Showing posts with label mialiko.. Show all posts
Showing posts with label mialiko.. Show all posts

Monday, August 7, 2017

Global Minnesota Wameniletea Kifuta Jasho

Juzi, tarehe 5, niliandika katika blogu hii kwamba nilikuwa nimepata barua ya shukrani kutoka Global Minnesota, kufuatia mhadhara niliotoa. Leo, bila kutegemea, nimepata cheki kutoka kwao, kama kifuta jasho.

Sikutegemea, kwani tangu mwanzo waliponialika kutoa mhadhara na hata baada ya mhadhara, sikuwa na hata fununu kwamba kuna kifuta jasho. Nami sikufikiria wala kutegemea. Nilichojali ni kufanya kazi waliyoniomba kufanya, yaani kujadili mada ya "African Folktales to Contemporary Authors."

Ninaongozwa na nasaha ya wahenga kwamba tenda wema nenda zako; usingoje shukrani. Kama nilivyosema katika blogu hii, mengine ni matokeo. Sijawahi kukataa mwaliko wa kwenda kutoa mhadhara kwa sababu ya malipo.

Watu wanaonihimiza nisitoe huduma bila malipo ninawaambia kuwa kuna baraka katika kuwasaidia watu. Fursa ya kutoa mhadhara ni ya manufaa kwangu, kwani inaniongezea uzoefu na kuniwezesha kujitathmini ufahamu wangu, hasa katika kipindi cha masuali na majibu. Vile vile matangazo ya mhadhara yanayoandaliwa na kusambazwa na wale wanaonialika yananiongezea kufahamika.

Mara nyingi, huwezi kujua watu unaowahutubia ni akina nani katika jamii. Nimeshuhudia baada ya mhadhara watu wakijitokeza na kujitambulisha kwangu na kuniuliza iwapo nitakuwa tayari kuhutubia kwenye taasisi au jumuia zao. Mwaliko moja unazaa mialiko mingine. Ninasema hayo ili kuwashawishi wale wanaosita kutoa huduma bila kuahidiwa malipo. Hakuna hasara, bali ni faida.

Thursday, June 25, 2015

Habari ya Malipo ya Mhadhara Chuoni Winona

Jumanne wiki hii, nilikwenda Chuo Kikuu cha Winona kutoa mhadhara, kama nilivyoandika katika blogu hii. Katika safari kama hii, kuna mambo mengi, na haiwezekani kuyaongelea yote. Hata hivi, naona ni vizuri tu kuelezea angalau yale yenye umuhimu Fulani kwangu na labda kwa wengine. Napenda kuongelea suala la malipo ya mhadhara ule.

Wakati nilipoombwa kwenda kutoa mhadhara, mhusika aliniuliza malipo yangu ni kiasi gani. Huu ni utaratibu hapa Marekani, nami kama ilivyo kawaida yangu, nilimwambia kuwa siweki kipaumbele kwenye malipo, bali kutoa huduma itakiwayo. Kama wanaonialika wana uwezo wa kunilipa, kwangu ni sawa, kama wana uwezo kidogo, kwangu ni sawa, na kama hawana uwezo, kwangu ni sawa pia. Niko tayari kuitikia mwito kwa hali yoyote. Nilidhani suala lilikuwa limeishia hapo.

Siku kadhaa baadaye, mhusika alinielezea tena habari ya malipo, akataja kiasi ambacho angeweza kunilipa, kutokana na bajeti yake. Nilimjibu kuwa sina tatizo, nikamshukuru. Alipoleta mkataba, ambao ulitaja kiasi hicho cha malipo, niliusaini bila kusita, nikamrudishia.

Siku ilipofika, yaani hiyo tarehe 23 Juni, binti yangu Zawadi nami tulikwenda Chuoni Winona. Tulikaribishwa vizuri, tukaingia kwenye ukumbi wa mkutano wakati huo huo wanafunzi walipokuwa wanaingia. Baada ya kila mtu kuketi, mwenyeji wangu alisimama kunitambulisha. Alisema tunaye mgeni hapa, Dr. Mbele, profesa wa Chuo cha St. Olaf. Ni mtu ambaye nimemfahamu kwa miaka kadhaa, na nimemwomba aje atoe mhadhara.

Hadi hapo, sikuona kitu cha pekee, kwani huo ni utaratibu wa kawaida. Kilichokuwa cha pekee ni pale alipoanza kuelezea mazungumzo yetu juu ya malipo. Aliwaambia wanafunzi kuwa Dr. Mbele aliniambia kuwa hajali kama nina malipo kiasi gani ya kumpa, angekuja tu. Nasikitika kuwa kiasi nilichoweza kumwekea hakifanani na umaarufu wake. Niko njiani kutafuta hela kwa program nyingine, niweze kumwalika na kumlipa kiwango anachostahili.

Kwa kweli, sikutegemea angesema yote hayo, na nilimsikiliza kwa kumhurumia kwa jinsi alivyoonekana kujisikia vibaya kwamba ameshindwa kunitayarishia malipo ninayostahili. Nilifarijika alipomaliza maelezo yake na kunikaribisha nitoe mhadhara.

Baada ya mhadhara, mwenyeji wangu aliniongoza kwenda ofisini kwake, akanipa fomu ya malipo nisaini. Kisha akanipa cheki. Nilishangaa kuona cheki ilikuwa imezidi kile kiwango alichoniambia mwanzo. Nikaona kuwa alikuwa amejitahidi alivyoweza kuvuka kile kiwango tulichokubaliana. Na bado aliendelea kulalamika kuwa angeridhika kama angenilipa ninavyostahili.

Nimeona niongelee jambo hili, kwani ni kati ya mambo ambayo sitayasahau. Pia ni jambo lenye maana kwangu. Nimetamka tena na tena kuwa siweki pesa mbele, bali huduma. Hata hivi, ninafahamu jinsi wa-Marekani wanavyojali malipo. Wanazingatia umuhimu wa kumlipa mtu kile wanachoona ni haki yake.

Ningeweza kusema kuwa ninapaswa kuzingatia umuhimu wa kufuata utamaduni wa mahali nilipo. Lakini suala hili la malipo bado ni mtihani kwangu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Ninaamini kuwa kwa kuzingatia huduma kwa wanadamu, badala ya ubinafsi, sipotezi chochote. Badala yake, Mungu ananibariki. Ninaishi na raha moyoni. Ninafurahi kwamba binti yangu alishuhudia yote niliyoeleza hapo juu. Labda yatamsaidia maishani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...