Showing posts with label Bunge la Tanzania. Show all posts
Showing posts with label Bunge la Tanzania. Show all posts

Thursday, May 5, 2011

Mitaani Namanga, 2007

Ingawa mdogo, mji wa Namanga ni maarufu, kwa vile uko mpakani. Hapa naonekana nikiwa Namanga, upande wa Tanzania. Naelekea kwenye geti la mpaka, hatua chache mbele yangu. Kule mbali unaona Mlima Longido. Barabara inapita kulia kwake, inaingia Longido, nyuma ya mlima, na kuelekea Arusha.

Hii ni moja ya hoteli ambapo napenda kufikia, kwa Bwana Minja, kupata chakula na kinywaji. Nimeshalala hapo.








Nilipendezwa na mpangilio wa nyumba hizi na ile
milima. Hizi nyumba ziko mwanzoni mwa mji wa Namanga, kabla hujafika kwenye geti la mpaka baina ya Kenya na Tanzania.







Nilikuwa Namanga na kikundi cha wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado na mwalimu wao, ambao walifika Tanzania katika kozi niliyoiunda, kuhusu mwandishi Hemingway. Hao ni wanafunzi waanzilishi wa kozi hii. Napangia kuibadili kidogo na kuiweka katika program ya Chuo cha St. Olaf.

Hapa nipo upande wa Kenya. Kama mdau unavyoona, mapokezi hayakuwa haba. Ndio mambo ya ujirani mwema hayo.








Namanga, kama ilivyo miji mingine, ina sehemu nyingi ambapo unaweza kupumzika, na kujipatia chakula na pia kukata kiu baada ya mizunguko yako mitaani.

Friday, April 15, 2011

Hatimaye, Bia Zitazinduliwa Ikulu

Ni juzi tu hapo niliandika makala kuhusu jinsi wa-Tanzania wanavyowajibika katika unywaji wa ulabu. Makala hiyo ni "Kazi ya Kunywa". Katika kuhitimisha, nilitamka kuwa, kwa mwendo tunaokwenda, huko mbele ya safari ulabu utakuwepo hadi shuleni na Bungeni.

Ni kama vile niliota. Wiki hii wabunge wa Tanzania wameweka historia kwa kuzindua vinywaji vikali huko Dodoma. Soma hapa.

Nchi yetu ni ya pekee. Tunauenzi ulabu kiasi hiki, ingawa unasababisha au kuchangia matatizo mengi, kuanzia ajali barabarani zinazosababisha vifo vingi na watu wengi kuumia, uharibifu wa mali, magomvi katika jamii, kuharibika akili na matatizo ya kisaikolojia.

Tunakwenda kwa kasi na ari kiasi kwamba siku si nyingi kuanzia sasa, bia zitakuwa zinazinduliwa Ikulu. Na siku ya kuzindua bia itakuwa ni ya kukumbukwa ki-Taifa.

Enzi za uongozi wa Mwalimu Nyerere, wabunge wangekuwa wanazindua maktaba, si ulabu. Hakuna mtu aliyethubutu kufanya mambo yanayofanyika leo. Lakini mambo ndio hayo: akiondoka paka, panya hutawala.

Wednesday, November 24, 2010

Kitendo cha CHADEMA Kususia Hotuba ya JK

Kitendo cha wabunge wa CHADEMA kususia hotuba ya JK Bungeni kimeibua mjadala mkubwa miongoni mwa wa-Tanzania. Wakati mjadala huu ukiendelea, nami nina la kusema.

CHADEMA imesema kuwa, mapema kabisa, ilipeleka malalamiko kwenye tume ya uchaguzi (NEC) kuhusu mchakato wa utangazaji wa matokeo ya urais, na kuomba utangazaji ule usimamishwe ili kuchunguza dosari ambazo CHADEMA ilikuwa na taarifa nazo.

Kwa msingi huu, ningependa kusikia taarifa ya NEC, niweze kufahamu kama kweli ililetewa malalamiko hayo. Kama iliyapata, napenda kujua iliyashughulikia vipi. CHADEMA inasema kuwa NEC haikuyajibu wala kuyashughulikia malalamiko yale.

Kama hii ni kweli, basi naitupia NEC lawama nzito. CHADEMA imesema kwamba kutokana na kuupuziwa malalamiko yao na NEC, na kutokana na kwamba sheria inasema kuwa tangazo la NEC la mshindi wa urais haliwezi kupingwa mahakamani au penginepo, walilazimika kutafuta hatua zingine za kuelezea malalamiko yao. CHADEMA wanasema kuwa kususia hotuba ya JK ni njia waliyoamua kuchukua kwa msingi huo.

Kama hali ndio hiyo inayoelezwa na CHADEMA, na kama NEC haitatoa maelezo ya kuthibitisha vingine, msimamo wangu ni kuwa CHADEMA walikuwa na haki ya kususia hotuba ya JK kama walivyofanya. Kama raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa, bali ni mpenda haki, uwazi, na ukweli, nawaunga mkono CHADEMA kwa suala hilo.

Nchi lazima iwe na kiongozi muda wote. Kwa msingi huu, JK ni rais, na CHADEMA hawajakataa hilo, ingawa kuna watu ambao, kwa sababu wanazozijua wao, wanaizushia CHADEMA uwongo kuwa haimtambui rais na serikali yake. Najiuliza kama watu hao wana akili timamu au kama wanaitakia mema nchi yetu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...