Showing posts with label Diamond Jubilee Hall. Show all posts
Showing posts with label Diamond Jubilee Hall. Show all posts

Wednesday, September 3, 2014

Matamasha Ninayoshiriki ni Kama Shule

Matamasha ninayoshiriki ni muhimu. Ni kama shule. Ninabadilishana mawazo na wadau mbali mbali. Kuna ambayo ninawaeleza na kuwaelimisha, na wao kuna ambayo wananieleza na kunielimisha. Kuna masuali na majibu, au angalau maelezo, kwa upande wao na wangu.

Hapa kushoto naonekana niko katika mazungumzo mazito na jamaa mmoja kutoka Liberia, aitwaye Ahmed. Tumefahamiana kwa miaka kadhaa. Hapo tulikuwa katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park.



Ninapata fursa ya kukutana na watu wa aina aina. Hapa kushoto niko na mama mmoja ambaye alionekana mkimya, lakini alikuwa na dukuduku ya kujua moja mawili. Ilikuwa katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park.









Hapa kushoto nilikuwa katika mji wa Brooklyn Park, na wa-Marekani Weusi wawili. Huyu aliyekaa pembeni yangu tulikuwa tunafahamiana, lakini huyu mwenye kofia ilikuwa ni mara ya kwanza kukutana. Ilikuwa katika tamasha fulani lililoandaliwa na taasisi ya wa-Afrika, inayoshughulikia masuala ya afya.

Huyu mwenye kofia alikuwa mtu asiye na papara katika kuzungumza, bali mwenye tafakari nzito. Unaweza kujionea jinsi tunavyomsikiliza kwa makini.




Shughuli zangu sifanyii Marekani tu. Hapa kushoto nilikuwa Diamond Jubilee Hall, mjini Dar es Salaam, katika tamasha lililoandaliwa na Tripod Media.

Ninaonekana nikiwahamasisha watoto wa shule kuhusu kufanya bidii shuleni,  nikiwapa mfano wangu mwenyewe na hatua niliyofikia maishani. Kuwaambia watoto kama hao kwamba juhudi niliyofanya shuleni imeniwezesha sasa kuwa mwalimu na mwandishi wa vitabu ni namna ya kuwahamasisha wazingatie shule.



Hapa kushoto niko na jamaa wawili, Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam, katika tamasha la Tripod Media nililotaja hapa juu. Kama unavyoona, tuko katika mazungumzo mazito.










Hapa kushoto, katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park, naonekana nikipata mawili matatu kutoka kwa bwana Bolstad, ambaye alizaliwa na kukulia Tanzania, na wazazi wa-Marekani. Ingawa sasa anaishi Marekani, anajisikia kama m-Tanzania, na ki-Swahili anaongea vizuri sana.

Yeye nami tumefahamiana kwa miaka mingi kidogo, na naguswa na jinsi anavyokipigia debe kwa watu mbali mbali kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Watu wa aina yake wanachangia katika kunifanya niwe na ari ya kuandika zaidi, kwa faida ya walimwengu.

Thursday, January 26, 2012

Africonexion: Kampuni Chipukizi

Mwaka 2002 nilisajili kampuni katika jimbo la Minnesota ambayo niliita Africonexion. Nilichagua aina ya usajili iitwayo "sole proprietorship." Yaani mmiliki na mhusika mkuu ni mimi.

Nilianzisha Africonexion kama chombo cha kushughulikia elimu kuhusu tamaduni duniani, kwa kuandika, kuchapisha, na kuuza vitabu, na kutoa mihadhara na ushauri kwa watu binafsi, mashirika, taasisi, makampuni, na kadhalika, kama ninavyoripoti mara kwa mara katika blogu zangu.


Africonexion ni kampuni ndogo sana kwa wakati huu, kwa maana kwamba sina timu ya wafanyakazi au washiriki. Lakini nimeitumia vizuri kama fursa ya kujielimisha, kwa kuzingatia kuwa elimu ni mtaji bora kuliko hata fedha. Shughuli zote ninazofanya, iwe ni kuandika au kutoa mihadhara au ushauri kwa watu binafsi, ni kama shule kwangu. Hii picha hapa kushoto ilipigwa wakati wa maonesho fulani Brooklyn Park, Minnesota.



Ninataka kuipeleka kampuni hii Tanzania na kwingineko. Nimeshaendesha warsha Dar es Salaam, Zanzibar na Pemba, Tanga, na Arusha. Pia nilishiriki maonesho ya elimu na ajira yaliyofanyika Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam. Hapa kushoto naonekana na wadau kwenye meza yangu. Nilishiriki maonesho hayo ili kuwapata wadau wa kujiunga nami, kwani nimejenga msingi mzuri wa uzoefu, na mtandao thabiti, huku Marekani. Lakini, kutokana na shughuli zangu, watu hao inabidi wawe wapenda vitabu na elimu kwa ujumla.

Tuesday, September 7, 2010

Watoto wa Tanzania Wanapenda Vitabu

Wengi wetu tunalalamika kuhusu kufifia au kutoweka kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu miongoni mwa wa-Tanzania. Inaonekana kuwa hata pale ambapo vitabu vipo, kama vile maktaba, wa-Tanzania hawaendi kusoma.

Ukweli ni kuwa tabia hii inajengeka na umri. Watoto wa Tanzania, wanapenda vitabu, sawa na watoto wengine popote. Nimeshuhudia hayo katika pita pita zangu Tanzania. Kwa mfano, ukienda kwenye maonesho ya vitabu Tanzania, utawaona watoto.

Mwanzoni mwa Septemba, 2004, kulikuwa na maonesho ya vitabu katika uwanja wa hifadhi ya kumbukumbu za Taifa, Dar es Salaam. Kama kawaida, waliohudhuria zaidi ni watoto.

Katika maonesho hayo, watoto wa shule walifanya michezo ya kuigiza, kuhusu umuhimu wa vitabu.
Waliimba pia nyimbo, wakiwahamasisha wazazi kuweka vitabu nyumbani na kuwa na utaratibu wa kusoma pamoja na watoto. Lakini, ujumbe wao uliishia hewani, kwani wazazi wenyewe hawakuwepo.

Wakati wa kuigiza mchezo, watoto hao walishika vitabu, kama vilelelezo. Nilimwona mtoto mmoja ameshika kijitabu changu kuhusu Things Fall Apart. Anaonekana hapa juu, wa pili kutoka kulia. Niliguswa na jambo hilo.

Mwaka huu, tarehe 24-25 Juni nilishiriki maonesho ya elimu na ajira, ambayo yaliandaliwa na Tripod Media. Yalifanyika Diamond Jubilee Hall, Dar es Salaam.
Nililipia banda, nikaweka vitabu vyangu na machapisho mengine, nikawa naongea na watu kwa siku zote mbili.

Walifika watoto wengi, na hapo nilijionea mwenyewe jinsi watoto walivyo na ari ya vitabu. Walikuwa wanaviangalia na waliniuliza masuali kem kem.
Nami nilitumia fursa hii kuwaelezea umuhimu wa kusoma na kutafuta elimu kwa dhati muda wote.



Nilipata faraja kubwa katika kuwa na watoto hao na kuona moyo wao juu ya vitabu.



Suali la msingi linabaki: Tufanyeje ili watoto waweze kukua na moyo huu walio nao bila kulegea au kufifia? Kuna njia gani ya kuwafanya watu wazima wahudhurie maonesho ya vitabu?

Katika jarida la Tanzania Schools Collection, toleo la kwanza, Moris Mwavizo anaripoti, ukurasa 12, kuwa katika maonesho fulani ya vitabu Dar es Salaam, mratibu mmoja alimwona mtoto akizunguka mwenyewe katika viwanja. Alipomwuliza kwa nini baba yake hakuja naye, mtoto alijibu kuwa baba yake angekuja kama kungekuwa na bia hapa kwenye maonesho. Je, hii si aibu?

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...