Showing posts with label Kenya. Show all posts
Showing posts with label Kenya. Show all posts

Thursday, October 12, 2017

Profesa Amekifurahia Kitabu

Ni kawaida yangu, kuchapisha maoni ya wasomaji wa vitabu vyangu. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa profesa moja ambaye alihudhuria mkutano wa Africa Network nilioshiriki kuuandaa hapa chuoni St. Olaf.

Profesa huyu Mmarekani anawapeleka wanafunzi wa ki-Marekani Kenya na Rwanda. Katika mkutano wetu, aliongelea programu hiyo, akielezea jinsi tofauti za tamaduni zinavyojitokeza.

Nilivutiwa na mhadhara wake, kwa kuwa nami ni mzoefu wa programu hizi za kupeleka wanafunzi Afrika, ikiwemo Tanzania. Nilimpelekea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, naye ameniandika ujumbe huu:

Dear Joseph,
There were several wonderful things that came from my attending the Africa Network conference. Meeting you and learning more is one. I just finished your book and enjoyed it so much. It made me laugh out loud and understand my Kenyan teaching colleague even more. I have been both to Rwanda and Kenya many times and am aware of many of the situations and misunderstandings you describe. I’ve shared my thoughts with Kitito and we hope to use your book in some way for our spring Cultural Identity course. 
Thanks again.

Ninashukuru kwamba kitabu hiki kinatoa mchango ambao nilipangia nilipokiandika, ikiwemo kuwaelimisha wanaohusika na programu za kupeleka wanafunzi Afrika. Msukumo wa kukiandika ulitoka katika mikutano ya jumuia ya vyuo iitwayo Associated Colleges of the Midwest (ACM), na baada ya kukichapisha, wahusika wa programu zingine nao wanakitumia. Mifano ni programu ya  chuo kikuu cha Wisconsin-Oshkosh na pia program ya chuo cha Gustavus Adolphus, ambayo nimeitaja mara kwa mara katika blogu hii.


Friday, June 2, 2017

Kitabu Kimependekezwa na Africa International University

Nimeona leo kuwa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimependekezwa na Africa International University (AIU) kwa ajili ya wanafunzi wa kigeni. Chuo hiki kiko Karen, nchini Kenya.

Nimevutiwa na maelezo yaliyotolewa kama Information for International Students juu ya hali halisi anayokumbana nayo mtu anapojikuta katika utamaduni wa kigeni:

Moving to a different cultural environment is a very stressful experience – that’s why it is sometimes referred to as “culture shock”. You will likely go through a difficult period of adjustment and homesickness after the initial excitement wears off. This is normal. As you learn your way around the campus and its unique culture, you will be more comfortable at AIU. Soon you will be helping other new international students adjust to AIU and Kenya. If you are willing to learn, you will learn a great deal about yourself and others who are different from you. You will leave here enriched and transformed.

Still, it is wise to take time before coming to prepare yourself and your family for the cultural adjustments that will be necessary. By reading as much as you can about cultural adjustment and talking to other international students, you can learn what to expect. Then you will better understand the feelings and frustrations you deal with as you adjust to your new environment. Since academics will demand a great deal of you at AIU, any preparation you can do before coming will help all of your adjustments once you arrive on campus....Due to cultural differences, you may feel somewhat confused when talking with fellow students. “What do they mean?” Communication in Africa is inferential rather than direct, so you will need to become adept at listening for what is being communicated between the lines.... Students at AIU are coming from all over Africa and the world. They will appreciate the time you invest in learning about the uniqueness of their own cultures—e.g. what communicates respect.

Maelezo na mawaidha haya yanahusiana na yaliyomo katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ni masuala yasiyokwepeka, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Yanawahusu sio tu wanafunzi, bali pia wafanya biashara, wanadiplomasia, na kadhalika, kama ninavyoelezea mara kwa mara katika blogu hii.

Thursday, April 27, 2017

Bendera ya Tanzania Kupepea Rochester, Minnesota

Kwa mara ya kwanza bendera ya Tanzania itapeperushwa katika tamasha la kimataifa mjini Rochester, Minnesota, tarehe 29 mwezi huu. Hili ni tamasha linaloandaliwa na Rochester International Association (RIA) kila mwaka. Nimewahi kuelezea kuhusu tamasha hili katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Napenda kuelezea mchakato uliowezesha bendera ya Tanzania kupewa hadhi hiyo. Mwaka jana wa-Kenya wawili, Olivia Njogu na Kennedy Ombaye, ambao ni wanabodi wa RIA, waliniambia kuwa wangependa nijiunge nao. Niliguswa na wazo lao, nikaafiki. Waliwasilisha ujumbe kwa mwenyekiti wa bodi, Brian Faloon, nami nikawasiliana naye kumthibitishia utayari wangu wa kujiunga. Wazo lilipitishwa na bodi, nami nikajiunga.

Wiki chache zilizopita, bodi ilianza kujadili mipango ya tamasha la kimataifa kwa mwaka huu. Wakati suala la bendera lilipojadiliwa, mwanabodi Olivia Njogu aliniambia kuwa iwepo bendera ya Tanzania. Kwa kuwa sikuelewa utaratibu wa bendera ukoje, Olivia na wanabodi wengine walinihakikishia kuwa sitahitaji kuileta bendera, bali wataipata kwa muuzaji. Nilifahamu kuwa utaratibu wa tamasha ni kuwa linapoanza, panakuwa na maandamano ya watu wakiwa wamebeba bendera za nchi mbali mbali.

Mwaka jana niliposhiriki tamasha hili, nilikuwa na bendera ya Tanzania, ambayo nilikuwa nimeinunua mwaka juzi, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Lakini kwa kuwa nilikuwa bado mgeni katika tamasha hili, sikuwa nimefanya utaratibu wa kuijumlisha katika maandamano ya bendera. Niliitandaza kwenye meza yangu, kama inavyoonekana pichani hapa kushoto.

Ninawashukuru tena wa-Kenya kwa urafiki na ukarimu ambao wamenionyesha tangu nilipokwenda nchini kwao kufanya utafiti, kuanzia mwaka 1989, hadi miaka yote niliyoishi huku Marekani. Jambo hili nimekuwa nikilitaja katika blogu hii.

Thursday, November 24, 2016

"A Far Cry From Africa," Shairi la Derek Walcott

Tangu nilipoanza kufundisha katika chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimepata fursa ya kusoma na kufundisha fasihi iliyoandikwa kwa ki-Ingereza kutoka sehemu mbali mbali ulimwenguni, kwa kiwango kikubwa kuliko ilivyowezekana nilipokuwa ninafundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwandishi mmojawapo ambaye kazi zake nimezishughulikia sana ni Derek Walcott wa St. Lucia, pande za Caribbean, maarufu kwa utunzi wa mashairi na tamthilia, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 1992.

Nimesoma na kufundisha mashairi yake mengi na tamthilia zake kadhaa. Moja ya mashairi hayo ni "A Far Cry From Africa," ambalo lilichapishwa mwaka 1962. Linaelezea mahuzuniko juu ya vita ya Mau Mau nchini Kenya iliyodumu kuanzia mwaka 1952 hadi 1960. Masetla wazungu walipigana na wa-Afrika waliotaka kuchukua ardhi yao iliyoporwa. Kwa kuwa Derek Walcott ni chotara, damu ya kizungu na ki-Afrika, alihisi vita hiyo ikitokea ndani ya nafsi yake. Uhasama na ukatili wa pande hizo mbili aliuhisi mithili ya sumu katika mishipa ya damu yake. Alijihisi kama mateka aliyekosa namna ya kujinasua.

Walcott anaimudu lugha ya ki-Ingereza kwa namna inayonikumbusha umahiri wa Shakespeare. Nitafurahi iwapo nitapata ujasiri wa kujaribu kulitafsiri shairi kwa ki-Swahili.
-------------------------------------------------------------------------------

A Far Cry From Africa

Derek Walcott


A wind is ruffling the tawny pelt 
Of Africa, Kikuyu, quick as flies, 
Batten upon the bloodstreams of the veldt. 
Corpses are scattered through a paradise. 
Only the worm, colonel of carrion, cries: 
'Waste no compassion on these separate dead!' 
Statistics justify and scholars seize 
The salients of colonial policy. 
What is that to the white child hacked in bed? 
To savages, expendable as Jews?

Threshed out by beaters, the long rushes break 
In a white dust of ibises whose cries 
Have wheeled since civilizations dawn 
From the parched river or beast-teeming plain. 
The violence of beast on beast is read 
As natural law, but upright man 
Seeks his divinity by inflicting pain. 
Delirious as these worried beasts, his wars 
Dance to the tightened carcass of a drum, 
While he calls courage still that native dread 
Of the white peace contracted by the dead. 

Again brutish necessity wipes its hands 
Upon the napkin of a dirty cause, again 
A waste of our compassion, as with Spain, 
The gorilla wrestles with the superman. 
I who am poisoned with the blood of both, 
Where shall I turn, divided to the vein? 
I who have cursed 
The drunken officer of British rule, how choose 
Between this Africa and the English tongue I love? 
Betray them both, or give back what they give? 
How can I face such slaughter and be cool? 
How can I turn from Africa and live?

Wednesday, December 30, 2015

Nimekutana na Mdau wa Miaka Mingi

Leo nimekutana na mdau wangu wa miaka mingi, Dr. Barbara Poole Galyen, ambaye anaishi California. Kwa siku chache hizi za Krismasi na Mwaka Mpya, yuko hapa Minnesota kwa ndugu zake. Kwa kupitia facebook tuliwasiliana na leo nilikwenda mjini Lakeville alikofikia.

Dr. Galyen na mimi tulifahamiana mwaka 1995, wakati nilipokuwa natafiti masimulizi ya jadi na tamaduni mkoani Mwanza. Utafiti huo ambao nilifanya tangu mwaka 1993 hadi 1996 uligharamiwa na shirika la Earthwatch. Dr. Galyen alikuwa mmoja wa watu kutoka nchi mbali mbali waliokuwa wanakuja Tanzania kushiriki utafiti wangu. Yeye alikuja wakati wa utafiti kisiwani Ukerewe.

Kwa kauli yake mwenyewe, huu ulikuwa mwanzo na msingi wa yeye kuipenda Afrika, hadi akaenda kufanya kazi Kenya katika United States International University, ambapo nilimtembelea mwaka 1997. Hatimaye alianzisha kampuni ya ushauri kuhusu masuala tamaduni ulimwenguni. Shughuli hizi, ambazo zinafanana na zangu, zimempa fursa ya kuzunguka sehemu mbali mbali za dunia na kujenga mtandao wa kimataifa wa washiriki.

Leo imekuwa furaha kubwa kuonana tena baada ya miaka mingi, kubadilishana mawazo na kupiga michapo. Nilimchukulia nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambamo nimegusia mambo yaliyotokana na utafiti wangu wa Earthwatch.

Dr. Galyen mwenyewe katika ukurasa wake wa facebook, ameandika kuhusu kukutana kwetu leo:

I enjoyed a wonderful visit with Dr. Joseph Mbele who was the one who originally introduced me to Africa in 1995 on an "Earthwatch" adventure. I give him credit for changing my life completely after I moved to Kenya as a result of our fascinating studies on a remote island in Lake Victoria, TZ. Born in Tanzania, Dr. Mbele is currently a professor at St. Olaf College in MN where he continues to work on special projects around the world! He's inspiring me again to get more involved in heart-felt projects globally.

Monday, October 12, 2015

Kama Mwandishi, Ninawaenzi wa-Kenya

Mimi kama mwandishi, ninawaenzi wa-Kenya. Naandika kutokana na uzoefu wangu. Tena na tena, mwaka hadi mwaka, nimeshuhudia wa-Kenya wakifuatilia vitabu vyangu. Wamekuwa bega kwa bega nami kama wasomaji wangu.

Tangu nilipochapisha kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, wa-Kenya walikichangamkia. Ndugu Tom Gitaa, mmiliki wa gazeti la Mshale aliandaa mkutano kuniwezesha kukitambulisha kitabu hicho, kama ilivyoelezwa katika taarifa hii.

Kati ya watu waliohudhuria alikuwepo Julia Opoti, m-Kenya mwingine, ambaye alishajipambanua kama mpiga debe wa kitabu hiki. Siku hiyo alimleta rafiki yake m-Kenya, Dorothy Rombo, naye akapata kunifahamu na kukifahamu kitabu changu.

Julia hakuishia hapo. Siku moja ulifanyika mkutano mkubwa wa wa-Kenya hapa Minnesota, ambao uliwakutanisha wana-diaspora wa Kenya na viongozi mbali mbali waliofika kutoka Kenya ili kuongelea fursa zilizopo nchini kwao katika uwekezaji na maendeleo kwa ujumla, na namna wana-diaspora wanavyoweza kushirikiana na wenzao walioko nyumbani.

Nilihudhuria mkutano ule sambamba na wengine waliokuwa wanaonesha bidhaa na huduma zao. Nilikuwa na meza ya vitabu vyangu. Julia alimleta ofisa wa ubalozi wa Kenya, Washington DC kwenye meza yangu, akatutambulisha. Alimwelezea kuhusu kitabu changu cha Africans Americans: Embracing Cultural Differences, naye akanunua nakala. Baada ya siku kadhaa aliniandikia ujumbe kama nilivyoandika katika blogu hii. Maneno ya afisa huyu yalinigusa, na baadhi ni haya:

Kuhusu kitabu chako, hivi sasa nafikiri kimesomwa na watu kadri ya watano hapa ubalozi wetu na kimependwa sana. Ni matumaini yangu kuwa ukipata wasaa mzuri utaandika vitabu zaidi katika fani hii ili upate kunufaisha watu juu ya swali hili muhimu la tafauti ya mila na utamaduni

Siku nyingine nilikuwa natoa mhadhara katika Chuo cha Principia. Aliyeanzisha mchakato wa kunialika ni m-Kenya ambaye alikuwa amesoma taarifa zangu mtandaoni. Mama mmoja m-Kenya aliyehudhuria aliamua kuniunganisha na jamii ya wa-Kenya wa Kansas City, ambako alikuwa anaishi, ili niweze kwenda kutoa mhadhara. Mipango ilikamilika nikaenda, kama nilivyoelezea hapa.

Mara kwa mara, nimeona jinsi wa-Kenya wanavyojitokeza katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki. Katika Afrifest, kwa mfano, hawakosekani. Nimewahi kuelezea jambo hilo, miaka michache iliyopita na mwaka jana.

Nimeona niandike taarifa hii kwa kuwa naguswa na tabia za majirani zetu hao wa-Kenya. Walinifanyia ukarimu mkubwa nilipokuwa nafanya utafiti nchini mwao baina ya mwaka 1989 na 1991, hata kunialika kutoa mihadhara kuhusu utafiti wangu. Naendelea kuguswa na moyo wao huku ughaibuni. Nimejithibitishia kuwa wanaheshimu taaluma, nami nawaheshimu kwa hilo. Nategemea kuandika zaidi kuhusu suala hilo hapa katika blogu yangu.

Wednesday, May 6, 2015

Leo Nimepata Bendera ya Tanzania

Leo nimepata bendera ya Tanzania. Niliwahi kuandika katika blogu hii kuwa mara kwa mara ninashiriki matamasha hapa Marekani ambapo watu huja na bendera za nchi zao, nami nilijisikia vibaya kwa kutokuwa na bendera kubwa ya nchi yangu. Nilifanya uamuzi muafaka, nikaagiza, na leo nimeipata.

Mwaka jana, nilipoandika ujumbe wangu, nilikuwa napeleleza katika tovuti kadhaa zinazouza bendera. Lakini safari hii, kwa kubahatisha tu, nimeingia katika tovuti ya Amazon nikaona bendera ziko, tena kwa bei rahisi sana.




Nimejionea hapa Marekani jinsi wa-Kenya walivyo hodari kwa suala hilo, na hapa naleta picha niliyopiga katika tamasha la Afrifest, tarehe 2 Agosti, mwaka jana, mjini Brooklyn Park, Minnesota. Inamwonyesha m-Kenya akitamba na bendera ya nchi yake.

Jiulize mwenyewe, ungejisikiaje kuwepo mahali ambapo wenzako wanatamba na bendera za nchi zao, nawe huna. Kwa nini ukae mahali hivyo, kama vile huna nchi? Hisia hizi ni kubwa unapokuwa ughaibuni. Sikutaka kuendelea kudhalilika namna hiyo.



Picha nyingine, inayoonekana hapa kushoto, nilipiga tarehe 11 Aprili, 2015, mjini Rochester, Minnesota, kwenye tamasha la tamaduni za ulimwengu. Inaonyesha meza ya wa-Kenya na bendera yao.

Kuna matamasha yanayokuja ambayo nitashiriki, kama vile tamasha la Afrifest, tarehe 1 Agosti, 2015. Nitakapokuwa naandika taarifa za matamasha hayo na maonesho, wadau mtajionea wenyewe bendera ya Tanzania ikipepea kwenye eneo la meza ya vitabu vyangu.

Saturday, December 8, 2012

Simba wa Tsavo

Leo napenda kuongelea habari ya simba wa Tsavo. Ni habari iliyokuwa inatusisimua sana tulipokuwa shuleni, baina ya darasa la tano na la nane. Kulikuwa na kitabu, Simba wa Tsavo, ambacho kilichapishwa mwaka 1966. Ni tafsiri ya kitabu cha J.H. Patterson kilichoitwa The Man Eaters of Tsavo.

Kitabu hiki kilielezea matukio ya kutisha wakati ujenzi wa daraja la reli kwenye mto Tsavo, nchini Kenya, miaka mia na kitu iliyopita. Kilielezea namna simba walivyokuwa wakiwavizia, kuwadaka na kuwaua wafanya kazi kwenye eneo la hili daraja wakawaua watu zaidi ya mia, hadi, hatimaye, Patterson alipofanikiwa kuwaua, mwezi Desemba 1898. Hiyo ndio habari tuliyosoma tukiwa shuleni, miaka hiyo ya sitini na kitu.

Lakini, kwa miaka hii ya karibuni, yapata miaka kumi, nimekutana na taarifa nyingine nyingi kuhusu simba wa Tsavo. Je, unajua wale simba waliishia wapi? Katika kusoma habari za mwandishi Ernest Hemingway, ambaye alizaliwa mwaka 1899 eneo la jirani na Chicago, nimegundua kuwa alipokuwa mtoto alipelekwa na baba yake katika hifadhi ya Field Museum of Natural History mjini Chicago. Hapo alipata kuziona maiti za wanyama mbali mbali kutoka Afrika ambazo zilikuwa zimehifadhiwa kitaalam ili zionekane kama vile ni wanyama hai.

Kati ya wanyama hao ni wale simba wa Tsavo, ambao picha yao inaonekana hapa juu. Habari hii ilinishtua sana, kwani sikujua kabisa kuwa simba wa Tsavo wamehifadhiwa na kwamba wako Chicago. Hiyo ni faida ya wazi ya kusoma vitabu, kwamba mtu unagundua mambo ambayo hukuyajua. Pamoja na kuangalia wanyama hao waliohifadhiwa, mtoto Hemingway alisoma kitabu cha The Man Eaters of Tsavo. Hayo yote yalichangia katika kumjengea Hemingway mapenzi makubwa aliyokuwa nayo juu ya Afrika kwa maisha yake yote.

Mwaka 1933, Hemingway na mke wake Pauline walifunga safari wakitokea Ulaya, wakaja Afrika Mashariki. Walishuka meli Mombasa, wakapanda treni kuelekea Nairobi. Walipita Tsavo, wakaenda hadi Machakos, kisha Tanganyika. Kuhusu safari yake ya Tanganyika, Hemingway aliandika kitabu maarufu kiitwacho Green Hills of Africa, ambacho ni kimoja ya vitabu vyake ambavyo nimevisoma na kuwafundisha wanafunzi.

Thursday, May 5, 2011

Mitaani Namanga, 2007

Ingawa mdogo, mji wa Namanga ni maarufu, kwa vile uko mpakani. Hapa naonekana nikiwa Namanga, upande wa Tanzania. Naelekea kwenye geti la mpaka, hatua chache mbele yangu. Kule mbali unaona Mlima Longido. Barabara inapita kulia kwake, inaingia Longido, nyuma ya mlima, na kuelekea Arusha.

Hii ni moja ya hoteli ambapo napenda kufikia, kwa Bwana Minja, kupata chakula na kinywaji. Nimeshalala hapo.








Nilipendezwa na mpangilio wa nyumba hizi na ile
milima. Hizi nyumba ziko mwanzoni mwa mji wa Namanga, kabla hujafika kwenye geti la mpaka baina ya Kenya na Tanzania.







Nilikuwa Namanga na kikundi cha wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado na mwalimu wao, ambao walifika Tanzania katika kozi niliyoiunda, kuhusu mwandishi Hemingway. Hao ni wanafunzi waanzilishi wa kozi hii. Napangia kuibadili kidogo na kuiweka katika program ya Chuo cha St. Olaf.

Hapa nipo upande wa Kenya. Kama mdau unavyoona, mapokezi hayakuwa haba. Ndio mambo ya ujirani mwema hayo.








Namanga, kama ilivyo miji mingine, ina sehemu nyingi ambapo unaweza kupumzika, na kujipatia chakula na pia kukata kiu baada ya mizunguko yako mitaani.

Monday, November 22, 2010

Kitabu Kilivyopokelewa Ubalozi wa Kenya

Mwaka 2007 mwanzoni, jumuia ya wa-Kenya wanaoishi Minnesota waliandaa mkutano kuhusu uwekezaji nchini kwao. Walihudhuria wa-Kenya wengi sana, wakiwemo maofisa wa serikali na taasisi mbali mbali waliofika kutoka Nairobi. Nilishiriki, nikiwa na meza ambapo niliweka vitabu vyangu na machapisho mengine.

Nilikutana na wa-Kenya wengi, baadhi ambao tulifahamiana kabla na wengine kwa mara ya kwanza. Mmoja wa hao tuliofahamiana kabla alikuwa Julia Opoti, ambaye ni mwanahabari anayeendelea kujipatia umaarufu, na ni shabiki wa siku nyingi wa maandishi yangu. Alikuja kwenye meza yangu akiwa na bwana mmoja, akatutambulisha.

Yule bwana alikuwa afisa katika ubalozi wa Kenya, Washington DC. Julia alikuwa amemwambia kuhusu kitabu cha Africans and Americans naye akakinunua. Tarehe 17 Aprili, yule afisa aliniandikia ujumbe huu:

Kuhusu kitabu chako, hivi sasa nafikiri kimesomwa na watu kadri ya watano hapa ubalozi wetu na kimependwa sana. Ni matumaini yangu kuwa ukipata wasaa mzuri utaandika vitabu zaidi katika fani hii ili upate kunufaisha watu juu ya swali hili muhimu la tafauti ya mila na utamaduni.


Ujumbe huu, ingawa ulinifurahisha, haukunishangaza, kwa sababu ninafahamu jinsi wa-Kenya wanavyothamini vitabu na elimu kwa ujumla. Nimefahamu jambo hilo tangu nilipoanza kutembelea Kenya, mwaka 1989, na katika kuwaona huku ughaibuni. Nimeshasema hivyo hata katika kitabu changu cha CHANGAMOTO. Jambo la pili ni kuwa nilivutiwa na wito kuwa niendelee kuandika, wito ambao nimeupata kutoka kwa wasomaji wengine pia. Naendelea kuandika.

Thursday, April 22, 2010

Kenya Yaondoa Vibali vya Kazi

Kuna taarifa kuwa Kenya inaondoa vibali vya kazi kwa raia wa Afrika Mashariki wanaotaka kufanya kazi Kenya. Bofya hapa. Sijui wa-Tanzania wanaipokeaje habari hii, lakini binafsi sishangai, kwani naifahamu Kenya kiasi fulani, na nafahamu kuwa wa-Kenya sio tu wamejiandaa kwa ushindani bali wanajiamini.

Tatizo liko upande wa wa-Tanzania. Kwa miaka mingi sana, labda kuanzia miaka ya themanini na kitu, wa-Tanzania wamekuwa na tabia ya kupuuzia elimu. Shuleni wanatafuta njia za mkato badala ya kusoma sana, ndani na nje ya yale yanafundishwa.

Wakishamaliza shule (ambayo ni dhana ya kipuuzi, kwani shule haimaliziki), wanaona kusoma ni kero. Sijui kuna wa-Tanzania wangapi wanaonunua vitabu na kuvisoma, au wanaoenda maktaba na kujisomea tu, au wana vitabu majumbani na wanavisoma, au wanashirikiana na watoto wao katika kusoma vitabu.

Binafsi, nimeandika kwa miaka mingi nikiwalalamikia wa-Tanzania kwa tabia hizo, na nimeelezea sana nilivyoona tofauti baina ya Tanzania na Kenya, tangu nilipoanza kutembelea Kenya, mwaka 1989.

Nimeelezea mara kwa mara kuwa hata huku ughaibuni, wa-Tanzania hawafanani na wenzetu wa nchi zingine za Afrika. Siwaoni wa-Tanzania kwenye tamasha za vitabu au kwenye maduka ya vitabu. Siwaoni wa-Tanzania wanaomiliki maduka ya vitabu au magazeti. Lakini wenzetu, kama vile wa-Kenya au Wanigeria, wamo katika shughuli hizi.

Watanzania ni wapenda ulabu na starehe, wawe Tanzania au ughaibuni. Hayo nimesema sana kwenye kumbi mbali mbali, na kwenye blogu zangu, na hata kwenye kitabu ambacho nimechapisha mwaka jana, kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii

Sasa basi, katika huu utandawazi, ni wazi wa-Kenya wanajiamini zaidi na hawatishiki kama wanavyotishika wa-Tanzania. Wa-Kenya wamejiandaa zaidi kielimu na wanaweza kujieleza. Watanzania wengi wanawapeleka watoto wao kusoma Kenya, na wa-Kenya wanazidi kuchukua ajira hata nchini Tanzania. Kwa hali ilivyo, wataendelea kuchukua ajira, iwe ni kwao au kwetu, au sehemu nyingine duniani. Wa-Kenya wamejiandaa kiasi kwamba hata fursa za kufundisha ki-Swahili huku ughaibuni wanazichukua zaidi wao.

Wahenga walisema kuwa asiyefunzwa na mama yake, hufunzwa na ulimwengu. Ndio yatakayowapata wa-Tanzania, katika ulimwengu huu wa utandawazi.

Siku za karibuni nitakuwa Tanzania nikiendesha warsha kuhusu masuala ya aina hiyo. Warsha mbili nitafanyia Arusha, tarehe 3 Julai, na nyingine tarehe 10 Julai. Nilishawahi kutangaza katika blogu hii. Lakini, sina hakika kama ni wa-Tanzania wangapi watakaohudhuria. Ila nina hakika wageni watahudhuria, ili mradi wapate taarifa.

Mimi kama mwalimu, siwezi kumezea au kuendekeza uzembe kama huu walio nao wa-Tanzania, ambao wanatumia pesa nyingi sana kwenye sherehe na bia, lakini kununua kitabu cha shilingi elfu saba hawakubali, wala kutumia saa mbili kwa wiki wakisoma maktabani hawawazii, uzembe ambao unawafanya wawe wanatoa visingizio kila siku, au lawama kwa wengine, hasa serikali, wakati wao wenyewe hawawajibiki.

Kama nilivyogusia, hakuna jipya ambalo nimesema hapa juu, bali ni marudio ya yale ambaye nimekuwa nasema kwa muda mrefu, katika blogu hii na kwingineko.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...