Friday, April 13, 2018

Taarifa Tatu Kuhusu Kitabu Changu

Blogu hii ni mahali ambapo ninajiwekea kumbukumbu zangu, sambamba na mambo mengine. Jana na leo zimekuwa siku za pekee, kwani nimefikiwa na taarifa tatu kuhusu kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Jana jioni, nilikutana na bwana moja mwenye asili ya ki-Somali aliyejitambulisha kama kiongozi mojawapo wa shule za Minneapolis. Tulipotambulishwa, alianza kunielezea kuwa alishasoma kitabu changu, akagusia jambo mojawapo analolikumbuka kuhusu dhana ya uzuri wa maumbile yetu. Huo ulikuwa ni ujumbe moja kuhusu kitabu changu.

Ujumbe mwingine nimepata leo kutoka Nairobi kwa muasisi na mkurugenzi wa taasisi iitwayo IIHT Tulifahamiana alipokuwa anafanya kazi jimboni Illinois hapa Marekani baada ya kuhitimu shahada ya uzamifu. Aliwahi kuendesha semina kwa washiriki yapata 100. Alikuwa ameagiza nakala za kitabu changu kwa washiriki wote wa semina na alinialika kuhutubia. Baada ya kupoteana kwa miaka yapata kumi, nilimtafuta mtandaoni. Nilimwandikia kumsalimia, naye ameandika kuwa ananikumbuka na kuwa anatumia kitabu changu kuwafundishia wakufunzi kutoka India.

Leo pia nimepata ujumbe kutoka kwa profesa mwenzangu wa hapa chuoni St. Olaf ambaye aliwahi kuniambia kuwa atapeleka wanafunzi Tanzania mwaka ujao. Alisema kuwa angependa nimpe ushauri. Leo katika ujumbe wake amesema anasoma kitabu changu na anakifurhia. Tumekubaliana kuwa niongee na wanafunzi wake tarehe 27 mwezi huu.

Kumbukumbu zangu hizi zitanisaidia siku za usoni endapo nitapenda kuandika kitabu kuhusu uzoefu wangu kama mwandisho wa vitabu. Akitokea mtu mwingine akataka kuandika, naye atakuwa na taarifa za kutumia.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...