Showing posts with label Uuguzi. Show all posts
Showing posts with label Uuguzi. Show all posts

Friday, April 27, 2018

Madaktari Wanafundishia Kitabu Hiki

Nilivyoandika kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, sikuwazia kingetumika kwa namna nyingi kama ilivyotokea baadaye. Kilichonishtua zaidi ni pale waalimu wa uuguzi wa chuo cha Gustavus Adolphus walipoamua kukitumia kufundishia, wakaanza, kila wanapofundisha kozi hiyo, kunialika kuongea na wanafunzi.

Baada ya muda si mrefu, Dr. Randy Hurley mwanzilishi na mhusika mkuu wa  na programu ya hospitali ya Ilula, mkoani Iringa, alinialika kuhutubia mkutano wa mwaka wa wadau wa hospitali hiyo. Ulikuwa ni mkutano wa kuchangisha fedha za kuendelezea programu. Hapo ndipo nikajua kuhusu programu ya kuelimisha wauguzi ambayo inafanyika Ilula, ikiwahusisha wa-Marekani na wa-Tanzania.

Nilijua kuwa wanatumia kitabu changu, bali sikuwa na taarifa zaidi. Lakini siku chache zilizopita nimeona jinsi kitabu hicho kinavyotajwa katika silabasi mpya ya kozi yao. Wanafunzi wanahimizwa kukisoma. Kwa kuwa mimi si mtaalam wa masuala ya uuguzi na matibabu, nilijiuliza masuali, kwa sababu baadhi ya mambo niliyoandika kitabuni ni tofauti na taaluma ya uuguzi na matibabu. Dukuduku yangu hii niliigusia katika blogu hii.

Hatimaye, nilikuja kuelewa vizuri mantiki ya madkatari na waalimu wa uuguzi kukitumia kitabu hiki. Ni kwa sababu kinaelezea utamaduni hauwezi kutenganishwa na masuala ya matibabu ba uuguzi. Madaktari na wauguzi wanatakiwa kuwafahamu wale wanaowahudumia, katika vipengele kama jadi, tabia, matarajio, miiko, imani, na hisia. Ni muhimu kwa muuguzi au daktari kuyafahamu na kuyazingatia wakati anatoa huduma. Kwa hivyo, sasa ninavyosikia kitabu kinatumiwa na watu katika taaluma hizo, sina masuali bali ninashukuru kwamba nimeweza kutoa mchango fulani wa manufaa.

Monday, December 22, 2014

Mkutano na Wanachuo wa Gustavus Adolphus Unakaribia

Siku zinakwenda haraka. Tarehe 5 Januari, ambayo imekaribia, ndio siku nitakayokutana na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus, kama nilivyoandika hapa. Hao ni wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya Tanzania, kujiongezea elimu kuhusu masuala ya afya na matibabu katika mazingira tofauti na ya Marekani, hasa kwa upande wa utamaduni.

Profesa wao aliniomba nikaongee nao kuhusu masuala ya aina hiyo kwa mapana kufuatia yale niliyoandika katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho watakuwa wamekisoma kabla ya mimi kukutana nao.

Kutokana na kusoma hiki kitabu, wanachuo hao watakuwa wameandaa masuali. Kama ilivyotokea siku zilizopita, masuali mengine yatazuka hapo hapo.

Jukumu hili linanifanya nikipitie tena kitabu changu, angalau kijuujuu, kwani sina mazoea ya kusoma sana yale ambayo nimeshayaandika na kuyachapisha. Napendelea kutumia muda wangu na akili yangu katika kutafiti, kutafakari na kuandika mambo mapya. Ingawa yale yaliyomo kitabuni sijayabadili, na sijaona sababu ya kuyabadili, ninafahamu mengi zaidi na naendelea kujifunza, kwani elimu haina mwisho.

Kutokana na ukweli huu, mazungumzo yangu na hao wanachuo wa safari hii hayawezi kuwa sawa na yale ya miaka iliyopita. Hata kama kutakuwa na masuali yanayofanana na yale ambayo nimeshaulizwa kabla, majibu yangu yatajengeka katika upeo mpana zaidi. Fursa za aina hii zinachangia kupanua upeo huo.

Tutakutana, kama siku zilizopita, Mount Olivet Conference & Retreat Center, pembeni mwa mji wa Lakeville, Minnesota. Nangojea kwa hamu kuonana tena na Profesa Zust, na kuonana na hao wanachuo wapya. Panapo majaliwa, nitaweka ripoti katika blogu hii, kama nilivyozoea.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...