Showing posts with label Namanga. Show all posts
Showing posts with label Namanga. Show all posts

Thursday, April 18, 2013

Mlima Longido, Tanzania

 Hakuna mtu ambaye anaweza kuzitembelea au kuziona sehemu zote za nchi yetu au nchi yoyote nyingine. Hii ni sababu moja ya mimi kuweka kwenye blogu hii picha za sehemu mbali mbali. Nataka wengine nao wafaidike angalau kidogo na kupanua ufahamu wao. Yawezekana, pia, wakahamasika kwenda kujionea.

Leo naleta picha za mlima Longido. Mlima huu uko Tanzania ya kaskazini, baina ya mji wa Longido na Namanga. Unaonekana vizuri kabisa kutoka kwenye barabara itokayo Arusha kwenda Namanga. Picha hizi nilizipiga mwishoni mwa Januari, mwaka huu, nikiwa safarini kutoka Namanga kwenda Longido. Baada ya kuondoka Namanga, picha ya kwanza niliyopiga ni hiyo hapa kushoto.
Muda mfupi baadaye, nilipiga picha hii inayoonekana kushoto.
 Baadaye kidogo nilipiga picha hii hapa kushoto.
Tulivyozidi kukaribia Longido, nilipiga picha hii hapa kushoto.

Nimeshauona mlima Longido mara nyingi, katika miaka zaidi ya ishirini iliyopita, wakati nikisafiri baina ya Tanzania na Kenya. Nimewahi kuutaja mlima huu katika ujumbe huu hapa.

Kitu kimoja kinachonivutia ni jinsi mlima huu unavyoonekana wakati unapoukaribia kutokea Namanga. Ile sehemu iliyochomoka inanifanya niwazie pembe ya kifaru. Picha ninayopata ndio hiyo. Lakini mwaka huu, nimetambua vizuri kwamba ile pembe ya kifaru inabadilika kabisa na kuwa mwamba unaoonekana hapa kushoto. Mwaka huu ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuangalia kwa makini taswira hii na kujionea jinsi pembe ya kifaru inavyotoweka na kuwa mwamba uliosimama, ukiwa na sura tofauti.

Thursday, May 5, 2011

Mitaani Namanga, 2007

Ingawa mdogo, mji wa Namanga ni maarufu, kwa vile uko mpakani. Hapa naonekana nikiwa Namanga, upande wa Tanzania. Naelekea kwenye geti la mpaka, hatua chache mbele yangu. Kule mbali unaona Mlima Longido. Barabara inapita kulia kwake, inaingia Longido, nyuma ya mlima, na kuelekea Arusha.

Hii ni moja ya hoteli ambapo napenda kufikia, kwa Bwana Minja, kupata chakula na kinywaji. Nimeshalala hapo.








Nilipendezwa na mpangilio wa nyumba hizi na ile
milima. Hizi nyumba ziko mwanzoni mwa mji wa Namanga, kabla hujafika kwenye geti la mpaka baina ya Kenya na Tanzania.







Nilikuwa Namanga na kikundi cha wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado na mwalimu wao, ambao walifika Tanzania katika kozi niliyoiunda, kuhusu mwandishi Hemingway. Hao ni wanafunzi waanzilishi wa kozi hii. Napangia kuibadili kidogo na kuiweka katika program ya Chuo cha St. Olaf.

Hapa nipo upande wa Kenya. Kama mdau unavyoona, mapokezi hayakuwa haba. Ndio mambo ya ujirani mwema hayo.








Namanga, kama ilivyo miji mingine, ina sehemu nyingi ambapo unaweza kupumzika, na kujipatia chakula na pia kukata kiu baada ya mizunguko yako mitaani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...