea mchakato uliowezesha bendera ya Tanzania kupewa hadhi hiyo. Mwaka jana wa-Kenya wawili, Olivia Njogu na Kennedy Ombaye, ambao ni wanabodi wa RIA, waliniambia kuwa wangependa nijiunge nao. Niliguswa na wazo lao, nikaafiki. Waliwasilisha ujumbe kwa mwenyekiti wa bodi, Brian Faloon, nami nikawasiliana naye kumthibitishia utayari wangu wa kujiunga. Wazo lilipitishwa na bodi, nami nikajiunga.

Wiki chache zilizopita, bodi ilianza kujadili mipango ya tamasha la kimataifa kwa mwaka huu. Wakati suala la bendera lilipojadiliwa, mwanabodi Olivia Njogu aliniambia kuwa iwepo bendera ya Tanzania. Kwa kuwa sikuelewa utaratibu wa bendera ukoje, Olivia na wanabodi wengine walinihakikishia kuwa sitahitaji kuileta bendera, bali wataipata kwa muuzaji. Nilifahamu kuwa utaratibu wa tamasha ni kuwa linapoanza, panakuwa na maandamano ya watu wakiwa wamebeba bendera za nchi mbali mbali.

Mwaka jana niliposhiriki tamasha hili, nilikuwa na bendera ya Tanzania, ambayo nilikuwa nimeinunua mwaka juzi, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Lakini kwa kuwa nilikuwa bado mgeni katika tamasha hili, sikuwa nimefanya utaratibu wa kuijumlisha katika maandamano ya bendera. Niliitandaza kwenye meza yangu, kama inavyoonekana pichani hapa kushoto.

Ninawashukuru tena wa-Kenya kwa urafiki na ukarimu ambao wamenionyesha tangu nilipokwenda nchini kwao kufanya utafiti, kuanzia mwaka 1989, hadi miaka yote niliyoishi huku Marekani. Jambo hili nimekuwa nikilitaja katika blogu hii.

Friday, April 29, 2016

Ninajiandaa Kushiriki Tamasha Rochester

Jioni hii, ninajiandaa kwenda Rochester, Minnesota, kushiriki tamasha la kimataifa kesho. Nitaondoka asubuhi sana ili nikawahi kabla ya saa nne litakapoanza tamasha. Nimeshalipia meza. Nitapeleka vitabu vyangu kama kawaida.

Meza ya vitabu katika tamasha ni kivutio kwa watu, sawa na meza za bidhaa na vitu vingine mbali mbali vinavyokuwepo. Watu wanapenda kuangalia vitabu, kuuliza masuali juu ya vitabu hivi, na wengine kuvinunua. Mimi mwenyewe ninapenda kuongelea mambo yanayonisukuma kuandika, hasa fasihi, tamaduni, na changamoto zitokanazo na tofauti za tamaduni.

Nitabeba pia bendera ya Tanzania. Nilishawahi kuelezea katika blogu hii namna nilivyofikia uamuzi wa kununua bendera hii, kwa ajili ya matamasha na maonesho mbali mbali. Huku ughaibuni, bendera ya Taifa ina mguso wa pekee moyoni. Kwa vile tamasha la kesho ni la kimataifa, bendera hii itakuwa mahali inapohitajika.

Tamasha la kimataifa hufanyika kila mwaka mjini Rochester. Mji huu una wakaazi kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Kufanyika kwa tamasha la kimataifa katika mji huu ni jambo lenye mantiki bora. Watu wanaonesha tamaduni za nchi zao, na wote wanajifunza kutoka kwa wenzao.

Mwaka jana nilihudhuria tamasha la Rochester kwa mara ya kwanza, na niliandika habari zake hapa, na hapa. Ninangojea kwa hamu kukutana tena kesho na baadhi ya watu niliokutana na kufahamiana mwaka jana.

Kwangu mimi mwalimu, matamasha ya aina hii ni kama darasa. Kila ninapohudhuria, ninajikuta nikifundisha na pia kujifunza siku nzima. Nategemea kuandika taarifa za tamasha la kesho hapa katika blogu yangu.

Monday, August 10, 2015

Bendera ya Tanzania Itapepea Faribault, Minnesota, 22 Agosti

Tarehe 22 Agosti, nitashiriki tamasha la kimataifa mjini Faribault, Minnesota. Nimeshalipia gharama. Nitakuwa na meza ambapo nitaweka vitabu vyangu na machapisho mengine.

Hapo nitaongea na watu siku nzima kuhusu shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, uandishi, na utoaji ushauri kuhusu athari za tofauti za tamadauni, ushauri ambao ninautoa kwa wanafunzi na waalimu wa vyuo vya Marekani na watu wengine waendao Afrika, taasisi na jumuia zenye mahusiano na wa-Afrika, na kadhalika.

Nitaweka pia mabango ya filamu ya "Papa's Shadow." Filamu hiyo, ambayo ni ya maelezo ("documentary"), kwa kiasi kikubwa ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliyebaki. Tunajadili maisha na maandishi ya Ernest Hemingway, hasa yale yanayohusu Afrika. Filamu hii itaanza kuonyeshwa hivi karibuni katika majumba ya sinema na itakuwa inapatikana katika DVD na kadhalika. Kwa taarifa zaidi tembelea tovuti ya Ramble Pictures.

Jambo jingine la pekee ni kuwa, kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa tamasha la kimataifa mjini Faribault, bendera ya Tanzania itapepea, sambamba na bendera za mataifa mengine. Siku chache zilizopita, nilipeperusha bendera hii katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Ninapokuwa Tanzania, ninaweza kuiangalia bendera ya Tanzania nikawa ninaguswa kwa namna fulani, lakini hisia hizo huwa za pekee zaidi huku ughaibuni. Ingekuwa natoka Dar es Salaam kwenda kushiriki tamasha Mtwara, Chake Chake au Mbeya nisingeona sababu ya kubeba bendera ya Tanzania, labda kama tamasha ni la kimataifa. Na hata ningebeba, watu hawangekuwa na duku duku nayo au mshangao. Ni kitu walichozoea.

Lakini mambo ni tofauti huku ughaibuni. Sina namna ya kuelezea vizuri ninachomaanisha. Labda kwa kuwa niko mbali, nina hisia za pekee kuhusu kijiji changu cha Lituru, kata yangu ya Litembo, wilaya yangu ya Mbinga, mkoa wangu wa Ruvuma, na nchi yangu ya Tanzania.

Isipokuwa, jambo moja ni wazi, na linaelezeka: watu watakaohudhuria tamasha mjini Faribault wataiona bendera ya Tanzania. Bendera hii itatokea katika picha mbali mbali watakazopiga siku hiyo na kuzihifadhi, kuwapelekea marafiki au kuziweka mitandaoni.

Sunday, August 2, 2015

Bendera ya Tanzania Katika Tamasha la Afrifest 2015

Jana, tarehe 1 Agosti, tamasha la Afrifest lilifanyika mjini Brooklyn Park, Minnesota. Hili ni tamasha ambalo huandaliwa mara moja kwa mwaka na bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. ili kuwakutanisha wa-Afrika, watu wenye asili ya Afrika waishio Marekani ya Kaskazini, Kati, na Kusini, pamoja na Caribbean, na pia watu wa mataifa mengine. Lengo kubwa ni kufahamiana, kuelimisha, na kuuenzi mchango wa watu weusi duniani kote, katika nyanja mbali mbali.

Hiyo jana ilikuwa ni mara ya kwanza kwa bendera ya Tanzania kupepea kwenye tamasha la Afrifest. Baada ya kushiriki matamasha na kujionea wenzetu wanavyotumia fursa kuzitangaza nchi zao, nilijiuliza kwa nini nisitafute bendera ya Tanzania, kama nilivyoeleza katika blogu hii.

Hatimaye, nilifanya uamuzi wa kununua bendera, niwe ninaipeperusha kwenye matamasha ninayoshiriki, maadam fursa zipo. Hapo kushoto naonekana na binti zangu Assumpta na Zawadi kwenye meza yetu, hiyo jana.
Sawa na kuweka vitabu mezani katika tamasha, ambavyo huwavutia watu waje kuulizia habari zake, sawa na kutundika bendera ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants, ambayo nayo huwavutia watu waje kuulizia maana ya Africonexion, bendera hiyo nayo ni kivutio na kianzio cha mazungumzo kuhusu Tanzania.

Miaka yote, nimekuwa nikishiriki matamasha chini ya kivuli cha kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Hata hivi katika kuelezea shughuli zangu, sikujiwekea mipaka, kwani utafiti wangu, ufundishaji, uandishi na utoaji ushauri katika masuala ya athari za tofauti za tamaduni, nagusia dunia yote, ikiwemo Tanzania. Lakini kuitundika bendera ya Tanzania kama nilivyofanya jana kunaongeza mwonekano wa nchi katika nchi za dunia.

Kwa kuwa bendera hiyo ilipepea hapo uwanjani siku nzima, kila mtu katika umati wa waliohudhuria tamasha aliiona. Wengi wa waliohudhuria walipiga picha hapo uwanjani, na haikwepeki bendera kuonekana katika baadhi ya picha.

Wednesday, May 6, 2015

Leo Nimepata Bendera ya Tanzania

Leo nimepata bendera ya Tanzania. Niliwahi kuandika katika blogu hii kuwa mara kwa mara ninashiriki matamasha hapa Marekani ambapo watu huja na bendera za nchi zao, nami nilijisikia vibaya kwa kutokuwa na bendera kubwa ya nchi yangu. Nilifanya uamuzi muafaka, nikaagiza, na leo nimeipata.

Mwaka jana, nilipoandika ujumbe wangu, nilikuwa napeleleza katika tovuti kadhaa zinazouza bendera. Lakini safari hii, kwa kubahatisha tu, nimeingia katika tovuti ya Amazon nikaona bendera ziko, tena kwa bei rahisi sana.




Nimejionea hapa Marekani jinsi wa-Kenya walivyo hodari kwa suala hilo, na hapa naleta picha niliyopiga katika tamasha la Afrifest, tarehe 2 Agosti, mwaka jana, mjini Brooklyn Park, Minnesota. Inamwonyesha m-Kenya akitamba na bendera ya nchi yake.

Jiulize mwenyewe, ungejisikiaje kuwepo mahali ambapo wenzako wanatamba na bendera za nchi zao, nawe huna. Kwa nini ukae mahali hivyo, kama vile huna nchi? Hisia hizi ni kubwa unapokuwa ughaibuni. Sikutaka kuendelea kudhalilika namna hiyo.



Picha nyingine, inayoonekana hapa kushoto, nilipiga tarehe 11 Aprili, 2015, mjini Rochester, Minnesota, kwenye tamasha la tamaduni za ulimwengu. Inaonyesha meza ya wa-Kenya na bendera yao.

Kuna matamasha yanayokuja ambayo nitashiriki, kama vile tamasha la Afrifest, tarehe 1 Agosti, 2015. Nitakapokuwa naandika taarifa za matamasha hayo na maonesho, wadau mtajionea wenyewe bendera ya Tanzania ikipepea kwenye eneo la meza ya vitabu vyangu.

Tuesday, August 19, 2014

Laiti Ningekuwa na Bendera ya Tanzania

Jana nimeona taarifa mtandaoni kuwa Jumamosi hii, tarehe 23, mjini Faribault, Minnesota, kutakuwepo na tamasha la kimataifa la tamaduni. Hapo hapo nilipiga simu kwa waandaaji, ili kuona kama bado kuna nafasi ya mimi kushiriki.

Leo mratibu mkuu wa tamasha, amenipigia simu. Tumeongea kwa muda, nami nikamwulizia kama bado kuna nafasi ya kushiriki katika tamasha. Hapo hapo aliniambia kuwa nafasi bado iko, na kwamba tukimaliza maongezi atanitumia fomu ya kujisajili.

Tuliongelea shughuli nifanyazo katika jamii, ikiwemo kushiriki matamasha ya aina hii kama mwandishi na mwelimishaji, hasa kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake. Tuligusia pia ushiriki wangu katika masuala ya Faribault, kama ilivyotamkwa katika taarifa hii hapa.

Wakati tunaendelea na mazungumzo, aliniuliza kama nina bendera ya nchi yangu, yaani Tanzania. Alifafanua kwamba kwenye jukwaa kuu, zitakuwepo bendera za nchi wanakotoka washiriki wa tamasha, na kuna kipindi ambapo wawakilishi wa nchi hizo watakuwepo jukwaani wakiwa na bendera zao. Watapata dakika kadhaa za kuongelea mbele ya kadamnasi kuhusu nchi zao na hizo bendera. Hapo nilijisikia vibaya, kwani sina bendera ya Tanzania ya ukubwa utakiwao, ambao ni angalau futi  tatu kwa tano. Nilikiri kuwa sina, ila nikasema nitajitahidi katika siku hizi mbili tatu kutafuta.

Baada ya maongezi, nimeangalia mtandaoni nione wapi naweza kuipata bendera ya aina hiyo. Nimeona sehemu kadhaa, ambapo naweza kuagiza bendera hiyo. Nimepiga simu sehemu tatu, nikaambiwa kuwa hatawezekana kuipata kabla ya tamasha.

Kwa maana hiyo, nimekwama. Nimekosa fursa ya kuelezea habari za Tanzania na bendera yetu, mbele ya wote watakaohudhuria tamasha. Nimejifunza. Niko mbioni kuagiza bendera, niweze kuitumia siku za usoni.

Mji wa Faribault uko umbali wa maili kama 25 tu kutoka hapa ninapoishi. Nami si mgeni katika mji ule, kwani, kwa miaka iliyopita, nimeshafanya shughuli nyingi za jamii katika mji ule, kama ilivyoelezwa hapa, hapa, na hapa.

Lakini, pamoja na yote, hili suala la kutokuwa na bendera limenikera na papo hapo limenigutua. Mimi kama m-Tanzania, tena sio m-Tanzania wa uraia pacha, ningejisikia vizuri sana kuwepo kwenye jukwaa kuu na bendera yangu, nikasema mawili matatu kuhusu nchi yangu na bendera yake. Dosari hii ni lazima irekebishwe hima.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...