Monday, March 2, 2015

Nimeulizwa Inakuwaje Siuzi Vitabu Vyangu Tanzania

Leo katika mtandao wa Facebook kuna mdau kaniuliza inakuwaje siuzi vitabu vyangu Tanzania. Nimemshukuru kwa ulizo lake, nikajaribu kulijibu. Napenda kuandika machache kuhusu suali hili.

Napenda kuanza kwa kusema kuwa vitabu hivyo vinapatikana mtandaoni, kama vile kwenye tovuti ya lulu na tovuti ya Amazon. Yeyote mwenye kadi ya "credit" kama vile VISA au MasterCard, anaweza kuvinunua. Haijalishi kama yuko Chake Chake, Dar es Salaam au Tukuyu. Ataletewa. Kama ana kifaa kama "kindle," ananunua bila tatizo.

Ninafahamu kuwa ni wa-Tanzania wachache walioko Tanzania wanaoweza kununua vitu mtandaoni. Lakini kuna maelfu ya wa-Tanzania katika nchi kama Marekani wenye hizo kadi. Kama kuna nia ya dhati ya kununua kitabu, haikosekani njia.

Mimi mwenyewe nimekuwa tayari kufanya mipango na wa-Tanzania wenye nia ya kuuza vitabu vyangu, kwa kuwapelekea. Nimewahi kufanya hivyo na Cultural Tourism Program (Longido), Bougainvillea Lodge (Karatu), na Cultural Tourism Program (Mto wa Mbu).

Kila inapowezekana, nafanya mpango wa kuvifikisha vitabu vyangu kwenye matamasha nchini Tanzania, kama ilivyoelezwa hapa.

Kwa kuwa mimi si mfanyabiashara, ningependa kuona wafanyabiashara wanajipatia faida kutokana vitabu vyangu. Duka la vitabu chuoni St. Olaf linauza vitabu vyangu kwa bei kubwa kuliko mtandaoni. Vile vile, nilipotembelea chuo cha South Central, katika duka la vitabu walikuwa wanauza kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kwa dola 17.95.

Hata hivi, huwa najiuliza ni wa-Tanzania wepi wanaotaka kusoma vitabu vyangu. Sijaona kama kuna utamaduni wa kununua na kusoma vitabu. Wa-Marekani ndio wasomaji wangu wakuu, kama ninavyobainisha mara kwa mara katika blogu hii. Kwa vyovyote, kuepusha lawama, na kuwatendea haki wa-Tanzania wanaoamini nina jambo la kuwaambia, najitahidi kuhakikisha vitabu vyangu vinapatikana Tanzania.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...