Showing posts with label maadili. Show all posts
Showing posts with label maadili. Show all posts

Tuesday, December 17, 2019

Kofia ya CCM Nchini China

Naleta picha ya ujumbe wa CCM kwenye kikao na wenyeji wao mjini Shanghai, China, mwaka 2018. Hapo mezani upande wa kushoto kuna kofia ya CCM. Yawezekana walikwenda ziarani na magwanda yao na vikofia. Je, kuna sababu gani mimi kuandika ujumbe kuhusu kofia? Sina jambo la maana zaidi la kuongelea? Kwa nini nisiongelee madhumuni ya ziara na mafanikio yake?

Ninaandika ujumbe huu kama mtafiti, mwandishi, na mtoa ushauri juu ya masuala ya utamaduni na utandawazi. Nimekuwa nikifanya shughuli hizo hapa Marekani na Tanzania pia, ambako nimeendesha warsha mara kadhaa kuanzia mwaka 2008 katika miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam.

Ninajaribu kuwaelewesha watu kuwa tofauti za tamaduni zina athari kubwa, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Tunapokutana na watu wa tamaduni tofauti na wetu, tuwe makini. Tunaweza tukaelewana vibaya, au tunaweza tusielewane. Ni muhimu tujielimishe kuhusu tofauti hizo kabla hayajatupata hayo.

Kofia ya CCM ni sehemu ya vazi rasmi la wana CCM. Ni utambulisho wao. Hata mimi ambaye sina chama ninawatambua kwa mavazi yao. Vyama vingine navyo vina mavazi yao. Kwa hapa nchini Tanzania, hakuna utata juu ya hayo mavazi. Lakini je, hali ni hiyo hiyo nje ya Tanzania kwenye tamaduni tofauti?

Nchini China, kofia ya kijani ni mkosi. Mwanaume kuvaa kofia ya kijani maana yake anatangaza kwamba mke wake ni mzinzi.

Kuhusu asili ya tafsiri hii ya waChina kuhusu kofia ya kijani, maelezo yanatofautiana. Baadhi ya maelezo ni kwamba zamani za kale, ndugu wa malaya walilazimishwa kuvaa kofia ya kijani wabebe aibu. Maelezo mengine ni kwamba zamani za kale, wahudumu katika madanguro walikuwa wanavaa kofia za kijani. Lakini kama nilivyogusia, maelezo yanahitilafiana. Ila jambo ambalo halina utata ni kwamba katika utamaduni wa China, kofia ya kijani ni mkosi kwani inatangaza habari ya uzinifu wa mke.

Sasa fikiria hiyo ziara ya ujumbe wa CCM China. Wafikirie wako sehemu mbali mbali kama wageni rasmi, wamevalia kofia za kijani. Bila shaka, wenyeji wao walifanya ukarimu na heshima kama ilivyo desturi. Lakini bila shaka, makada hao wa CCM watakuwa wameacha gumzo na taswira ambayo hawakutegemea.

Katika warsha ambazo nimeandaa Tanzania tangu mwaka 2008, waTanzania wachache sana wamekuwa wakihudhuria. Mbali ya warsha, nimekuwa nikielezea katika blogu zangu masuala ya athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Nimeandika hata kitabu, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapatikana Tanzania pia, kutoka katika maduka ya Kimahama (Arusha), Soma Book Cafe (Dar es salaam), na A Novel Idea (Arusha na Dar es Salaam).

Pamoja na kujaribu njia zote hizo, nimeona kuwa labda, kwa kuandika ujumbe huu kuhusu kofia ya CCM nchini China, waTanzania watanielewa vizuri na watachukua hatua stahiki katika masuala yote husikka, iwe ni mahusiano binafsi, biashara za kimataifa, utalii, diplomasia na kadhalika.

Wednesday, December 14, 2016

Wosia wa Rabindranath Tagore Kuhusu Uhuru wa Kutoa Maoni

Rabindranath Tagore ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa waliowahi kuishi. Alizaliwa mwaka 1861 Calcutta na kufariki 1941. Aliheshimika duniani kote wakati wa uhai wake na bado anaheshimika. Aliandika mashairi, tamthilia, insha, riwaya, hadithi fupi, na pia maelfu ya barua. Niliwahi kufundisha utungo wake maarufu Gitanjali, hapa chuoni St. Olaf.

Tagore alikuwa mwalimu aliyetukuka, kioo cha ubinadamu wa kweli ("humanism"), mwenye fikra pevu na nzito juu ya maisha na maadili. Watu maarufu kama W.B. Yeats, Mahatma Gandhi na Albert Einstein, walimmwenzi sana. Mwaka 1913 alipata tuzo ya Nobel katika fasihi. Nina vitabu vyake vitatu, kimojawapo kikiwa Rabindranath Tagore: An Anthology.

Kutoka katika kitabu hiki nimenukuu sehemu ya ujumbe wa tarehe 25 Septemba, 1930, kwa gazeti la Izvestia la Urusi. Ni ujumbe unaopaswa kutafakariwa na kuzingatiwa, tunaposhuhudia ukandamizaji wa uhuru wa watu kujieleza. Ili kuufikisha ujumbe kwa watu wasiojua ki-Ingereza, nimejaribu kuutafsiri.

     There must be disagreement where minds are allowed to be free. It would not only be an uninteresting but sterile world of mechanical regularity if all our opinions were forcibly made alike. If you have a mission which includes all humanity, you must, for the sake of that living humanity, acknowledge the existence of differences of opinion. Opinions are constantly changed and re-changed only through the free circulation of intellectual forces and moral persuasion. Violence begets violence and blind stupidity. Freedom of mind is needed for the reception of truth; terror hopelessly kills it. The brute cannot subdue the brute. It is only the man who can do it.

Tafsiri

     Lazima pawepo na kutokubaliana mahali ambapo akili zinaruhusiwa kuwa huru. Dunia itakuwa sio tu haipendezi bali tasa yenye kwenda kwa mwendo ule ule kama mashine, iwapo maoni yetu yote yatalazimishwa kufanana. Kama watu mna malengo yanayowahusu wanadamu kwa ujumla wao, sherti, kwa manufaa ya uhai wa jamii hiyo ya wanadamu, kutambua uwepo wa tofauti za maoni. Maoni hubadilishwa bila ukomo pale tu panapokuwa na mzunguko huru wa nguvu za akili na ushawishi wa mwenendo wa kimaadili. Mabavu huzaa mabavu na ujinga mithili ya upofu. Uhuru wa akili unahitajika ili ukweli upokelewe, na vitisho huua kabisa ukweli huo. Hayawani hawezi kumdhibiti hayawani. Ni binadamu tu ndiye anaweza.

Tuesday, November 22, 2016

Ninaendelea Kusoma "Hamlet"

Miaka miwili iliyopita, niliandika katika blogu hii kuwa nina tabia ya kusoma vitabu kiholela. Wakati wowote nina vitabu kadhaa ninavyovisoma, bila mpangilio maalum, na pengine bila nia ya kufikia mwisho wa kitabu chochote.

Kusoma kwa namna hii hakuna ubaya wowote, bali kuna manufaa. Nilipokuwa mwanafunzi wa sekondari, katika seminari ya Likonde, mwalimu wetu, Padri Lambert OSB alituhimiza tuwe na mazoea ya kusoma sana vitabu, na pia mazoea ya kuvipitia vitabu kijuu juu, ambayo kwa ki-Ingereza huitwa "browsing."

Nikiachilia mbali vitabu ninavyofundisha, wakati huu nimezama zaidi katika kusoma Hamlet, kama nilivyoandika katika blogu hii. Ninasoma Hamlet pole pole, ili kuyanasa vizuri akilini yaliyomo, hasa maudhui kuhusu maisha, maadili, na tabia za binadamu. Kusoma pole pole kunaniwezesha kukifurahia ki-Ingereza cha Shakespeare, ingawa si rahisi kama ki-Ingereza tunachotumia leo.

Tofauti kati ya ki-Ingereza cha leo na kile cha Shakespeare ninaifananisha na tofauti kati ya ki-Swahili cha leo na kile cha mashairi ya zamani kama yale ya Muyaka au Utenzi wa Rasi lGhuli. Kwa msingi huo, kusoma utungo kama Hamlet ni chemsha bongo inayoboresha akili, sawa na mazoezi ya viungo yanavyoboresha afya ya mwili.

Mwandishi maarufu Ernest Hemingway alielezea vizuri thamani ya vitabu aliposema, "There is no friend as a loyal as a book," yaani hakuna rafiki wa kweli kama kitabu. Ujumbe uko wazi, nami sina la kuongeza. Kitabu bora ukishakinunua, ni rafiki wa kudumu.


  

Tuesday, August 18, 2015

Warsha Kuhusu Jamii na Taaluma Inaendelea

Siku chache zilizopia niliandika katika blogu hii kuhusu warsha tuliyokuwa tunaisibiri hapa chuoni St. Olaf juu ya jamii na taaluma. Warsha hiyo ilianza jana; tulijadili sura kadhaa za kitabu cha Martha C. Nussbaum, Not for Profit: Why Democracy Needs the Humanities.

Kitabu hiki kinaelezea namna mwelekeo wa elimu ya juu unavyochepuka kutoka katika hali yake ya asili na unavyoingia katika mkondo wa kibiashara. Malengo ya elimu, ambayo yanapaswa kuwa kumjenga mtu na jamii katika tabia ya kutafakari, kuhoji mambo, kujitambua, na kuwa na mahusiano mema, ya ushirikiano na kusaidiana, yamekuwa yakibadilika. Malengo hayo sasa ni kuwaandaa watu kwa ajira na uzalishaji wa mali.

Not for Profit kinaongelea umuhimu wa elimu katika demokrasia. Kwa kuiingiza elimu katika mfumo wa biashara, tunahujumu demokrasia na mahusiano bora ulimwenguni. Nilifurahi kusoma katika kitabu hiki nadharia za mabingwa niliowasoma nilipokuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam: Socrates, Jean Jacques Rousseau, Johann Pestalozzi, na John Dewey. Ningefurahi zaidi iwapo nadharia za Paulo Freire zingekuwemo pia, kwani huyu ni mwelimishaji maarufu aliyeonyesha njia ya kuifanya elimu kuwa nyenzo ya mapinduzi.

Nilifunguka akili niliposoma kuwa Rabindranath Tagore alikuwa mwelimishaji, sio tu kinadharia, bali kwa kuanzisha na kuendesha vyuo. Tangu zamani nilimfahamu Tagore kama mwandishi maarufu wa riwaya, tamthilia na mashairi, aliyepata tuzo ya Nobel mwaka 1913. Niliwahi kufundisha kitabu chake maarufu, Gitanjali, hapa chuoni St. Olaf. Lakini sikuwa nimefuatilia mchango wake ulivyoelezwa katika Not for Profit.

Leo tumejadili sura kadhaa za kitabu cha Stanley Fish, Versions of Academic Freedom: From Professionalism to Revolution. Fish anafafanua vizuri dhana ya uhuru wa taaluma, kwa kuangalia mitazamo mbali mbali iliyopo kuhusu dhana hiyo. Ameweka wazi masuali muhimu kuhusu dhana ya uhuru wa taaluma. Kwa mfano, uhuru wa taaluma ni haki ya kikatiba? Kwa nini waalimu katika elimu ya juu wanaamini wana haki ya kuwa na uhuru wa taaluma mpana kuliko uhuru walio nao wananchi wengine? Wanafunzi nao wanao au wanastahili uhuru huo?

Fish anaongelea pia masuala ya mtazamo wa kisiasa wa waalimu katika vyuo vikuu, na uhusiano wa maadili na uhuru wa taaluma. Tulipokuwa tunajadili suala hilo la maadili, profesa mwenzetu mmoja alielezea alivyowahi kukataa kuchora michoro ya kuboresha muundo wa ndege za kivita za jeshi la Marekani.

Kama ilivyokuwa jana, mjadala wa leo ulikuwa mzuri na wa kuelimisha. Nimefurahi kuvisoma vitabu viwili nilivyovitaja hapo juu. Kesho tutajadili Professors and their Politics, kitabu kilichohaririwa na Neil Gross na Solon Simmons.

Thursday, June 25, 2015

Habari ya Malipo ya Mhadhara Chuoni Winona

Jumanne wiki hii, nilikwenda Chuo Kikuu cha Winona kutoa mhadhara, kama nilivyoandika katika blogu hii. Katika safari kama hii, kuna mambo mengi, na haiwezekani kuyaongelea yote. Hata hivi, naona ni vizuri tu kuelezea angalau yale yenye umuhimu Fulani kwangu na labda kwa wengine. Napenda kuongelea suala la malipo ya mhadhara ule.

Wakati nilipoombwa kwenda kutoa mhadhara, mhusika aliniuliza malipo yangu ni kiasi gani. Huu ni utaratibu hapa Marekani, nami kama ilivyo kawaida yangu, nilimwambia kuwa siweki kipaumbele kwenye malipo, bali kutoa huduma itakiwayo. Kama wanaonialika wana uwezo wa kunilipa, kwangu ni sawa, kama wana uwezo kidogo, kwangu ni sawa, na kama hawana uwezo, kwangu ni sawa pia. Niko tayari kuitikia mwito kwa hali yoyote. Nilidhani suala lilikuwa limeishia hapo.

Siku kadhaa baadaye, mhusika alinielezea tena habari ya malipo, akataja kiasi ambacho angeweza kunilipa, kutokana na bajeti yake. Nilimjibu kuwa sina tatizo, nikamshukuru. Alipoleta mkataba, ambao ulitaja kiasi hicho cha malipo, niliusaini bila kusita, nikamrudishia.

Siku ilipofika, yaani hiyo tarehe 23 Juni, binti yangu Zawadi nami tulikwenda Chuoni Winona. Tulikaribishwa vizuri, tukaingia kwenye ukumbi wa mkutano wakati huo huo wanafunzi walipokuwa wanaingia. Baada ya kila mtu kuketi, mwenyeji wangu alisimama kunitambulisha. Alisema tunaye mgeni hapa, Dr. Mbele, profesa wa Chuo cha St. Olaf. Ni mtu ambaye nimemfahamu kwa miaka kadhaa, na nimemwomba aje atoe mhadhara.

Hadi hapo, sikuona kitu cha pekee, kwani huo ni utaratibu wa kawaida. Kilichokuwa cha pekee ni pale alipoanza kuelezea mazungumzo yetu juu ya malipo. Aliwaambia wanafunzi kuwa Dr. Mbele aliniambia kuwa hajali kama nina malipo kiasi gani ya kumpa, angekuja tu. Nasikitika kuwa kiasi nilichoweza kumwekea hakifanani na umaarufu wake. Niko njiani kutafuta hela kwa program nyingine, niweze kumwalika na kumlipa kiwango anachostahili.

Kwa kweli, sikutegemea angesema yote hayo, na nilimsikiliza kwa kumhurumia kwa jinsi alivyoonekana kujisikia vibaya kwamba ameshindwa kunitayarishia malipo ninayostahili. Nilifarijika alipomaliza maelezo yake na kunikaribisha nitoe mhadhara.

Baada ya mhadhara, mwenyeji wangu aliniongoza kwenda ofisini kwake, akanipa fomu ya malipo nisaini. Kisha akanipa cheki. Nilishangaa kuona cheki ilikuwa imezidi kile kiwango alichoniambia mwanzo. Nikaona kuwa alikuwa amejitahidi alivyoweza kuvuka kile kiwango tulichokubaliana. Na bado aliendelea kulalamika kuwa angeridhika kama angenilipa ninavyostahili.

Nimeona niongelee jambo hili, kwani ni kati ya mambo ambayo sitayasahau. Pia ni jambo lenye maana kwangu. Nimetamka tena na tena kuwa siweki pesa mbele, bali huduma. Hata hivi, ninafahamu jinsi wa-Marekani wanavyojali malipo. Wanazingatia umuhimu wa kumlipa mtu kile wanachoona ni haki yake.

Ningeweza kusema kuwa ninapaswa kuzingatia umuhimu wa kufuata utamaduni wa mahali nilipo. Lakini suala hili la malipo bado ni mtihani kwangu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Ninaamini kuwa kwa kuzingatia huduma kwa wanadamu, badala ya ubinafsi, sipotezi chochote. Badala yake, Mungu ananibariki. Ninaishi na raha moyoni. Ninafurahi kwamba binti yangu alishuhudia yote niliyoeleza hapo juu. Labda yatamsaidia maishani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...