Showing posts with label Dar es Salaam. Show all posts
Showing posts with label Dar es Salaam. Show all posts

Sunday, June 21, 2015

Niliyoyaona Maktabani Brookdale, Minnesota

Jana, kama nilivyoandika katika blogu hii, nilihudhuria mkutano Brooklyn Park, ambao tulifanyia katika maktaba ya Brookdale. Hapa kushoto ni picha ya upande wa Mbele wa maktaba hii, inavyoonekana kabla hujaingia ndani. Jana ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kufika hapa, na niliona jinsi jengo lilivyo tofauti na majengo ya maktaba zingine ambazo nimeingia hapa Minnesota.



Nilivyoingia ndani, nilijikuta sehemu hii inayoonekana kushoto, ingawa ni kubwa na pana zaidi ya hii inayoonekana pichani. Wakutubi wengi wapo katika eneo hilo, tayari kuwasiaida wateja, na sehemu ya maulizo ambayo ni kubwa pia, iko eneo hili. Unapokuwa sehemu hii, kwa mbele yako na pembeni kuna maeneo yenye vitabu, majarida, kompyuta nyingi na hifadhi mbali mbali za taarifa, kama vile CD, DVD na na kaseti.

Niliulizia kilipo chumba cha mkutano, nikapita katikati ya makabati ya vitabu vya kila aina hadi mwishoni kabisa.




Baada ya mkutano, nilirejea tena sehemu hii na kuchungulia katika makabati mbali mbali, hasa ya fasihi. Kuna utajiri mkubwa wa vitabu, vya masomo na taaluma mbali mbali, vya watoto na watu wazima, na vitu vingine vingi. Inapendeza kuona wenzetu wanavyowekeza katika vitu vya namna hii, kuelimisha jamii.

Hiyo jana ilikuwa ni Jumamosi, na ilikuwa ni alasiri. Jua lilikuwa linawaka vizuri, na walikuwepo watu wengi katika maktaba, watu wa kila rangi, na kila rika. Wwnginw walikuwa wanasoma vitabu, wengine wanaazima, wengine wanatumia kompyuta, na wengine walikuwa wanarudufu maandishi.

Nilivyoangalia hali hii, ya watu wengi kuwemo maktabani wakati wa alasiri, Jumamosi, niliwazia hali ya Tanzania. Nilijiuliza ni wapi katika Tanzania unaweza kuona hali hii, tena Jumamosi mchana. Ni wapi unaweza kuwaona watu wa rika mbali mbali wamejaa maktabani wanajisomea. Hata huyu dada Latonya  niliyekutana naye jana hapo nje ya maktaba alikuwa anakuja maktabani na akina dada wenzake.

Ningekuwa na uwezo, ningebadili mioyo ya wa-Tanzania, wawe kama hao wa-Marekani, wenye kupenda kusoma. Ningehamasisha ujenzi wa maktaba zaidi. Kwa mji kama Dar es Salaam, ningependa ziwepo maktaba Sinza, Kinondoni, Buguruni, Kigamboni, Kawe, Kimara, Ukonga na sehemu zingine. Ingekuwa ni Marekani, mji wa ukubwa wa Dar es Salaam ungekuwa na maktaba nyingi. Lakini, miaka hamsini na zaidi tangu tupate uhuru, maktaba ni hiyo hiyo moja. Si jambo la kujivunia.

Wednesday, January 26, 2011

Kitimoto

Neno kitimoto ni maarufu Tanzania. Kitimoto ni nyama ya nguruwe; inapendwa sana katika mabaa na sehemu zingine. Ubora wa kitimoto ni kivutio kwa wateja na neema kubwa kibiashara kwa wenye baa. Hapa kushoto ni sahani ya kitimoto ambayo niliinunua kwenye baa moja Sinza, hatua chache kutoka Lion Hotel.

Ninapokuwa katika miji kama Dar es Salaam, napatikana mitaa ya u-Swazi, kama inavyoonekana katika picha hii, iliyopigwa Sinza, bondeni ukifuata barabara inayopita mbele ya Lion Hotel. Kwa wale wasiojua, neno u-Swazi linamaanisha sehemu wanazoishi wananchi wa kawaida.

Hapo kushoto kuna baa na sehemu ya kitimoto ambapo nimeshakuwa mteja mara kadhaa. Picha hii inaonyesha jinsi mwenye kitimoto anayotangaza biashara yake. Tofauti na zamani, anaweza kuagiza nyama kutoka bucha kwa kutumia simu, na anaweza kuchukua oda za wateja kwa simu pia.


Pamoja na umaarufu wake, kuna hisia tofauti, michapo, na utani kuhusu kitimoto, mambo ambayo yanaweza kufanyiwa utafiti kama sehemu muhimu ya utamaduni wa leo wa m-Tanzania.

Tuesday, January 11, 2011

Wauza Vitabu wa Mitaani Dar es Salaam

Kitu kimojawapo kinachonivutia ninapokuwa Dar es Salaam ni wauza vitabu wa mitaani. Wako wa aina mbili. Wako wenye sehemu maalum ya kuuzia vitabu, iwe ni meza tu au kibanda. Hao wanaonekana sehemu mbali mbali za mjini Dar es Salaam, kuanzia katikati ya mji, kama vile barabara ya Samora, hadi sehemu za pembeni, kama vile Mwenge na Ubungo. Picha iliyoko hapa kushoto niliipiga Ubungo, mwaka jana, karibu na kituo kikuu cha mabasi. Pembeni ya mwuza vitabu kuna kibanda cha muuza machungwa.

Wako wauza vitabu wengine ambao hutembeza vitabu mitaani, sawa na wale vijana ambao wanatembeza bidhaa mbali mbali, ambao tunawaita machinga. Hapo kushoto kuna picha niliyopiga Sinza Kijiweni, mwaka jana, kwenye hoteli ya Deluxe.



Nilikuwa hapo, na hao vijana wawili wakaja, mmoja akiuza vitabu na mwingine peni za kuandikia. Nilivutiwa, nikaanza kuongea nao. Nilimwuliza huyu muuza vitabu kuhusu wateja, na kama wa-Tanzania wananunua vitabu, akanielezea uzoefu wake. Nilinunua vitabu viwili. Kimoja ni tafsiri ya maneno ya ki-Ingereza kwenda ki-Swahili, na kingine ni tafsiri ya maneno ya ki-Swahili kwenda ki-Ingereza. Vyote vimechapishwa Kenya, na walengwa ni wageni wanaotembelea Afrika Mashariki. Ni vijitabu vidogo vidogo sana, kimoja cha kurasa 30 na kingine kurasa 32.

Karibu na lango la kituo cha mabasi Ubungo nilipiga picha iliyo hapa kushoto, mwaka jana, baada ya kumwomba kijana mwenye kibanda hicho. Tuliongea kuhusu biashara yake, naye alinieleza kuwa biashara inaenda vizuri, ila ingekuwa nzuri zaidi kama angekuwa na mtaji wa kutosha ili kuwa na meza kubwa zaidi na vitabu vingi zaidi. Nilifurahi kusikia hivyo, ushahidi kuwa wako watu wanaonunua vitabu. Kinachobaki ni kufuatilia zaidi kuona ni watu wa aina gani. Yule kijana niliyeongea naye Sinza alisema kuwa wanaonunua vitabu zaidi ni watu wa Zambia. Nitafuatilia zaidi suala hili siku zijazo, panapo majaliwa.

Katika pitapita yangu na kuangalia nimeona kuwa kuna vitabu vya aina nyingi humo mitaani, kuanzia hadithi za waandishi maarufu wa sehemu mbali mbali za dunia, hadi taaluma mbali mbali. Kuna vitabu vilivyotumika na vipya pia. Mtu makini anaweza kujipatia vitabu vingi vya manufaa kutoka kwa hao wauzaji wa mitaani akawa na maktaba binafsi ya kueleweka.

Sunday, December 19, 2010

Kitabu Kimetua St. Cloud, Minnesota

Wasomaji wa blogu zangu, hii na ile ya ki-Ingereza, wanafahamu ninavyopenda kujishughulisha na masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake katika ulimwengu wa leo.

Nafanya shughuli hizi si kwa ajili ya kutafuta umaarufu, bali naamini ni wajibu kwa wanadamu kusaidiana katika maisha na kuifanya dunia iwe bora kuliko ilivyo.

Miezi ya karibuni nimejishughulisha sana na matatizo yanayowapata wahamiaji wa ki-Somali katika jimbo la Minnesota, ambalo linaongoza kwa idadi ya wahamiaji wa ki-Somali. Wasomaji wa blogu zangu watakumbuka taarifa za shughuli zangu katika mji wa Faribault.

Matatizo kama haya ya Faribault yako pia katika miji mingine, kama vile St. Cloud. Kutokana uzoefu nilioupata Faribault, nimeanzisha mawasiliano na ndugu Mohamoud Mohamed, mkurugenzi wa SASSO, jumuia inayoshughulikia masuala ya wa-Somali mjini St. Cloud.

Nilimpelekea nakala ya kitabu cha Africans and Americans, kama mchango wangu na changamoto. Jana ameniambia kuwa kitabu amekipata, anaendelea kukisoma, na anakipenda. Atawaonyesha wadau wa St. Cloud: halmashauri ya mji, shule na vyuo, idara ya polisi, mahospitali, na kadhalika. Nami nilimhakikishia kuwa ni jambo bora. Badala ya watu kununiana tu au kugombana, ni vema wakaanza utaratibu wa kuzungumzia matatizo kama ilivyofanyika Faribault, na ikapokelewa vizuri.

Kama ninavyosema katika mihadhara, blogu na maandishi mengine, matatizo ya aina hii yanayoikumba miji ya Faribault na St. Cloud yanajitokeza katika miji na jamii nyingine duniani: Afrika, Asia, Australia, Marekani, Ulaya, na kwingineko, na yataongezeka, kutokana na mwenendo wa utandawazi wa leo. Ninapokuwa Dar es Salaam, kwa mfano, nasikiliza na kutafakari minong'ono na majungu kuhusu wa-China, ambao wanaendelea kuja katika mji ule. Niliwahi pia kuongelea tafrani iliyotokea Zanzibar. Kinachobaki ni sisi kujizatiti kwa kuelimishana kuhusu tofauti zetu na kutafuta namna ya kuishi bila matatizo.

Najiandaa kushiriki katika masuala ya St. Cloud. Mbali ya umuhimu wake kwa jinsi hali ilivyo, ni fursa ya mimi kujiongezea ujuzi na uzoefu nitakaoutumia katika kuwasaidia wengine.

Tuesday, September 21, 2010

Kiboko ya Wachawi

Nilipokuwa Tanzania mwaka huu, nilipata wazo la kupiga picha za matangazo mbali mbali ya waganga wa kienyeji, ambayo ni mengi kwenye miji kama Dar es Salaam. Matangazo hayo yanahusu uponyaji wa magonjwa na matatizo mengine ya afya, mafanikio ya biashara na maisha, kuwavuta wapenzi, na kadhalika.

Tangazo hili la "Kiboko ya Wachawi" nililiona Kibamba, kandokando ya barabara itokayo Dar es Salaam kwenda Morogoro, tarehe 28 Julai. Nilipita hapo na walimu wengine watatu kutoka Marekani, kutembelea shule ya sekondari ya Shulua ambayo iko maeneo hayo.

Tuesday, September 7, 2010

Watoto wa Tanzania Wanapenda Vitabu

Wengi wetu tunalalamika kuhusu kufifia au kutoweka kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu miongoni mwa wa-Tanzania. Inaonekana kuwa hata pale ambapo vitabu vipo, kama vile maktaba, wa-Tanzania hawaendi kusoma.

Ukweli ni kuwa tabia hii inajengeka na umri. Watoto wa Tanzania, wanapenda vitabu, sawa na watoto wengine popote. Nimeshuhudia hayo katika pita pita zangu Tanzania. Kwa mfano, ukienda kwenye maonesho ya vitabu Tanzania, utawaona watoto.

Mwanzoni mwa Septemba, 2004, kulikuwa na maonesho ya vitabu katika uwanja wa hifadhi ya kumbukumbu za Taifa, Dar es Salaam. Kama kawaida, waliohudhuria zaidi ni watoto.

Katika maonesho hayo, watoto wa shule walifanya michezo ya kuigiza, kuhusu umuhimu wa vitabu.
Waliimba pia nyimbo, wakiwahamasisha wazazi kuweka vitabu nyumbani na kuwa na utaratibu wa kusoma pamoja na watoto. Lakini, ujumbe wao uliishia hewani, kwani wazazi wenyewe hawakuwepo.

Wakati wa kuigiza mchezo, watoto hao walishika vitabu, kama vilelelezo. Nilimwona mtoto mmoja ameshika kijitabu changu kuhusu Things Fall Apart. Anaonekana hapa juu, wa pili kutoka kulia. Niliguswa na jambo hilo.

Mwaka huu, tarehe 24-25 Juni nilishiriki maonesho ya elimu na ajira, ambayo yaliandaliwa na Tripod Media. Yalifanyika Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam.
Nililipia banda, nikaweka vitabu vyangu na machapisho mengine, nikawa naongea na watu kwa siku zote mbili.

Walifika watoto wengi, na hapo nilijionea mwenyewe jinsi watoto walivyo na ari ya vitabu. Walikuwa wanaviangalia na waliniuliza masuali kem kem.
Nami nilitumia fursa hii kuwaelezea umuhimu wa kusoma na kutafuta elimu kwa dhati muda wote.



Nilipata faraja kubwa katika kuwa na watoto hao na kuona moyo wao juu ya vitabu.



Suali la msingi linabaki: Tufanyeje ili watoto waweze kukua na moyo huu walio nao bila kulegea au kufifia? Kuna njia gani ya kuwafanya watu wazima wahudhurie maonesho ya vitabu?

Katika jarida la Tanzania Schools Collection, toleo la kwanza, Moris Mwavizo anaripoti, ukurasa 12, kuwa katika maonesho fulani ya vitabu Dar es Salaam, mratibu mmoja alimwona mtoto akizunguka mwenyewe katika viwanja. Alipomwuliza kwa nini baba yake hakuja naye, mtoto alijibu kuwa baba yake angekuja kama kungekuwa na bia hapa kwenye maonesho. Je, hii si aibu?

Thursday, July 15, 2010

Ninasoma "Siku ya Watenzi Wote"

Kwa siku kadhaa sasa nimekuwa nikisomaa Siku ya Watenzi Wote, kitabu cha Shaaban Robert, ambacho nilikinunua tarehe 8 Julai pale Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Chuo Kikuu Dar es Salaam, kwa bei ya shilingi 5,000 tu.

Ninapenda kusoma vitabu muhimu kama hivi vya Shaaban Robert, kama nilivyoandika katika blogu hii na katika kitabu cha CHANGAMOTO. Nimeamua kujielimisha ili niweze kuandika kwa ki-Swahili vizuri iwezekanavyo. Ni jitihada binafsi ya kujikomboa kutokana na kasumba na fikra potofu tulizo nazo wengi, hasa wasomi, kuhusu lugha ya ki-Swahili. Ninataka kuonyesha heshima kwa lugha hii kwa kuiandika kwa usahihi.

Mambo mengi yaliyomo katika Siku ya Watenzi Wote yanatokea Dar es Salaam. Tunawaona wahusika wakiwa katika mitaa kama Kichwele, Ilala, Mnazi Moja, Kariakoo, na Msasani. Hii inafurahisha, kwani mwandishi anauenzi mji huu kwa kuuweka kitabuni namna hii. Inanikumbusha hadithi za mwandishi Moyez Vassanji, kama vile Uhuru Street, ambaye naye aliandika sana kuhusu Dar es Salaam.

Katika Siku ya Watenzi Wote, ambacho kinasemekana kuwa ni kitabu chake cha mwisho, Shaaban Robert anarejea katika masuala ambayo alikuwa ameyashughulikia katika maandishi yake yaliyotangulia, kwa miaka mingi. Shaaban Robert anaongelea na kutafakari masuala muhimu ya jamii, kama vile tofauti za matabaka, tabaka la maskini na tajiri, hali ya wanawake. Tunamsikia Shaaban Robert mwanafalsafa, mchambuzi wa masuala ya jamii, mwenye hisia nzito kuhusu maana ya maisha, mahusiano baina ya wanadamu, haki, na utu. Shaaban Robert anawakosoa walimwengu kwa ufinyu wa mawazo ambao tunauendekeza kwa kisingizio cha dini.

Kitabu kama Siku ya Watenzi Wote ni hazina kubwa. Kila ukurasa una mambo ya kugusa akili na hisia, kupanua mawazo na ufahamu wa lugha. Thamani ya kitabu kama hiki ni kubwa mno, wala haipimiki kwa fedha, hata kama kingeuzwa kwa shilingi 50,000.

Friday, June 18, 2010

Nashiriki Tamasha la Elimu, Dar es Salaam, Juni 24-25

Tarehe 24 na 25 Juni nitakuwa Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam, nikishiriki tamasha la elimu. Nitakuwa na meza yangu na hapo nitaongea na watu kuhusu masuala ya elimu, utamaduni na kadhalika, na hasa shughuli zangu katika nyanja hizo. Vitabu vyangu vitakuwepo.

Nawakaribisha wote; tuonane, tubadilishane mawazo, na tulumbane. Karibuni sana.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...