Showing posts with label safari Tanzania. Show all posts
Showing posts with label safari Tanzania. Show all posts

Thursday, September 24, 2015

"Papa's Shadow" Yapongezwa na Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa

Tarehe 20 mwezi huu nilipeleka ujumbe Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa kuhusu filamu ya Papa's Shadow. Sikuandika ujumbe mrefu, bali niliwatumia kiunganishi hiki.

Bila kuchelewa, tarehe 22 nilipata ujumbe kutoka kwao, ukiwa umeandikwa na Ndugu Noel Kabanda. Uwakilishi unaafiki kuwa Papa's Shadow ni "fursa maridhawa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni" na unasisitiza kuwa "Serikali inatambua mchango wa sanaa katika kuitangaza Tanzania katika sekta mbali mbali ikiwemo utalii na utamaduni."

Kwanza, kwa kuzingatia uwingi wa majukumu yanayowakabili wawakilishi wetu katika balozi zetu, nimeona ni muhimu kusema nilivyoguswa na jinsi Uwakilishi ulivyoushughulikia ujumbe wangu.

Pili, ujumbe wa Uwakilishi unawatia moyo wahusika wa Ramble Pictures, ambao ndio watengeneaji wa Papa's Shadow. Timu nzima ya Ramble Pictures ni vijana wa ki-Marekani, na baadhi yao walikuja Tanzania mwaka 2013 kwenye kozi yangu ya Hemingway Katika Afrika Mashariki. Ni furaha kwangu, na jambo la kujivunia, kuwaeleza vijana hao kuwa Uwakilishi wa Kudumu waTanzania Umoja wa Mataifa umeipokea Papa's Shadow kwa namna hii.

Papa's Shadow si filamu ya maigizo. Ni filamu ya kuelimisha kuhusu mwandishi Ernest Hemingway. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni maongezi baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi Hemingway. Tunaongelea maisha ya Hemingway, safari zake, uandishi wake, na fikra zake kuhusu masuala mbali mbali. Tunawafungua macho walimwengu kuhusu namna Hemingway alivyoipenda Afrika na alivyokuwa mtetezi wa Afrika.

Hemingway alisafiri na kuishi Afrika Mashariki mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54. Aliandika hadithi, insha, barua na maandishi mengine ambayo ni hazina kubwa. Wenzetu katika nchi zingine ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari za huko, wametumia fursa hiyo kujitangaza, na wanawavutia watalii wengi sana. Mifano ni miji kama Paris (Ufaransa), Havana (Cuba), Oak Park (Illinois, Marekani), Key West (Florida, Marekani), na Pamplona (Hispania). Hemingway anapendwa ulimwenguni kote ambako watu wana utamaduni wa kusoma vitabu. Sina shaka kuwa Papa's Shadow italeta msisimko wa aina hiyo kwa kuwaelekeza mashabiki wa Hemingway nchini kwetu.

Hamu ya kuona Tanzania inafunguka macho kuhusu fursa hii ilinihamasisha kufanya utafiti juu ya safari za Hemingway katika nchi yetu na maandishi aliyoandika. Kozi niliyotunga ilikuwa na lengo hili. Nilitaka pia kuwasaidia walimwengu kuelewa umuhimu wa Afrika katika maisha na uandishi wa Hemingway. Kwa msingi huo huo, nilishiriki kikamilifu katika kufanikisha filamu ya Papa's Shadow.

Nimeeleza hayo yote ili kuweka wazi umuhimu wa ujumbe wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa. Ni mfano wa mshikamano unaotakiwa baina yetu wanadiaspora, serikali, na wananchi wenzetu.

Sunday, March 15, 2015

Darasa la "Hemingway in East Africa 2013" Kando ya Ziwa Babati

Mwezi Januari, 2013, nilikuwa Tanzania na wanafunzi kutoka Chuo cha St. Olaf katika kozi ya "Hemingway in East Africa."

Niliitunga kozi hii mwaka 2006, kwa ajili ya Chuo cha Colorado. Kwa miaka kadhaa, kabla ya kutunga kozi hiyo, nilisoma maandishi ya Ernest Hemingway aliyoandika kufuatia safari zake mbili Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54.

Lengo la kozi lilikuwa kuwafundisha wanafanuzi kwa kusafiri nao katika baadhi ya maeneo alimopita Hemingway, huku tukisoma maandishi yake kuhusu safari zake katika maeneo haya. Maandishi hayo ni pamoja na kitabu cha Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, hadithi ya "The Short Happy Life of Francis Macomber," barua, na insha kadhaa katika magazeti.

Pichani wanaonekana wanafunzi na madereva wetu pembeni mwa Ziwa Babati. Katika Green Hills of Africa, Hemingway aliandika kuhusu Babati na Ziwa Babati:

     We left, soon after midnight, ahead of the outfit, who were to strike camp and follow in the two lorries. We stopped in Babati at the little hotel overlooking the lake and bought some more Pan-Yam pickles and had some cold beer (uk. 143).

Wednesday, February 4, 2015

Wanachuo wa Gustavus Adolphus, Marekani, Wameifurahia Tanzania

Wanachuo wa Chuo cha Gustavus Adolphus, ambao walikuwa Tanzania mwezi Januari mwaka huu kwa ziara ya kimasomo, wamerejea salama nchini kwao Marekani. Hao ni wale ambao niliongea nao kuhusu tofauti baina ya utamaduni wa Marekani na ule wa kwetu Afrika, katika kuwaandaa kwa safari.

Jana, mmoja wao ameandika ujumbe katika blogu yangu ya ki-Ingereza:

Dr. Mbele,
Thank you very much for meeting with us before we left for Tanzania. We had a wonderful trip and learned so much about the differences and similarities between our two cultures. The Tanzanians are a beautiful people-- so full of happiness and passion for life. I will never forget my time there and hope that I can go back someday! Thanks you also for signing my copy of your book.
Abby Simms


Natafsiri ujumbe huu hivi:

Dr. Mbele,
Asante sana kwa kukutana nasi kabla hatujaondoka kwenda Tanzania. Safari yetu ilikuwa nzuri sana, na tulijifunza mengi kuhusu jinsi tamaduni zetu mbili zinavyofanana na jinsi zinavyotofautiana. Wa-Tanzania ni watu wazuri--wamejaa furaha na ari ya maisha. Sitasahau kamwe muda niliokuwepo kule na natumaini siku moja kwenda tena! Asante pia kwa kusaini nakala yangu ya kitabu chako.
Abby Simms.


Niliandika katika blogu hii kuwa hao wanachuo, kama walivyo wa-Marekani wengine, wana tabia ya kuripoti kuhusu safari na kukaa kwao Tanzania, nikaahidi kuwa nitakavyopata ripoti hizo, nitaziweka hapa katika blogu yangu.

Sidhani kama kuna m-Tanzania ambaye hatafurahi kusoma ripoti kama hii ya Abby Simms, kwa jinsi inavyotukumbusha kuwa tunayo mema na mazuri. Tukiamua, tunaweza kujibadili tukaachana na yale mabaya na tukaendeleza yale mema na mazuri.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...