Sunday, April 8, 2018

Nimenunua Kitabu cha Grimm Brothers

Leo, nilikwenda Apple Valley kumpelekea mama mmoja Mmarekani Mweusi nakala ya kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kama zawadi, kwa kuwa alikuwa ameniambia anapenda kujifunza kuhusu utamaduni wa Afrika.

Baada ya kukutana naye, nilikwenda katika duka la Half Price Books. Nilipita upesi sehemu yenye vitabu vya Hemingway, halafu nikaenda kwenye sehemu yenye vitabu vvya bei ya chini kabisa, yaani "clearance" kwa ki-Ingereza cha Marekani.

Hapo ingawa nilishawishika kununua kitabu hiki au kile, kikiwemo The Inheritance of Loss cha cha Kiran Desai,sikununua. Nilishawishika kuhusu hiki kitabu cha Desai kwa sababu muhula huu ninafundisha kitabu chake kingine, Hullabaloo in the Guava Orchard.

Badala ya vitabu hivyo, nilinunua The Complete Illustrated Stories of the Brothers Grimm. Kitabu hiki nimekifahamu kwa miaka mingi, kwani hao ndudu wawili, Wajerumani, Jacob na Wilhelm Grimm ndio wanaotambulika kama waasisi wa taaluma ya ukusanyaji na uchambuzi wa hadithi za jadi.

Walirekodi hadithi sehemu mbali mbali katika nchi yao wakaanza kuzichapisha mwaka 1812. Walifanya kazi hiyo kwa miaka mingi, wakaanza vile vile kutafakari mambo yanayojitokeza katika hadithi za jadi. Kwa namna hiyo waliasisi taaluma ambayo nami ninashughulika nayo.

Kuna mjadala wa tangu zamani kuhusu kama ndugu hao wawili walichapisha hadithi kama walivyosimuliwa au walizihariri ili kuondoka vipengele walivyoona havifai kimaadili na vinginevyo. Hili ni suala tata hadi leo, katika jamii kadhaa, kama vile Marekani.

Ninazo hadithi mbali mbali zilizorekodiwa na hao ndugu wawili, lakini kitabu hiki ni muhimu kwa sababu kina hadithi zote kwa pamoja.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...