Showing posts with label Msomaji. Show all posts
Showing posts with label Msomaji. Show all posts

Thursday, October 12, 2017

Profesa Amekifurahia Kitabu

Ni kawaida yangu, kuchapisha maoni ya wasomaji wa vitabu vyangu. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa profesa moja ambaye alihudhuria mkutano wa Africa Network nilioshiriki kuuandaa hapa chuoni St. Olaf.

Profesa huyu Mmarekani anawapeleka wanafunzi wa ki-Marekani Kenya na Rwanda. Katika mkutano wetu, aliongelea programu hiyo, akielezea jinsi tofauti za tamaduni zinavyojitokeza.

Nilivutiwa na mhadhara wake, kwa kuwa nami ni mzoefu wa programu hizi za kupeleka wanafunzi Afrika, ikiwemo Tanzania. Nilimpelekea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, naye ameniandika ujumbe huu:

Dear Joseph,
There were several wonderful things that came from my attending the Africa Network conference. Meeting you and learning more is one. I just finished your book and enjoyed it so much. It made me laugh out loud and understand my Kenyan teaching colleague even more. I have been both to Rwanda and Kenya many times and am aware of many of the situations and misunderstandings you describe. I’ve shared my thoughts with Kitito and we hope to use your book in some way for our spring Cultural Identity course. 
Thanks again.

Ninashukuru kwamba kitabu hiki kinatoa mchango ambao nilipangia nilipokiandika, ikiwemo kuwaelimisha wanaohusika na programu za kupeleka wanafunzi Afrika. Msukumo wa kukiandika ulitoka katika mikutano ya jumuia ya vyuo iitwayo Associated Colleges of the Midwest (ACM), na baada ya kukichapisha, wahusika wa programu zingine nao wanakitumia. Mifano ni programu ya  chuo kikuu cha Wisconsin-Oshkosh na pia program ya chuo cha Gustavus Adolphus, ambayo nimeitaja mara kwa mara katika blogu hii.


Sunday, October 23, 2016

Siku ya Mashujaa wa Kenya, Rochester, Minnesota

Jana nilikwenda mjini Rochester, Minnesota, kuhudhuria sherehe ya siku ya Mashujaa wa Kenya. Hii ni sikukuu ambayo wa-Kenya huifanya kila mwaka tarehe 20 Oktoba, kuwakumbuka mashujaa wa tangu enzi za kupigania uhuru hadi leo. Sherehe ya jana iliandaliwa na jumuia ya wa-Kenya waishio Rochester.

Nilipata taarifa ya sikukuu hii kutoka kwa Olivia Njogu, m-Kenya aishiye Rochester, na mwanabodi wa Rochester International Association. Anaonekana pichani hapa kushoto, wa pili kutoka kulia. Chama hiki huandaa tamasha la kimataifa kila mwaka, na Olivia tulifahamiana niliposhiriki tamasha hilo mwaka huu, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Baada ya tamasha, Olivia alisoma kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na kisha akaniandikia kunielezea alivyokipenda. Taarifa hiyo niliiandika katika blogu hii.

 .


Hii haikuwa mara yangu ya kwanza kuhudhuria sherehe za wa-Kenya hapa Marekani. Daima nimependezwa kujumuika nao, kama nilivyowahi kuandika katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Hali ilikuwa hivyo hivyo jana. Nilivyokuwa ninapaki gari kwenye eneo la sherehe, walikuja wa-Kenya kadhaa kunipokea, ingawa hatukuwa tunafahamiana. Tulitambulishana na hima tukazama katika maongezi ya dhati na michapo.













Hii ilikuwa ni sherehe iliyojumuisha watoto vijana na watu wazima. Pamoja na maongezi yasiyo kikomo, vicheko na chereko, kulikuwa na vyakula tele na muziki. Nilivutiwa kwa namna ya pekee na muziki wa Kenya, nikakumbuka safari zangu za Kenya kuanzia mwaka 1989, za utafiti juu ya tungo za zamani na utamaduni wa wa-Swahili.














Picha hapa kushoto ni ushahidi wa hali ya furaha iliyotawala.






























Wengi waliohudhurua sherehe ya jana sikuwa nimefahamiana nao kabla, ingawa wachache walinikumbuka kwa kuwa waliniona katika tamasha la kimataifa la Rochester la mwaka huu.

Sherehe hii haikuwa ya wa-Kenya pekee. Ingawa sikuweza kuongea na kila mtu, nilipata fursa ya kuongea na watu wawili wa mataifa mengine: mmoja kutoka Nigeria na mwingine kutoka Uganda.




Katika kuishi kwangu hapa Minnesota, nimeweza kufahamiana na wa-Afrika wengi waishio Minneapolis, St. Paul, na maeneo ya jirani. Sasa ninafurahi kuweza kujenga mtandao wa aina hiyo maeneo ya Rochester.

Wanadiaspora wa Afrika tuna wajibu wa kujenga mshikamano miongoni mwetu, kama msingi wa ushirikiano katika bara letu. Waliotutangulia huku ughaibuni, kama akina Peter Abrahams, Jomo Kenyatta, na Kwame Nkrumah walifanya hivyo. Kwangu kama mwandishi na mwalimu, hizi zote ni fursa za kielimu. Darasa ni popote, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.


Thursday, February 5, 2015

Kitabu Kimemgusa Mdau wa Bangladesh

Leo asubuhi nimepigiwa simu na mama mmoja kutoka Bangladesh anayefanya kazi katika benki ninayoitumia. Wiki kadhaa zilizopita, baada ya kufahamu kuwa hakuwa amekaa sana hapa Marekani, nilimwazimisha nakala ya kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ili aone mambo yalivyokuwa kwangu katika utamaduni huu mgeni. Nilihisi kuwa kingemsaidia kwa namna moja au nyingine.

Siku nyingine, nilipokwenda benki kwa shughuli zangu, tulionana, na aliniambia kuwa kitabu amekipenda, ila kilikuwa nyumbani. Basi nilimwambia kuwa tutafanya mpango nikichukue siku nyingine.

Jana nilimpigia simu kazini kwake, na kwa vile hakuwepo, niliacha ujumbe kwenye simu kwamba ninashiriki maonesho Jumamosi hii na, ikiwezekana, ningechukua kile kitabu; la sivyo, akitaka, anaweza kukilipia katika akaunti yangu na kukichukua moja kwa moja.

Leo asubuhi amenipigia simu, tukaongelea suala la kitabu. Alisema amekipenda na angetaka kumpelekea kaka yake aliyeko Canada, ila sasa hajui itakuwaje kwa vile ninakihitaji kwenye maonesho. Nilimwambia kuwa nina nakala zingine ambazo nadhani zitatosha, naye alisema atalipia kitabu. Nilimshukuru, nikamwuliza iwapo tutaweza kupanga siku tukutane, ili anieleze mawazo yake kuhusu yaliyomo kitabuni. Alikubali hima.

Nimeona niandike kumbukumbu hizi, kama ilivyo kawaida katika hii blogu yangu. Tangu siku ya kwanza mama huyu aliponiambia kuwa kitabu amekipenda, nilitambua kuwa ingawa niliandika kuhusu utamaduni wa mu-Afrika, kitabu kinawagusa watu wasio wa-Afrika pia.

Hili halikuwa jambo la ajabu kwangu, kwani katika kufundisha fasihi za sehemu mbali mbali za dunia, napata fursa ya kuyaelewa mambo kadha wa kadha ya tamaduni hizo. Nimegusia jambo hilo katika utangulizi wa kitabu changu.

Hata hivi, ingawa kusoma fasihi kutoka nchi fulani ni fursa ya kuufahamu utamaduni wa nchi ile, kuongea ana kwa ana na mtu au watu wa nchi ile ni fursa ya aina yake. Nami nangojea kwa hamu kuongea na huyu mama wa Bangladesh kuhusu kitabu changu na utamaduni wa kwao. Ninahisi nitajifunza mengi.

Thursday, August 26, 2010

Ujumbe wa Msomaji wa Kitabu

Naichukulia blogu hii kama mahali ambapo naweka mambo yangu binafsi: kumbukumbu, fikra, dukuduku, hisia na kadhalika. Ingawa najua watu wanasoma ninayoandika, siwezi kusema kuwa wao ndio walengwa. Ninajiandikia mwenyewe, kwa uhuru na namna ninayotaka, mambo yangu binafsi.

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mshiriki mmojawapo wa warsha niliyoendesha Dar es Salaam mwaka jana. Bofya hapa. Ameniulizia naenda lini kutoa warsha zingine akahudhurie.

Pia amesema kuwa kitabu cha Africans and Americans ambacho alikinunua wakati wa warsha kinamsaidia katika kutoa mihadhara na kushughulikia masuala mengine ya mahusiano sehemu za kazi.

Ni wazi nimefurahi kusikia hayo. Nani asingefurahi? Nimemwambia nafarijika kuwa kitabu kimezaa matunda mema kwake, hasa nikikumbuka gharama ya warsha na kitabu. Lengo moja la kuandika kitabu hiki lilikuwa kuwasaidia wanaohitajika kutoa mihadhara kuhusu tofauti za tamaduni na matatizo na changamoto zitokanazo na tofauti hizi. Wengine wanakuwa na majukumu ya kusuluhisha migogoro. Mimi mwenyewe nakitumia kitabu hiki, mahali pa kuanzia.

Maoni ya wasomaji ni msaada mkubwa kwa mwandishi. Nami nina bahati ya kuyapata mara kwa mara. Wengine, kama ilivyo katika ulimwengu wa vitabu, wanayaweka maoni yao hadharani, kama haya hapa. Nawajibika kutoa shukrani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...