Friday, April 29, 2016

Ninajiandaa Kushiriki Tamasha Rochester

Jioni hii, ninajiandaa kwenda Rochester, Minnesota, kushiriki tamasha la kimataifa kesho. Nitaondoka asubuhi sana ili nikawahi kabla ya saa nne litakapoanza tamasha. Nimeshalipia meza. Nitapeleka vitabu vyangu kama kawaida.

Meza ya vitabu katika tamasha ni kivutio kwa watu, sawa na meza za bidhaa na vitu vingine mbali mbali vinavyokuwepo. Watu wanapenda kuangalia vitabu, kuuliza masuali juu ya vitabu hivi, na wengine kuvinunua. Mimi mwenyewe ninapenda kuongelea mambo yanayonisukuma kuandika, hasa fasihi, tamaduni, na changamoto zitokanazo na tofauti za tamaduni.

Nitabeba pia bendera ya Tanzania. Nilishawahi kuelezea katika blogu hii namna nilivyofikia uamuzi wa kununua bendera hii, kwa ajili ya matamasha na maonesho mbali mbali. Huku ughaibuni, bendera ya Taifa ina mguso wa pekee moyoni. Kwa vile tamasha la kesho ni la kimataifa, bendera hii itakuwa mahali inapohitajika.

Tamasha la kimataifa hufanyika kila mwaka mjini Rochester. Mji huu una wakaazi kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Kufanyika kwa tamasha la kimataifa katika mji huu ni jambo lenye mantiki bora. Watu wanaonesha tamaduni za nchi zao, na wote wanajifunza kutoka kwa wenzao.

Mwaka jana nilihudhuria tamasha la Rochester kwa mara ya kwanza, na niliandika habari zake hapa, na hapa. Ninangojea kwa hamu kukutana tena kesho na baadhi ya watu niliokutana na kufahamiana mwaka jana.

Kwangu mimi mwalimu, matamasha ya aina hii ni kama darasa. Kila ninapohudhuria, ninajikuta nikifundisha na pia kujifunza siku nzima. Nategemea kuandika taarifa za tamasha la kesho hapa katika blogu yangu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...