Showing posts with label Gustavus Adolphus College. Show all posts
Showing posts with label Gustavus Adolphus College. Show all posts

Thursday, October 12, 2017

Profesa Amekifurahia Kitabu

Ni kawaida yangu, kuchapisha maoni ya wasomaji wa vitabu vyangu. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa profesa moja ambaye alihudhuria mkutano wa Africa Network nilioshiriki kuuandaa hapa chuoni St. Olaf.

Profesa huyu Mmarekani anawapeleka wanafunzi wa ki-Marekani Kenya na Rwanda. Katika mkutano wetu, aliongelea programu hiyo, akielezea jinsi tofauti za tamaduni zinavyojitokeza.

Nilivutiwa na mhadhara wake, kwa kuwa nami ni mzoefu wa programu hizi za kupeleka wanafunzi Afrika, ikiwemo Tanzania. Nilimpelekea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, naye ameniandika ujumbe huu:

Dear Joseph,
There were several wonderful things that came from my attending the Africa Network conference. Meeting you and learning more is one. I just finished your book and enjoyed it so much. It made me laugh out loud and understand my Kenyan teaching colleague even more. I have been both to Rwanda and Kenya many times and am aware of many of the situations and misunderstandings you describe. I’ve shared my thoughts with Kitito and we hope to use your book in some way for our spring Cultural Identity course. 
Thanks again.

Ninashukuru kwamba kitabu hiki kinatoa mchango ambao nilipangia nilipokiandika, ikiwemo kuwaelimisha wanaohusika na programu za kupeleka wanafunzi Afrika. Msukumo wa kukiandika ulitoka katika mikutano ya jumuia ya vyuo iitwayo Associated Colleges of the Midwest (ACM), na baada ya kukichapisha, wahusika wa programu zingine nao wanakitumia. Mifano ni programu ya  chuo kikuu cha Wisconsin-Oshkosh na pia program ya chuo cha Gustavus Adolphus, ambayo nimeitaja mara kwa mara katika blogu hii.


Thursday, December 1, 2016

Maandalizi ya Wanachuo wa Gustavus Adolphus Waendao Tanzania

Jana nilipata ujumbe kutoka kwa Profesa Barbara Zust wa Chuo cha Gustavus Adolphus akiulizia iwapo nitaweza kwenda kuongea na wanafunzi wanaojiandaa kwenda naye Tanzania kwa safari ya kimasomo. Ameniambia kuwa watakuwa na kikao cha maandalizi ya safari tarehe 2 na 3 Januari, katika kituo cha mikutano cha Mount Olivet. Nimefanya mazungumzo hayo tena na tena miaka iliyopita.

Katika ujumbe wake, Profesa Zust amekumbushia kuwa, kama ilivyo jadi, wanafunzi hao watakuwa wameshasoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Pia amekumbushia jinsi wanafunzi wanavyoshukuru na kufurahia kwamba wanapokuwa Tanzania wanakutana na yale ambayo ninakuwa nimewaeleza kitabuni na katika mazungumzo.

Taarifa hii ni muhimu kwangu, na ndio maana ninaiweka hapa katika blogu yangu, kama kumbukumbu. Kwa kuzingatia umuhimu wa suala hili, nimeitika mwaliko wa Profesa Zust na kumwambia kuwa nitakwenda kukutana nao tarehe 2 Januari. Kama kawaida, panapo majaliwa, nitaandika taarifa katika blogu hii.

Wednesday, February 4, 2015

Wanachuo wa Gustavus Adolphus, Marekani, Wameifurahia Tanzania

Wanachuo wa Chuo cha Gustavus Adolphus, ambao walikuwa Tanzania mwezi Januari mwaka huu kwa ziara ya kimasomo, wamerejea salama nchini kwao Marekani. Hao ni wale ambao niliongea nao kuhusu tofauti baina ya utamaduni wa Marekani na ule wa kwetu Afrika, katika kuwaandaa kwa safari.

Jana, mmoja wao ameandika ujumbe katika blogu yangu ya ki-Ingereza:

Dr. Mbele,
Thank you very much for meeting with us before we left for Tanzania. We had a wonderful trip and learned so much about the differences and similarities between our two cultures. The Tanzanians are a beautiful people-- so full of happiness and passion for life. I will never forget my time there and hope that I can go back someday! Thanks you also for signing my copy of your book.
Abby Simms


Natafsiri ujumbe huu hivi:

Dr. Mbele,
Asante sana kwa kukutana nasi kabla hatujaondoka kwenda Tanzania. Safari yetu ilikuwa nzuri sana, na tulijifunza mengi kuhusu jinsi tamaduni zetu mbili zinavyofanana na jinsi zinavyotofautiana. Wa-Tanzania ni watu wazuri--wamejaa furaha na ari ya maisha. Sitasahau kamwe muda niliokuwepo kule na natumaini siku moja kwenda tena! Asante pia kwa kusaini nakala yangu ya kitabu chako.
Abby Simms.


Niliandika katika blogu hii kuwa hao wanachuo, kama walivyo wa-Marekani wengine, wana tabia ya kuripoti kuhusu safari na kukaa kwao Tanzania, nikaahidi kuwa nitakavyopata ripoti hizo, nitaziweka hapa katika blogu yangu.

Sidhani kama kuna m-Tanzania ambaye hatafurahi kusoma ripoti kama hii ya Abby Simms, kwa jinsi inavyotukumbusha kuwa tunayo mema na mazuri. Tukiamua, tunaweza kujibadili tukaachana na yale mabaya na tukaendeleza yale mema na mazuri.

Monday, January 5, 2015

Mkutano na Wanachuo wa Gustavus Adolphus

Leo asubuhi nilikwenda Mount Olivet Conference & Retreat Center, eneo la Farmington, hapa Minnesota, kuongea na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus ambao wanaelekea Tanzania kimasomo. Kwa siku hizi mbili tatu kabla ya safari yao, wamekuwa katika maandalizi, nami niliitwa na profesa wao Barbara Zust, kuongea nao kuhusu masuala ya utamaduni ambayo yamo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimeshaalikwa mara kadhaa miaka iliyopita, kuongea na wanachuo wa Gustavus Adolphus, katika maandalizi ya kwenda Tanzania, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Nilikuwa nimeamua kuwa leo, baada kutoa utangulizi mfupi, nitumie muda karibu wote katika kujibu masuali ya hao wanachuo, kwani nilishafahamishwa kuwa watakuwa wamekisoma kitabu changu. Ilidhihirika wazi, kutokana na masuali yao, kuwa walikuwa wamekisoma kwa makini. Wote tuliyafurahia mazungumzo yetu, ambayo yalidumu kuanzia saa nne hadi saa sita. Baada ya hapo, tulikula chakula cha mchana, ambapo niliendelea na maongezi na Profesa Zust na mshiriki wake Mchungaji Todd Mattson, na wanachuo ambao tulikaa meza moja.

Tulipokuwa tayari kwenda kula, na mara baada ya chakula, wanafunzi kadhaa waliniletea nakala zao za kitabu changu ili nisaini,shughuli ambayo ninaamini inamgusa kila mwandishi na yule anayesainiwa kitabu. Baada ya shughuli hii tuliagana, tukiwa tunapeana shukrani tele, nami nikaanza safari ya kurejea Northfield, ambapo ninaishi.

Katika picha ya mwanzo hapa juu, ninaonekana hapo mbele. Kule nyuma kabisa, upande wa kulia mwishoni, anaonekana Mchungaji Mattson, mwenye ndevu nyeupe, na mbele yake ni Profesa Zust. Pichani hapa kushoto, naonekana nikisaini kitabu cha mwanafunzi mojawapo.

Monday, December 22, 2014

Mkutano na Wanachuo wa Gustavus Adolphus Unakaribia

Siku zinakwenda haraka. Tarehe 5 Januari, ambayo imekaribia, ndio siku nitakayokutana na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus, kama nilivyoandika hapa. Hao ni wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya Tanzania, kujiongezea elimu kuhusu masuala ya afya na matibabu katika mazingira tofauti na ya Marekani, hasa kwa upande wa utamaduni.

Profesa wao aliniomba nikaongee nao kuhusu masuala ya aina hiyo kwa mapana kufuatia yale niliyoandika katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho watakuwa wamekisoma kabla ya mimi kukutana nao.

Kutokana na kusoma hiki kitabu, wanachuo hao watakuwa wameandaa masuali. Kama ilivyotokea siku zilizopita, masuali mengine yatazuka hapo hapo.

Jukumu hili linanifanya nikipitie tena kitabu changu, angalau kijuujuu, kwani sina mazoea ya kusoma sana yale ambayo nimeshayaandika na kuyachapisha. Napendelea kutumia muda wangu na akili yangu katika kutafiti, kutafakari na kuandika mambo mapya. Ingawa yale yaliyomo kitabuni sijayabadili, na sijaona sababu ya kuyabadili, ninafahamu mengi zaidi na naendelea kujifunza, kwani elimu haina mwisho.

Kutokana na ukweli huu, mazungumzo yangu na hao wanachuo wa safari hii hayawezi kuwa sawa na yale ya miaka iliyopita. Hata kama kutakuwa na masuali yanayofanana na yale ambayo nimeshaulizwa kabla, majibu yangu yatajengeka katika upeo mpana zaidi. Fursa za aina hii zinachangia kupanua upeo huo.

Tutakutana, kama siku zilizopita, Mount Olivet Conference & Retreat Center, pembeni mwa mji wa Lakeville, Minnesota. Nangojea kwa hamu kuonana tena na Profesa Zust, na kuonana na hao wanachuo wapya. Panapo majaliwa, nitaweka ripoti katika blogu hii, kama nilivyozoea.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...