Showing posts with label Longido. Show all posts
Showing posts with label Longido. Show all posts

Sunday, February 8, 2015

Mwenyeji Wetu Longido, Tanzania

Picha hii ilipigwa Januari, 2013, nilipokuwa Longido, Tanzania. Niko na Ndugu Ally Ahamadou, mkurugenzi wa programu ya utalii wa utamaduni hapa Longido. Yeye ndiye alikuwa mwenyeji wa misafara yangu katika kozi kuhusu safari na maandishi ya Ernest Hemingway.

Programu ya utalii wa utamaduni Longido ni moja kati ya programu maarufu za aina hii nchini Tanzania. Taarifa kuhusu program hii zinapakana kirahisi mtandaoni.

Binafsi nimeshuhudia jambo hili kwa jinsi makala niliyochapisha katika blogu yangu ya ki-Ingereza kuhusu utalii wa utamaduni Longido inavyotembelewa na wasomaji wengi. Hali hii imenithibitishia kuwa blogu inaweza kuwa nyenzo yenye uwezo mkubwa wa kutangaza utalii.

Ingawa Ndugu Ally Ahmadou si mzaliwa wa Longido, bali Tanga, niliona anakubalika sana na watu wa Longido. Hata kwa kuongea naye muda mfupi tu, unapata picha kuwa huyu ni mpenzi Longido na shughuli za utalii wa utamaduni. Programu hii ya utalii wa utamaduni Longido niliona inapendwa na watu wa Longido, kwa kuwa faida zake katika jamii yao wanaziona.

Ndugu Ally Ahmadou nilimwona kuwa mtu mwepesi wa kuangalia fursa mpya katika shughuli ya utalii. Mfano ni jinsi tulivyoongelea suala la vitabu katika utalii, suala ambalo nimeliongelea katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii na nililigusia pia katika blogu hii. Ndugu Ally alipofahamu kuwa nimechapisha vitabu vinavyoweza kuchangia katika sekta hiyo, alichukua nakala za kutosha za Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kwa ajili ya watalii ambao wangependa kuvinunua.

Wednesday, June 4, 2014

Kazi na Dawa, Longido


Hapa niko katika baa mojak kwenye mji mdogo wa Longido. Ilikuwa ni mwezi Januari, 2013, wakati nilipokuwa Tanzania nikiendesha kozi ya "Hemingway in East Africa." Naonekana nikisoma kitabu kimoja cha Hemingway, True at First Light.

Nadhani tulikuwa na kipindi baadaye mchana ule, nami nilikuwa katika maandalizi.














Kutokana na kazi nzito, na pia joto, ilinibidi kujipatia kitu kidogo cha kuburudisha koo na akili. Hapa naonekana nimeshika kachupa ka bia na glasi.

Watanzania wengi tumejiaminisha kuwa katika hali ya uchovu na joto, bia ndio wakati wake. Tunasema "kazi na dawa." Sijui kama ni ukweli au tumejiwekea hiyo dhana kwa maslahi yetu tu, au ni uzembe. Labda soda ingetosha, au maji. Sijui.

Thursday, April 18, 2013

Mlima Longido, Tanzania

 Hakuna mtu ambaye anaweza kuzitembelea au kuziona sehemu zote za nchi yetu au nchi yoyote nyingine. Hii ni sababu moja ya mimi kuweka kwenye blogu hii picha za sehemu mbali mbali. Nataka wengine nao wafaidike angalau kidogo na kupanua ufahamu wao. Yawezekana, pia, wakahamasika kwenda kujionea.

Leo naleta picha za mlima Longido. Mlima huu uko Tanzania ya kaskazini, baina ya mji wa Longido na Namanga. Unaonekana vizuri kabisa kutoka kwenye barabara itokayo Arusha kwenda Namanga. Picha hizi nilizipiga mwishoni mwa Januari, mwaka huu, nikiwa safarini kutoka Namanga kwenda Longido. Baada ya kuondoka Namanga, picha ya kwanza niliyopiga ni hiyo hapa kushoto.
Muda mfupi baadaye, nilipiga picha hii inayoonekana kushoto.
 Baadaye kidogo nilipiga picha hii hapa kushoto.
Tulivyozidi kukaribia Longido, nilipiga picha hii hapa kushoto.

Nimeshauona mlima Longido mara nyingi, katika miaka zaidi ya ishirini iliyopita, wakati nikisafiri baina ya Tanzania na Kenya. Nimewahi kuutaja mlima huu katika ujumbe huu hapa.

Kitu kimoja kinachonivutia ni jinsi mlima huu unavyoonekana wakati unapoukaribia kutokea Namanga. Ile sehemu iliyochomoka inanifanya niwazie pembe ya kifaru. Picha ninayopata ndio hiyo. Lakini mwaka huu, nimetambua vizuri kwamba ile pembe ya kifaru inabadilika kabisa na kuwa mwamba unaoonekana hapa kushoto. Mwaka huu ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuangalia kwa makini taswira hii na kujionea jinsi pembe ya kifaru inavyotoweka na kuwa mwamba uliosimama, ukiwa na sura tofauti.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...