Showing posts with label Becky Fjelland Davis. Show all posts
Showing posts with label Becky Fjelland Davis. Show all posts

Wednesday, February 25, 2015

Yatokanayo na Mihadhara ya Jana Chuoni South Central

Tangu nilipomaliza ziara yangu chuoni South Central jana, nimekuwa na furaha kutokana na mafanikio ya ziara ile. Kuanzia jana ile ile, taarifa zimeenea za kuisifia ziara ile. Mfano ni namna mwenyeji wangu, Mwalimu Becky Fjelland Davis, alivyoandika katika blogu yake. Ninafurahi kuwa sikumwangusha, kwani katika kuandaa ujio wangu, alikuwa ameutangazia umma kama ifuatavyo:

Come one, come all, to hear what he has to say. You'll be touched by his wisdom and wit, as well as his gentle demeanor.

Mwalimu Fjelland Davis aliandika hivyo kwa kujiamini, kwani alishanialika mwaka 2013 kuongea na wanafunzi wake, kama alivyoripoti katika blogu yake.

Kwa kuwa nilialikwa ili nikaongelee masuala yaliyomo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nimefurahi kuona jinsi ziara yangu ilivyotekeleza mategemeo ya waandaaji na wote waliohudhuria  mihadhara yangu.

Ninafurahi kuwa ziara ya jana imefanyika mwezi huu, ambapo ninasherehekea kutimia kwa miaka kumi tangu nilipochapisha kitabu hiki. Pia ni faraja kwangu, baada ya miezi mingi ya kuwa katika matatizo ya afya. Nakumbuka kauli ya wahenga kuwa baada ya dhiki, faraja.

Makala hii fupi haiwezi kumaliza tathmini ya ziara ya jana. Kumbukumbu itaendelea mawazoni mwangu na katika jamii. Ila kuna jambo moja ambalo napenda kulitaja. Duka la vitabu la chuoni South Central lilikuwa linauza kitabu changu kwa dola 17.95. Ukifananisha na bei yake ya dola 13 niliyoweka mtandaoni, ni wazi kuwa mwuzaji anajipatia faida. Hakuna kizuizi kwa muuzaji yeyote kujipangia bei yake.

Sunday, January 25, 2015

Mipango ya Ziara Yangu Mankato Inaendelea

Kama nilivyoandika katika blogu hii, nitakwenda kuongea na wanafunzi wa chuo cha South Central mjini Mankato. Mipango ya ziara hii, ambayo itafanyika tarehe 24 Februari, inaendelea vizuri.

Mwenyeji wangu, mwalimu Rebecca Fjelland Davis, amenieleza kuwa shughuli ya kwanza nitakayofanya siku hiyo ni kuongea na wanafunzi katika darasa lake, kuanzia saa nne hadi saa tano na dakika hamsini asubuhi. Hao ni wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya kimasomo Afrika Kusini. Kama sehemu ya maandalizi hayo, wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na maongezi yangu nao yatahusu yale niliyoandika kitabuni.

Baada ya darasa hilo, kuanzia yapata saa sita, nitatoa mhadhara kwa wanachuo na wana jamii. Mwalimu Fjelland Davis ameniarifu kuwa duka la vitabu la hapo chuoni litakuwa limeandaa nakala za kitabu changu, kwa ajili ya kuuza. Kama ilivyo desturi hapa Marekani, nategemea kuwa baada ya mazungumzo nitasaini nakala za vitabu.

Hii sio mara yangu ya kwanza kufanya shughuli mjini Mankato. Nimewahi kwenda kutoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Mankato kwa wanachuo waliokuwa wanajiandaa kwenda Afrika Kusini. Nilialikwa na Profesa Scott Fee, ambaye ni muasisi na mratibu wa mpango wa ushirikiano baina ya chuo kikuu cha Mankato na chuo kiitwacho Eden Campus cha Afrika Kusini. Nakumbuka ukumbi ulivyojaa watu siku hiyo, nami kwa kutekeleza ombi la Profesa Fee, niliwasilisha nakala yapata 40 za Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimewahi pia kushiriki maonesho ya Deep Valley Book Festival, na mengine yaliyofanyika katika uwanja wa maonesho ya magari, ambao jina lake nimesahau. Ningekuwa na blogu miaka ile, ningekuwa nimeandika taarifa. Siku nyingine nilialikwa Mankato na taasisi inayoshughulika na huduma kwa jamii, nikaongea na wahamiaji na wakimbizi kutoka nchi mbali mbali, kama vile Somalia, Ethiopia, na Sudani. Mazungumzo hayo yaliripotiwa katika gazeti la Mankato Free Press.

Nikirudi kwenye mwaliko wa tarehe 24 Februari, napenda kusema kuwa Mwalimu Fjelland Davis na Profesa Scott Fee wanashirikiana katika mpango wa kupeleka wanafunzi Afrika Kusini. Wote wawili walihusika katika mhadhara niliotoa kwa wanafunzi wao ambao taarifa yake iliandikwa hapa na hapa.

Wednesday, December 17, 2014

Mwaliko Mwingine

Leo nimepata mwaliko mwingine wa kwenda kuzungumza na wanachuo wa chuo cha South Central ambao wanajiandaa kwa safari ya masomo Afrika Kusini. Mwaliko umetoka kwa mwalimu wao, Becky Djelland Davis. Hii ni mara pili yeye kunialika. Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka jana, naye baadaye aliandika kuhusu mazungumzo yale katika blogu yake.

Nami nimeguswa kwa namna alivyoniandikia leo:

I will be taking students to South Africa again in May. This coming semester, we will again be reading your book Africans and Americans. I hope that perhaps you can talk with my students again? They loved you last time!

Huu ni mwaliko wa tatu kwa siku za hivi karibuni, na yote inangojea utekelezaji katika miezi michache ijayo. Wa kwanza niliuelezea hapa, na wa pili hapa. Mialiko hii ninayopata sio jambo jepesi au la mteremko. Inahitaji tafakari katika kujiandaa ili nitoe mawazo na mitazamo ya kiwango kinachokidhi mahitaji ya hao wanaonialika, na bora zaidi ni kufanya vizuri kuliko wanavyotegemea.

Hiyo inawezekana kutokana na juhudi ya kutafiti na kutafakari mambo kwa kina na upeo mpana zaidi ya yale yaliyomo katika kitabu changu, ambacho ndicho kinachochea hii mialiko. Sijioni kama ni mtaalam, bali mtafutaji wa elimu.

Kwa kuhitimisha, sherti nikiri kuwa ninafurahi kuona kuwa watu walionialika kabla wanaendelea kufanya hivyo, nami siwezi kuwaangusha. Hii ndio habari moja muhimu ya leo, ambayo nimeona niiwekee kumbukumbu katika blogu yangu hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...