Thursday, February 5, 2015

Kitabu Kimemgusa Mdau wa Bangladesh

Leo asubuhi nimepigiwa simu na mama mmoja kutoka Bangladesh anayefanya kazi katika benki ninayoitumia. Wiki kadhaa zilizopita, baada ya kufahamu kuwa hakuwa amekaa sana hapa Marekani, nilimwazimisha nakala ya kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ili aone mambo yalivyokuwa kwangu katika utamaduni huu mgeni. Nilihisi kuwa kingemsaidia kwa namna moja au nyingine.

Siku nyingine, nilipokwenda benki kwa shughuli zangu, tulionana, na aliniambia kuwa kitabu amekipenda, ila kilikuwa nyumbani. Basi nilimwambia kuwa tutafanya mpango nikichukue siku nyingine.

Jana nilimpigia simu kazini kwake, na kwa vile hakuwepo, niliacha ujumbe kwenye simu kwamba ninashiriki maonesho Jumamosi hii na, ikiwezekana, ningechukua kile kitabu; la sivyo, akitaka, anaweza kukilipia katika akaunti yangu na kukichukua moja kwa moja.

Leo asubuhi amenipigia simu, tukaongelea suala la kitabu. Alisema amekipenda na angetaka kumpelekea kaka yake aliyeko Canada, ila sasa hajui itakuwaje kwa vile ninakihitaji kwenye maonesho. Nilimwambia kuwa nina nakala zingine ambazo nadhani zitatosha, naye alisema atalipia kitabu. Nilimshukuru, nikamwuliza iwapo tutaweza kupanga siku tukutane, ili anieleze mawazo yake kuhusu yaliyomo kitabuni. Alikubali hima.

Nimeona niandike kumbukumbu hizi, kama ilivyo kawaida katika hii blogu yangu. Tangu siku ya kwanza mama huyu aliponiambia kuwa kitabu amekipenda, nilitambua kuwa ingawa niliandika kuhusu utamaduni wa mu-Afrika, kitabu kinawagusa watu wasio wa-Afrika pia.

Hili halikuwa jambo la ajabu kwangu, kwani katika kufundisha fasihi za sehemu mbali mbali za dunia, napata fursa ya kuyaelewa mambo kadha wa kadha ya tamaduni hizo. Nimegusia jambo hilo katika utangulizi wa kitabu changu.

Hata hivi, ingawa kusoma fasihi kutoka nchi fulani ni fursa ya kuufahamu utamaduni wa nchi ile, kuongea ana kwa ana na mtu au watu wa nchi ile ni fursa ya aina yake. Nami nangojea kwa hamu kuongea na huyu mama wa Bangladesh kuhusu kitabu changu na utamaduni wa kwao. Ninahisi nitajifunza mengi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...