Friday, April 27, 2018

Madaktari Wanafundishia Kitabu Hiki

Nilivyoandika kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, sikuwazia kingetumika kwa namna nyingi kama ilivyotokea baadaye. Kilichonishtua zaidi ni pale waalimu wa uuguzi wa chuo cha Gustavus Adolphus walipoamua kukitumia kufundishia, wakaanza, kila wanapofundisha kozi hiyo, kunialika kuongea na wanafunzi.

Baada ya muda si mrefu, Dr. Randy Hurley mwanzilishi na mhusika mkuu wa  na programu ya hospitali ya Ilula, mkoani Iringa, alinialika kuhutubia mkutano wa mwaka wa wadau wa hospitali hiyo. Ulikuwa ni mkutano wa kuchangisha fedha za kuendelezea programu. Hapo ndipo nikajua kuhusu programu ya kuelimisha wauguzi ambayo inafanyika Ilula, ikiwahusisha wa-Marekani na wa-Tanzania.

Nilijua kuwa wanatumia kitabu changu, bali sikuwa na taarifa zaidi. Lakini siku chache zilizopita nimeona jinsi kitabu hicho kinavyotajwa katika silabasi mpya ya kozi yao. Wanafunzi wanahimizwa kukisoma. Kwa kuwa mimi si mtaalam wa masuala ya uuguzi na matibabu, nilijiuliza masuali, kwa sababu baadhi ya mambo niliyoandika kitabuni ni tofauti na taaluma ya uuguzi na matibabu. Dukuduku yangu hii niliigusia katika blogu hii.

Hatimaye, nilikuja kuelewa vizuri mantiki ya madkatari na waalimu wa uuguzi kukitumia kitabu hiki. Ni kwa sababu kinaelezea utamaduni hauwezi kutenganishwa na masuala ya matibabu ba uuguzi. Madaktari na wauguzi wanatakiwa kuwafahamu wale wanaowahudumia, katika vipengele kama jadi, tabia, matarajio, miiko, imani, na hisia. Ni muhimu kwa muuguzi au daktari kuyafahamu na kuyazingatia wakati anatoa huduma. Kwa hivyo, sasa ninavyosikia kitabu kinatumiwa na watu katika taaluma hizo, sina masuali bali ninashukuru kwamba nimeweza kutoa mchango fulani wa manufaa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...