Showing posts with label uuzaji wa vitabu. Show all posts
Showing posts with label uuzaji wa vitabu. Show all posts

Sunday, February 12, 2017

Nimemaliza Kusoma The Highly Paid Expert

Leo nimemaliza kusoma The Highly Paid Expert, kitabu kilichotungwa na Debbie Allen, ambacho nilikitaja katika blogu hii. Nimekifurahia kitabu hiki, kwa jinsi kilivyoelezea misingi na mbinu za kumwezesha mtu kuwa mtoa ushauri mwenye mafanikio kwake na kwa wateja.

Mambo anayoelezea mwandishi Debbie Allen yananihusu moja kwa moja katika ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Kwa hivi, kitabu hiki kimekuwa na mvuto wa pekee kwangu. Nimevutiwa na namna mwandishi anavyoelezea mbinu za mtu kujijenga katika uwanja wake hadi kufikia kileleni. Anaelezea mategemeo ya wateja na namna ya kushughulika nao. Anaelezea umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wataalam wengine, matumizi ya tekinolojia katika kuwasiliana na wateja, kuendesha mikutano, na kujitangaza. Vile vile anasisitiza uaminifu na uwajibikaji.

Ameelezea vizuri namna wengi wetu tunavyoshindwa kujitangaza na tunavyoshindwa au kusita kutambua umaarufu na umuhimu wetu na thamani ya ujuzi wetu, jambo ambalo linatufanya tusitegemee malipo yanayoendana na ubingwa wetu. Tunaridhika na malipo hafifu, wakati tulistahili malipo makubwa.

Sura ya 24 ya The Highly Paid Expert inaelezea uandishi wa kitabu. Mwandishi anasema kuwa kitabu ni nyenzo muhimu ya mtaalam katika fani yake. Kitabu kinamjengea sifa na kuonekana. Kinamfanya mtaalam aaminike. Mwandishi anaeleza wazi kuwa kitabu hakileti utajiri, bali kinafungua milango ya fursa.

Hayo nimejionea mwenyewe. Kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimenifungulia fursa nyingi. Nimepata mialiko ya kwenda kutoa mihadhara au ushauri katika taasisi na jumuia mbali mbali, kama vile makanisa, vyuo, na makampuni.

Nimevutiwa na mambo anayoelezea mwandishi wa The Highly Paid Expert kuhusu uandishi na uuzaji wa kitabu. Yanafanana na yale ambayo nami nimekuwa nikieleza katika blogu hii. Kwa mfano, anasema kuwa jukumu kubwa la kutangaza na kuuza kitabu ni la mwandishi.

The Highly Paid Expert ni kati ya vitabu ambavyo nimevifurahia kwa dhati. Mawaidha yake mengi ni ya kukumbukwa daima. Mfano ni msisitizo wake juu ya kushirikiana na wengine. Mtu hufanikiwi kwa uwezo wako mwenyewe tu na kutojihusisha na wengine wenye utaalam, hata kama ni washindani wako.

Saturday, May 9, 2015

Neno Jingine Kuhusu Uandishi na Uchapishaji

Mimi ni mwandishi wa vitabu. Ninaandika vitabu vya tahakiki ya fasihi, juu ya masuala ya jamii, fasihi simulizi, na masuala ya athari za tofauti za tamaduni, hali halisi ya uandishi wa vitabu, mbinu za kujichapishia vitabu. Naandika kuhusu utangazaji na uuzaji wa vitabu, na kuhusu hali halisi ya usomaji wa vitabu Tanzania na ughaibuni.

Ninatoa ushauri kwa wengine kupitia blogu hii na katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Yeyote anayetaka kujifunza kutoka kwangu anaweza kufanya hivyo, bila kipingamizi. Lakini namtegemea aanze kwa kusoma nilichoandika, mawasiano ya ziada yafuate baadaye.

Siwezi kuwasiliana na kila mtu na kuongelea hata yale ambayo tayari nimeshaandika. Nina kazi yangu na majukumu mengine kila siku. Nikisema niwasiliane na kila mtu hata kwa yale ambayo nimeshaandika, nitashindwa kufanya kazi zangu zinazoniwezesha kuishi, kulipia nyumba, matibabu, na mahitaji mengine.

Labda niache kazi niliyoajiriwa kufanya, nijiajiri kama mshauri. Ikiwa hivyo, kila anayetafuta ushauri kwangu atatakiwa alipie. Ndivyo wanavyofanya watoa ushauri. Nami ujuzi na uzoefu ninao, kama inavyodhihirika katika taarifa ninazoandika katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza.

Suali ambalo ninaulizwa tena na tena ni kuhusu mikakati ya kuchapisha miswada. Ni wazi kuwa watu bado wana fikra za jadi kuhusu uchapishaji. Nawashauri waondokane na fikra za kuwateemea wachapishaji. Badala yake, waingie katika ulimwengu wa kujichapishia vitabu.

Wafanyeje au waanzie wapi ndio aima ya masuala ninayoongelea katika blogu na katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Kama mtu anataka mafanikio, ni lazima awekeze katika elimu inayohusiana na shughuli anayotaka kufanya. Kununua vitabu na kuvisoma ni uwekezaji, sawa na uwekezaji wa kununua trekta ya kilimo au nyavu za kuvulia samaki.

 Suala la kujichapishia vitabu ni tata, hasa kwa upande wa wanataaluma. Jadi iliyopo katika kuchapisha vitabu vya kitaaluma au makala za kitaaluma imekuwa ya kuzingatia umuhimu wa wanataaluma tofauti na mwandishi kufanya uhakiki na udhibiti wa andiko kabla ya kuchapishwa. Ninapangia kuandika zaidi kuhusu suala hilo.  

Monday, March 2, 2015

Nimeulizwa Inakuwaje Siuzi Vitabu Vyangu Tanzania

Leo katika mtandao wa Facebook kuna mdau kaniuliza inakuwaje siuzi vitabu vyangu Tanzania. Nimemshukuru kwa ulizo lake, nikajaribu kulijibu. Napenda kuandika machache kuhusu suali hili.

Napenda kuanza kwa kusema kuwa vitabu hivyo vinapatikana mtandaoni, kama vile kwenye tovuti ya lulu na tovuti ya Amazon. Yeyote mwenye kadi ya "credit" kama vile VISA au MasterCard, anaweza kuvinunua. Haijalishi kama yuko Chake Chake, Dar es Salaam au Tukuyu. Ataletewa. Kama ana kifaa kama "kindle," ananunua bila tatizo.

Ninafahamu kuwa ni wa-Tanzania wachache walioko Tanzania wanaoweza kununua vitu mtandaoni. Lakini kuna maelfu ya wa-Tanzania katika nchi kama Marekani wenye hizo kadi. Kama kuna nia ya dhati ya kununua kitabu, haikosekani njia.

Mimi mwenyewe nimekuwa tayari kufanya mipango na wa-Tanzania wenye nia ya kuuza vitabu vyangu, kwa kuwapelekea. Nimewahi kufanya hivyo na Cultural Tourism Program (Longido), Bougainvillea Lodge (Karatu), na Cultural Tourism Program (Mto wa Mbu).

Kila inapowezekana, nafanya mpango wa kuvifikisha vitabu vyangu kwenye matamasha nchini Tanzania, kama ilivyoelezwa hapa.

Kwa kuwa mimi si mfanyabiashara, ningependa kuona wafanyabiashara wanajipatia faida kutokana vitabu vyangu. Duka la vitabu chuoni St. Olaf linauza vitabu vyangu kwa bei kubwa kuliko mtandaoni. Vile vile, nilipotembelea chuo cha South Central, katika duka la vitabu walikuwa wanauza kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kwa dola 17.95.

Hata hivi, huwa najiuliza ni wa-Tanzania wepi wanaotaka kusoma vitabu vyangu. Sijaona kama kuna utamaduni wa kununua na kusoma vitabu. Wa-Marekani ndio wasomaji wangu wakuu, kama ninavyobainisha mara kwa mara katika blogu hii. Kwa vyovyote, kuepusha lawama, na kuwatendea haki wa-Tanzania wanaoamini nina jambo la kuwaambia, najitahidi kuhakikisha vitabu vyangu vinapatikana Tanzania.

Wednesday, February 25, 2015

Yatokanayo na Mihadhara ya Jana Chuoni South Central

Tangu nilipomaliza ziara yangu chuoni South Central jana, nimekuwa na furaha kutokana na mafanikio ya ziara ile. Kuanzia jana ile ile, taarifa zimeenea za kuisifia ziara ile. Mfano ni namna mwenyeji wangu, Mwalimu Becky Fjelland Davis, alivyoandika katika blogu yake. Ninafurahi kuwa sikumwangusha, kwani katika kuandaa ujio wangu, alikuwa ameutangazia umma kama ifuatavyo:

Come one, come all, to hear what he has to say. You'll be touched by his wisdom and wit, as well as his gentle demeanor.

Mwalimu Fjelland Davis aliandika hivyo kwa kujiamini, kwani alishanialika mwaka 2013 kuongea na wanafunzi wake, kama alivyoripoti katika blogu yake.

Kwa kuwa nilialikwa ili nikaongelee masuala yaliyomo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nimefurahi kuona jinsi ziara yangu ilivyotekeleza mategemeo ya waandaaji na wote waliohudhuria  mihadhara yangu.

Ninafurahi kuwa ziara ya jana imefanyika mwezi huu, ambapo ninasherehekea kutimia kwa miaka kumi tangu nilipochapisha kitabu hiki. Pia ni faraja kwangu, baada ya miezi mingi ya kuwa katika matatizo ya afya. Nakumbuka kauli ya wahenga kuwa baada ya dhiki, faraja.

Makala hii fupi haiwezi kumaliza tathmini ya ziara ya jana. Kumbukumbu itaendelea mawazoni mwangu na katika jamii. Ila kuna jambo moja ambalo napenda kulitaja. Duka la vitabu la chuoni South Central lilikuwa linauza kitabu changu kwa dola 17.95. Ukifananisha na bei yake ya dola 13 niliyoweka mtandaoni, ni wazi kuwa mwuzaji anajipatia faida. Hakuna kizuizi kwa muuzaji yeyote kujipangia bei yake.

Tuesday, January 11, 2011

Wauza Vitabu wa Mitaani Dar es Salaam

Kitu kimojawapo kinachonivutia ninapokuwa Dar es Salaam ni wauza vitabu wa mitaani. Wako wa aina mbili. Wako wenye sehemu maalum ya kuuzia vitabu, iwe ni meza tu au kibanda. Hao wanaonekana sehemu mbali mbali za mjini Dar es Salaam, kuanzia katikati ya mji, kama vile barabara ya Samora, hadi sehemu za pembeni, kama vile Mwenge na Ubungo. Picha iliyoko hapa kushoto niliipiga Ubungo, mwaka jana, karibu na kituo kikuu cha mabasi. Pembeni ya mwuza vitabu kuna kibanda cha muuza machungwa.

Wako wauza vitabu wengine ambao hutembeza vitabu mitaani, sawa na wale vijana ambao wanatembeza bidhaa mbali mbali, ambao tunawaita machinga. Hapo kushoto kuna picha niliyopiga Sinza Kijiweni, mwaka jana, kwenye hoteli ya Deluxe.



Nilikuwa hapo, na hao vijana wawili wakaja, mmoja akiuza vitabu na mwingine peni za kuandikia. Nilivutiwa, nikaanza kuongea nao. Nilimwuliza huyu muuza vitabu kuhusu wateja, na kama wa-Tanzania wananunua vitabu, akanielezea uzoefu wake. Nilinunua vitabu viwili. Kimoja ni tafsiri ya maneno ya ki-Ingereza kwenda ki-Swahili, na kingine ni tafsiri ya maneno ya ki-Swahili kwenda ki-Ingereza. Vyote vimechapishwa Kenya, na walengwa ni wageni wanaotembelea Afrika Mashariki. Ni vijitabu vidogo vidogo sana, kimoja cha kurasa 30 na kingine kurasa 32.

Karibu na lango la kituo cha mabasi Ubungo nilipiga picha iliyo hapa kushoto, mwaka jana, baada ya kumwomba kijana mwenye kibanda hicho. Tuliongea kuhusu biashara yake, naye alinieleza kuwa biashara inaenda vizuri, ila ingekuwa nzuri zaidi kama angekuwa na mtaji wa kutosha ili kuwa na meza kubwa zaidi na vitabu vingi zaidi. Nilifurahi kusikia hivyo, ushahidi kuwa wako watu wanaonunua vitabu. Kinachobaki ni kufuatilia zaidi kuona ni watu wa aina gani. Yule kijana niliyeongea naye Sinza alisema kuwa wanaonunua vitabu zaidi ni watu wa Zambia. Nitafuatilia zaidi suala hili siku zijazo, panapo majaliwa.

Katika pitapita yangu na kuangalia nimeona kuwa kuna vitabu vya aina nyingi humo mitaani, kuanzia hadithi za waandishi maarufu wa sehemu mbali mbali za dunia, hadi taaluma mbali mbali. Kuna vitabu vilivyotumika na vipya pia. Mtu makini anaweza kujipatia vitabu vingi vya manufaa kutoka kwa hao wauzaji wa mitaani akawa na maktaba binafsi ya kueleweka.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...