Showing posts with label demokrasia. Show all posts
Showing posts with label demokrasia. Show all posts

Saturday, May 13, 2017

Msikilize Raia wa Marekani Anavyomrarua Kiongozi

Jambo moja linalonivutia kuhusu Marekani ni uhuru wa kujieleza. Katiba ya Marekani inalinda uhuru huo kikamilifu. Kwa mfano, kulikuwa na kesi dhidi ya mtu aliyechoma moto bendera ya Taifa, lakini mahakama kuu iliamua na imeendelea kusisitiza kuwa kuchoma moto bendera ya Taifa ni sehemu ya uhuru wa kujieleza, ambao unalindwa na katiba. Mahakama kuu inasisitiza kuwa kauli tata, za kukera, au za kuwakosoa watawala ndizo hasa katiba ilikusudiwa kuzilinda.

Serikali ya Marekani inafahamu kuwa raia ana uhuru na haki kamili ya kuikosoa. Viongozi wa Marekani wanajua hilo. Ninaleta video hapa, inayomwonyesha mwananchi akimfokea kiongozi bila kumung'unya maneno. Mwone kiongozi huyu kutoka chama tawala cha Rais Donald Trump alivyonywea, wakati kipigo kinaendelea.

Monday, September 28, 2015

Kampeni za CCM Mwaka Huu

Najaribu kutafakari picha hii iliyopigwa katika moja ya mikutano ya kampeni za uchaguzi zinazoendelea Tanzania. Ina maana kwamba mwenye uwezo wa kupiga "push-up" nyingi ndio anafaa kuwa kiongozi? Je, ili uukwae ubunge, unatakiwa upige angalau "push-up" ngapi? Udiwani je? Na ili uwe waziri, unahitaji "push-up" ngapi? Na kwa uwaziri, ni sahihi tuwe na "push-up" tu au na kuruka viunzi pia? Na kwa kuzingatia uzito wa cheo cha uwaziri, kwa nini tusiongezee pia uwezo wa kunyanyua matofali angalau manne ya zege? Kwa kweli, tukifanya hivyo, tutapata serikali imara kabisa.

Tuesday, August 18, 2015

Warsha Kuhusu Jamii na Taaluma Inaendelea

Siku chache zilizopia niliandika katika blogu hii kuhusu warsha tuliyokuwa tunaisibiri hapa chuoni St. Olaf juu ya jamii na taaluma. Warsha hiyo ilianza jana; tulijadili sura kadhaa za kitabu cha Martha C. Nussbaum, Not for Profit: Why Democracy Needs the Humanities.

Kitabu hiki kinaelezea namna mwelekeo wa elimu ya juu unavyochepuka kutoka katika hali yake ya asili na unavyoingia katika mkondo wa kibiashara. Malengo ya elimu, ambayo yanapaswa kuwa kumjenga mtu na jamii katika tabia ya kutafakari, kuhoji mambo, kujitambua, na kuwa na mahusiano mema, ya ushirikiano na kusaidiana, yamekuwa yakibadilika. Malengo hayo sasa ni kuwaandaa watu kwa ajira na uzalishaji wa mali.

Not for Profit kinaongelea umuhimu wa elimu katika demokrasia. Kwa kuiingiza elimu katika mfumo wa biashara, tunahujumu demokrasia na mahusiano bora ulimwenguni. Nilifurahi kusoma katika kitabu hiki nadharia za mabingwa niliowasoma nilipokuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam: Socrates, Jean Jacques Rousseau, Johann Pestalozzi, na John Dewey. Ningefurahi zaidi iwapo nadharia za Paulo Freire zingekuwemo pia, kwani huyu ni mwelimishaji maarufu aliyeonyesha njia ya kuifanya elimu kuwa nyenzo ya mapinduzi.

Nilifunguka akili niliposoma kuwa Rabindranath Tagore alikuwa mwelimishaji, sio tu kinadharia, bali kwa kuanzisha na kuendesha vyuo. Tangu zamani nilimfahamu Tagore kama mwandishi maarufu wa riwaya, tamthilia na mashairi, aliyepata tuzo ya Nobel mwaka 1913. Niliwahi kufundisha kitabu chake maarufu, Gitanjali, hapa chuoni St. Olaf. Lakini sikuwa nimefuatilia mchango wake ulivyoelezwa katika Not for Profit.

Leo tumejadili sura kadhaa za kitabu cha Stanley Fish, Versions of Academic Freedom: From Professionalism to Revolution. Fish anafafanua vizuri dhana ya uhuru wa taaluma, kwa kuangalia mitazamo mbali mbali iliyopo kuhusu dhana hiyo. Ameweka wazi masuali muhimu kuhusu dhana ya uhuru wa taaluma. Kwa mfano, uhuru wa taaluma ni haki ya kikatiba? Kwa nini waalimu katika elimu ya juu wanaamini wana haki ya kuwa na uhuru wa taaluma mpana kuliko uhuru walio nao wananchi wengine? Wanafunzi nao wanao au wanastahili uhuru huo?

Fish anaongelea pia masuala ya mtazamo wa kisiasa wa waalimu katika vyuo vikuu, na uhusiano wa maadili na uhuru wa taaluma. Tulipokuwa tunajadili suala hilo la maadili, profesa mwenzetu mmoja alielezea alivyowahi kukataa kuchora michoro ya kuboresha muundo wa ndege za kivita za jeshi la Marekani.

Kama ilivyokuwa jana, mjadala wa leo ulikuwa mzuri na wa kuelimisha. Nimefurahi kuvisoma vitabu viwili nilivyovitaja hapo juu. Kesho tutajadili Professors and their Politics, kitabu kilichohaririwa na Neil Gross na Solon Simmons.

Wednesday, April 1, 2015

Tunahitaji Demokrasia, Lakini Tunahitaji Vyama vya Siasa?

Bila shaka tutakubaliana kuwa tunahitaji demokrasia, yaani mfumo wa utawala ambao ni wa umma, unaendeshwa na umma, kwa maslahi ya umma. Kwa ki-Ingereza wanasema "rule of the people, by the people and for the people."

Hii ndio maana na tafsiri ya demokrasia. Lakini je, tunahitaji chama cha siasa? Tunahitaji vyama vya siasa? Ni lini wa-Tanzania walikaa na kulitafakari suali hili? Kwa kweli hawajawahi kufanya tafakari hii. Badala yake wamekurupuka na wazo la chama au vyama, kikasuku tu.

Hata wale tunaowaita wasomi wetu nao wameshindwa kuhoji hali hii. Wameshindwa kujinasua kutokana na mtazamo huu, badala ya kufanya kile kinachoitwa kwa ki-Ingereza "thinking outside the box."

Nimeelezea zaidi huu ukurupukaji, mkanganyiko, na ukasuku wa wa-Tanzania katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Tuesday, May 24, 2011

Nataka Tanzania Isitawalike Kamwe

Nataka Tanzania isitawalike kamwe. Kama hupendi kusikia hayo, shauri lako. Mimi si mwanachama wa chama chochote cha siasa, ila nataka Tanzania isitawalike.

Nataka Tanzania iwe na viongozi, sio watawala. Wanaotaka kutawala wasipate nafasi hiyo. Uongozi unahitaji busara na ushawishi, kukubalika na jamii husika. Kama ni kutawaliwa, tulitawaliwa na wakoloni. Masultani walikuwa wanatawala. Walikuwa wakandamizaji, sawa na wakoloni. Wazee wetu walipambana hadi Uhuru ukapatikana.

Nataka nchi yetu iimarishe misingi ya Uhuru na demokrasia. Kutawala ni suala la mabavu, kwani hakuna jamii inayokubali kutawaliwa, labda iwe ni jamii ya wajinga, au waoga, au ambao wamelishwa sana kasumba ili wasitambue haki zao.

Lakini jamii inayojitambua, inayotambua maana ya uhuru, haki, na demokrasia, jamii inayothamini na kutetea hayo, haiwezi kutawalika, labda kwa mabavu na vitisho. Itakuwa ni jambo la kuhuzunisha iwapo Tanzania itatawalika. Nataka tuwe macho, tuwe makini, nchi yetu isitawalike, kamwe.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...