Showing posts with label biashara. Show all posts
Showing posts with label biashara. Show all posts

Sunday, June 3, 2018

Vitendea Kazi vya Kampuni Yangu

Mwaka 2002, nilianzisha na kusajili kampuni ambayo niliita Africonexion, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nilisajili kama kampuni binafsi, usajili ambao hapa Marekani hujulikana kama "sole proprietorship." Niliamua kuanzisha na kusajili kampuni hii ya kutoaelimu na ushauri wa masuala ya utamaduni kwa kuwa tayari nilikuwa na uzoefu wa shughuli hizo, nikihudumia vyuo, makanisa, mashirika, jumuia na watu binafsi.

Shughuli zangu hizi zimekuwa na mafanikio makubwa, kwa maana kwamba nimewasaidia watu kuelewa na kuepukana na mambo ambayo yanaweza kusababisha migogoro na kutoelewana. Wale ambao tayari walishakumbana na migogoro na kutoelewana nimewasaidia kufahamu kwa nini walijikuta katika migogoro na kutoelewana. Lakini mimi mwenyewe nimefanikiwa pia kujifunza mengi katika shughuli zote hizo.

Napenda kuelezea siri moja kubwa ya mafanikio haya. Siri hiyo ni kujielimisha kwa kutumia vitabu. Vitabu ndio vitendea kazi vyangu. Sichoki kununua na kusoma vitabu. Kulingana na shughuli za kampuni yangu, ninanunua na ninasoma vitabu kuhusu masuala kama utandawazi, utamaduni, na saikolojia. Jana, kwa mfano, bila kutegemea, nilikiona kitabu kiitwacho Riding the Waves of Culture, katika duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilipokiona tu, nilitambua kuwa kitakuwa kitendea kazi muhimu.

Mbali na kutumia vitabu vya wengine, ninatumia pia kitabu nilichoandika mwenyewe, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitabu hiki kilitokana na uzoefu nilioongelea hapa juu. Si mimi tu ambaye ninakichukulia kitabu hiki kama kitendea kazi muhimu. Mifano ni profesa na mwandishi maarufu Becky Fjelland Brooks, ambaye aliakiongelea kitabu katika blogu yake. Mzee Patrick Hemingway, ambaye aliwahi kuishi Tanzania miaka yapata ishirini na tano, aliwahi kuniambia kuwa kitabu hiki ni "a tool of survival" yaani kimbilio la usalama.

Hili suala la kuviona vitabu kama vitendea kazi ni muhimu. Hainiingii akilini mtu aanzishe biashara, kwa mfano, halafu asitafute na kusoma vitabu au maandishi mengine juu ya uendeshaji wa biashara. Atafanikishaje malengo yake kama hafahamu vitu kama saikolojia ya binadamu, ambao ndio wateja wake? Atafanikiwaje kama hafahamu namna ya kuwasiliana na watu? Kama wateja wake ni wa tamaduni tofauti na utamaduni wake, ni muhimu mno afahamu tofauti hizo.

Nilivutiwa na msimamo wa Mama Barbro Finskas Mushendwa, mmiliki wa kampuni ya utalii ya J.M Tours, yenye makao yake Arusha, Tanzania. Baada ya kusoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliamua kununua nakala kadhaa kwa ajili ya wafanyakazi wake, ambao walikuwa ni madreva wa watalii. Aliona haraka kuwa kitabu hiki kinafaa kama kitendea kazi na madreva wake walinithibitishia hivyo, kama nilivyoripoti katika blogu ya ki-Ingereza.

Mmiliki wa kampuni yoyote anajua ulazima wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta, sawa na mkulima navyojua ulazima wa jembe na shoka. Lakini sijui ni wamiliki wa makampuni na wafanya biashara wangapi wa Tanzania wenye mtazamo kama wa Mama Mushendwa, wa kutambua kuwa vitabu ni vitendea kazi. Ninaona wanaanzisha kampuni au biashara na kuziendesha kimazoea,  au kwa kutegemea kudra ya Mungu au hata waganga wa kienyeji. Daima ninaona matangazo ya waganga wa kienyeji wakinadi dawa za mafanikio kibiashara.

Ninapoongelea mada hii ya vitabu kama vitendea kazi, ninakumbuka juhudi aliyofanya Mwalimu Nyerere katika kutekeleza kile alichoita elimu yenye manufaa. Aliwahimiza watu kujisomea ili kuboresha shughuli walizokuwa wanafanya. Chini ya uongozi wake, vilichapishwa na kusambazwa vitabu kuhusu kilimo, uvuvi, useremala, na kadhalika. Ninakumbuka kwamba kijijini kwangu, vitabu hivyo vilihifadhiwa katika nyumba ya baba yangu.

Pamoja na mimi kutumia vitabu vya wengine kama vitendea kazi, ninashukuru kwamba nami ni mwandishi. Ninapangia kuendelea kuandika ili kuchangia ufanisi katika shughuli zangu na za wengine.

Tuesday, February 6, 2018

Mteja Anapokupigia Debe

Tarehe 3 Februari, nilipata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa dada au mama ambaye amejitambulisha kwa jina la Cynthia, ila simjui. Ameandika kuulizia kitabu changu namna hii:

Hello,

I am planning a trip to Tanzania and someone recommended your book about cultural differences between Africans and Americans. How can I purchase your book? Thank you very much.

Kwa wasiojua ki-Ingereza, tafsiri yake ni hii:

Habari

Ninapanga safari ya kwenda Tanzania na mtu fulani alikipendekeza kitabu chako juu ya tofauti za tamaduni za wa-Afrika na wa-Marekani. Nitakinunuaje kitabu chako? Shukrani sana.

Kwa mwandishi, habari ya aina hii ni habari njema. Kwamba mtu fulani ambaye alitumia hela zake kununulia kitabu chako alikisoma akaridhika au kufurahi kiasi cha kukipendekeza kwa mwingine, si jambo jepesi. Mtu anapopendekeza kitu kwa mwingine namna hii, anajiweka katika hali ya kueleweka vibaya, iwapo kile anachopendekeza hakitamridhisha huyu mwingine. Tunapendekeza vitu kwa marafiki zetu tukiwa na uhakika na hicho tunachopendekeza.

Sisi wote ni wateja wa hiki au kile, iwe ni vitu au huduma. Muda wote tunawashawishi wenzetu wakanunue kitu fulani au wanapohitaji huduma, tunawaelekeza sehemu ambayo tunaiamini. Tunapopendekeza kitu au huduma tunatoa tamko kuhusu ubora wa kile tunachopendekeza. Nimekuwa nikielezea masuala haya katika blogu hii.

Muda wote sisi binadamu tunafanya hii shughuli ya kupiga debe bila malipo. Tunafanya hiki kibarua kisicho na malipo bila hata kujitambua. Ni sehemu ya mazungumzo yetu na marafiki au watu wengine. Mwenye kuuza bidhaa au kutoa huduma anafaidika bila kutumia hela kulipia matangazo.

Hayo ni baadhi ya mawazo yangu wakati huu ninapotafakari suala la huyu mpiga debe asiyejulikana ambaye amekipendekeza kitabu changu kwa mtu huyu aitwaye Cynthia, ambaye naye simjui. Nimemjibu Cynthia nikamwambia sijui mahali alipo, lakini kitabu anaweza kukipata mtandaoni.

Sunday, May 21, 2017

"Contagious Success," Kitabu Muhimu

Nina furaha wakati huu kwa kuwa ninasoma kitabu kiitwacho Contagious Success: Spreading High Performance Throughout Your Organization. Nilinunua kitabu hiki siku chache zilizopita, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Sikupoteza fedha zangu.

Mwandishi wa kitabu hiki, mwenyekiti wa Hudson Highland Center for High Performance, ni mwenye ujuzi na uzoefu mkubwa. Kitabu chake hiki ni matokeo ya utafiti ulioshirikisha watu wa sehemu mbali mbali ulimwenguni, ambao ni wafanyakazi katika sekta zinazotegemea na kuendeshwa na ujuzi na maarifa. Kwa ki-Ingereza, watu hao huitwa "knowledge workers." Hii ni dhana muhimu katika dunia ya leo na kesho, ambayo inaendelea kuwa dunia ya "knowledge economy."

Tangu mwanzo, kitabu hiki kina mafundisho muhimu kwa viongozi, mameneja, wamiliki wa biashara, watoa huduma na kadhalika. Ujumbe mahsusi ni namna ya kuyaeneza mafanikio katika shirika, kampuni, taasisi, au jamii. Mwandishi anasema: "Every company has high-performing workgroups that both make money for the business and develop new products, services, or markets. These work groups create environments in which results are achieved and people flourish."

Jambo muhimu kabisa ni kujenga mazingira ya kuwezesha ufanisi. Hata kama mtu ni hodari namna gani, hawezi kufanikiwa ipasavyo katika mazingira yasiyo muafaka. Mazingira ni msingi wa mafanikio, na ufanisi wa kikundikazi au vikundikazi unapata fursa ya kuenea katika kampuni au shirika zima.

Mwandishi ananukuu kauli za wataalam waliofafanua mawazo hayo: "According to Daniel Gilbert, Professor of psychology at Harvard University, 'Four decades of scientific research have shown that situations are powerful determinants of human behavior--and much more powerful determinants than most of us realize.'"

Baada ya maelezo, mwandishi analeta nukuu nyingine: "'Changing the situation and shaping the environment--that's what leadership is all about,' noted Linda Ginzel, clinical professor of managerial psychology at the University of Chicago Graduate School of Business."

Mwandishi anaelezea zaidi wazo hilo, na halafu analeta mawazo ya ziada. Kwanza, nyakati zimebadilika. Dunia ya leo si ile ya wakati mapinduzi ya viwanda ("Industrial Age") ambapo wafanyakazi walisimama katika mstari na uzalishaji wa bidhaa ulikuwa unatiririka kama mnyororo ("assembly line"). Wakati ule maamuzi ya namna kuendesha kiwanda yalikuwa mepesi na wazi kuliko sasa. Ushindani haukuwa mkubwa kama leo. Amri zilikuwa zinatoka juu kwa viongozi na kwenda chini, bila matatizo. Wafanya kazi waliwajibika kutii walichoambiwa. Hawakuhitaji kuwa wabunifu.

Leo mambo yamebadilika. Wafanyakazi hawatakiwi wawe watu wa kufuata tu maelekezo. Lazima watumie akili na ubunifu, kukabiliana na mazingira ya leo. Mazingira haya yanahitaji pia mabadiliko ya mtindo wa uongozi: "The strategies that worked in the Industrial Age are no longer effective. Leaders need to be honest about their own strengths and weaknesses. They must recognize that they can't be or do everything and, therefore, should make sure the people around them have complementary strengths."

Anaendelea kufafanua, kwa kunukuu kauli ya Carol Hymowitz katika Wall Street Journal:  "Arrogance is out of fashion in the executive suite. So are autocratic executives who rule by intimidation, think they have all the answers and don't believe they need to be accountable to anyone."

Kuhitimisha suala hili la uongozi mpya, mwandishi anasema kuwa uongozi ni lazima uwe unawathamini watu, unathamini ubunifu na uthubutu, na uwe mwepesi kuzitambua na kuzikamata fursa zinazojitokeza.

Nilivyokuwa ninasoma haya mawazo, nimejikuta nikiwazia Tanzania na malengo ya serikali ya kujenga nchi ya viwanda. Nimeona wazi kuwa ili tufanikiwe, lazima tujiweke sawa kwa mambo mengi, kama haya ya kuwathamini watu, kuweka mazingira muafaka na kuzingatia rasilimali watu, ambayo inakwenda sambamba na kuwapa watu uhuru wa kufikiri, kuwa wabunifu na watundu, hata kama kwa utundu wao wanaishia kufanya makosa. Watu wakiwa na uoga wa kufanya makosa, mafanikio yanaweza kuwa shida kupatikana.

Kitabu hiki cha Contagious Success nimekifurahia sio tu kwa sababu kinaelimisha sana, bali pia, kwa kiasi kikubwa, kwa sababu kimenikumbusha kitabu kingine, Leading Beyond the Walls, ambacho ninacho na nilikiongelea katika blogu hii.

Sunday, May 14, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilikwenda tena Apple Valley, kwa muda mfupi, nikaingia katika duka la Half Price Books. Niliangalia kwanza sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway au juu ya Hemingway. Kitabu cha pekee nilichokiona, ambacho nimekifahamu kwa miezi kadhaa ila sijakinunua, ni Hemingway's Boat: Everything He Loved in Life, And Lost, kilichotungwa na Paul Hendrickson.

Nilielekea sehemu ambapo huwekwa vitabu vya bei rahisi kabisa. Kwa kuwa sikuwa na muda mwingi, niliangalia haraka haraka, nikaona kitabu cha Matigari cha Ngugi wa Thiong'o, kilichotafsiriwa kwa ki-Ingereza na Wangui wa Goro. Ngugi alikuwa amekiandika kwa Kikuyu. Nilivutiwa kuona kuwa ni nakala ya jalada gumu, iliyochapishwa na Africa World Press. Nilichukua. Wasomaji wa Ngugi wanakumbuka kuwa tafsiri hii ilichapishwa kwanza na Heinemann.

Kisha, sehemu hiyo hiyo, katika kuchungulia chungulia, niliona kitabu Contagious Success: Spreading High Performance Throughout Your Organization, kilichoandikwa na Susan Lucia Annunzio. Nilivyoona kuwa kinahusu mbinu za kusambaza ufanisi katika makampuni na mashirika nilikichukua hima. Dhana ya maambukizi ya mafanikio ilinivutia.

Ninapenda kusoma vitabu vinavyohusu ujasiriamali na biashara, kwa sababu mimi mwenyewe ninajiona kama mjasiriamali jamii ("social enterpreneur"). Vile vile, ninavipenda vitabu hivi vinahusu masuala yenye uhusiano na taaluma ambazo nimezizoea, hasa saikolojia.

Friday, February 17, 2017

Umuhimu wa Kuzifahamu Tamaduni za Wengine

Mada ya tofauti za tamaduni na athari zake duniani ninaishughulikia sana. Kwa mfano, nimeandika kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nimeongelea suala hilo pia katika kitabu changu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Vile vile ninaliongelea mara kwa mara katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Umuhimu wa kuzifahamu tofauti za tamaduni unaonekana wazi wazi wakati tunapokumbana na matatizo katika mahusiano yetu na watu wa tamaduni ambazo si zetu. Tusijidanganye kwamba jambo hilo ni la kinadharia tu na kwamba halituhusu. Miaka michache iliyopita, wafanya biashara wa Tanzania walikwenda Oman kushiriki maonesho ya biashara. Walipata shida kutokana na kutojua utamaduni wa watu wa Oman. Taarifa hiyo iliandikwa katika blogu ya Michuzi.

Suala hili haliwahusu wafanya bashara tu, bali wengine pia, kama vile wanafunzi wanaokwenda nchi za nje, wanadiplomasia, watu wanaokwenda mikutanoni, na kadhalika. Kwa kuzingatia hayo, na kwa kuwa nimekuwa nikifanya utafiti katika masuala hayo, nimekuwa nikipata mialiko ya kutoa ushauri kwa jumuia na taasisi mbali mbali hapa Marekani. Vyuo vya Marekani, kwa mfano, vinapopeleka wanafunzi nchi za nje, kama vile nchi za Afrika, vinazingatia suala la kuwaandaa wanafunzi kwa kuwaelimisha kuhusu utamaduni wa huko waendako. Mwaka hadi mwaka nimealikwa kutoa elimu hiyo.

Nimewahi pia kuendesha semina Tanzania, kwenye miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam. Vile vile, kwa kuombwa na ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, niliwahi kutoa mihadhara Zanzibar na Pemba, juu ya utamaduni wa Marekani, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Kwa jinsi ninayofahamu umuhimu wa suala hili, nimekuwa nikikumbushia mara kwa mara kila ninapoweza. Kwa mfano, uhusiano ulipoanza kuimarika baina ya Tanzania na u-Turuki, nilikumbushia suala hilo katika blogu hii. Ningependa kuona suala hili la athari za tofauti za tamaduni linapewa kipaumbele katika maisha yetu kwani kulipuuzia ni kujitakia matatizo yasiyo ya lazima. Hii ndio sababu iliyonifanya nianzishe kampuni ya kutoa elimu na ushauri iitwayo Africonexion: Cultural Consultants.

Monday, January 30, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Highly Paid Expert"

Leo nilikwenda Minneapolis na wakati wa kurudi, nilipita Mall of America, kuangalia vitabu katika duka la Barnes & Noble. Nilitaka hasa kuona kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Niliangalia scheme vinapowekwa vitabu vya fasihi, nikakuta kitabu kipya juu ya Ernest Hemingway, Everybody Behaves Badly: The Backstory to 'The Sun Also Rises.' kilichoandikwa na Lesley M.M. Blume. Kwa kuwa nimezama sana katika uandishi wa Hemingway, maisha na falsafa yake, na kwa kuwa nimeshasoma The Sun Also Rises, nilitamani kukinunua kitabu hiki, ambacho, kwa maelezo niliyoyaona, kinazungumzia yaliyo nyuma ya pazia.

Sikuwa na hela za kutosha, kwa hivyo nikaamua kuangalia vitabu vingine. Nilitumia muda zaidi katika sehemu ya "Business/Management." Huwa ninapenda sana kununua na kusoma vitabu vya taaluma hii, kwani vinanifundisha mengi kuhusu mambo ya ujasiriamali na biashara. Taaluma hii inanisaidia katika kuendesha shughuli za kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants.

Hatimaye, nilikiona kitabu kilichonivutia kwa namna ya pekee, The Highly Paid Expert, kilichoandikwa na Debbie Allen.  Kwa mujibu maelezo nyuma ya kitabu, huyu mwandishi ni mtaalam maarufu katika mambo ya biashara na ujasiriamali. Niliangalia ndani, nikaona mada anazoongelea ni za kuelimisha kabisa, kama vile matumizi ya tekinolojia za mawasiliano na mitandao.

Niliona anatoa ushauri wa kusisimua. Kwa mfano, anasema kuwa ni lazima mtu unayetaka mafanikio katika shughuli zako, uwasaidie wengine kufanikiwa. Unavyowasaidia wengine wafanikiwe, unajijengea mtandao wenye manufaa kwako pia. Ubinafsi na uchoyo wa maarifa haukuletei mafanikio. Kitabu hiki kinavutia kwa jinsi mwandishi anavyothibitisha mawazo yake, ambayo kijuu juu yanaonekana kama ya mtu anayeota ndoto.

Kwa bahati niliweza kuimudu gharama ya kitabu hiki, nikakinunua na kuondoka zangu, kwani nilikuwa sina hela iliyosalia. Sijutii kununua vitabu. Vitabu vinavyoelimisha ni mtaji, kwani hakuna mtaji muhimu zaidi ya elimu. Kwa wajasiriamali, wafanya biashara, watoa huduma, na kwa kila mtu, elimu ni tegemeo na nguzo muhimu. Ulazima wa kununua vitabu ni sawa na ilivyo lazima kwa mkulima kununua pembejeo.

Tuesday, November 24, 2015

Kitabu Changu Bado Kiko Maoneshoni

Nimepita tena katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf, kama ilivyo kawaida yangu, kuangalia vitabu vipya, na pia kuangalia vitabu ambavyo maprofesa wa masomo mbali mbali wanapangia kufundisha.

Katika kuzunguka humo dukani, nilipita tena sehemu ambapo vinawekwa vitabu vilivyoandikwa na maprofesa wa chuo hiki. Kabla sijafika kwenye sehemu hiyo, macho yangu yalivutiwa na kitabu change cha Matengo Folktales, ambacho kilikuwa bado kiko sehemu maalum vinakowekwa vitabu ambavyo uongozi wa duka huamua kuvipa fursa ya kuonekana vizuri zaidi kwa kipindi fulani, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii.

Kuna mambo yanayonigusa kila niingiapo katika duka hili la vitabu na maduka mengine ya vitabu popote hapa Marekani. Kubwa zaidi ni jinsi wahudumu wanavyokuwa ni watu makini katika masuala ya vitabu. Wanajua habari za vitabu, na wanaweza kukuelimisha kwa namna mbali mbali. Hawako katika kazi hii kwa kubahatisha au kwa kubabaisha. Wanajua wanachokifanya. Unaweza kuingia katika duka la vitabu hapa Marekani bila mpango wa kununua kitabu, lakini ukianza kuongea na wahudumu, unaweza kujikuta umeelimishwa kuhusu vitabu fulani ukaishia kununua.

Katika haya maduka ya vyuo, nimeona wana huu utaratibu wa kuwa na sehemu ya kuweka vitabu vilivyoandikwa na maprofesa wa vyuo hivyo, na pengine pia vitabu vya watu waliohitimu zamani, ambao huitwa "alumni" (wanaume) au "alumnae" (wanawake). Ni namna mojawapo ambayo taasisi hizo huwatambua na kuwaenzi waalimu na wahitimu. Nami najisikia vizuri kama profesa wa chuo hiki cha St. Olaf kuwa kazi zangu zinatambuliwa, vikiwemo vitabu.

Kwa upande wa biashara, naona kuwa haya maduka ya vitabu ya vyuo vya Marekani yanaonyesha ubunifu wa kibiashara kwa kuweka vitabu vyetu namna hiyo. Mbali  ya wanafunzi, tuna wageni wengi wanaopita hapa chuoni kila siku, wakiwemo wazazi wa wanafunzi, wahitimu wa zamani, na wale wanaokuja kuangalia ubora wa chuo ili wawalete vijana wao kusoma hapa. Duka la vitabu ni sehemu moja muhimu wanamoingia. Humo wanakuwa na fursa ya kununua vitabu vyetu hasa inapokuwa kwamba wamesikia habari zetu. Kwa mfano, duka la St. Olaf limeshauza nakala mia kadhaa za vitabu vyangu.

Hayo ni baadhi ya mambo niliyojifunza katika suala hili ambayo nimeona niyaweke katika blogu yangu, kwa lugha rahisi kabisa. Labda yanaweza kuwa na manufaa kwa vyuo nchini mwangu.

Friday, June 19, 2015

Mteja Nimefurahia Huduma

Leo nilipeleka gari langu kwenye kituo cha Car Time hapa mjini Northfield kubadilishiwa "oil." Kwa hapa Marekani, inashauriwa kubadili "oil" kila baada ya kuendesha gari maili 3000. Sijui utaratibu wa Tanzania.

Kama ilivyo kawaida, nilipokewa vizuri, nikakaa sehemu ambapo wateja hungojea huduma. Baada ya dakika kama ishirini hivi, mtu aliyenipokea sehemu ya mapokezi alifika nilipokaa akachuchumaa kwa heshima zote na kuniambia kuwa mafundi walikuwa wamegundua kuwa gari langu linahitaji pia "tire rotation."

Kwa kuogopa kuwa labda ingekuwa gharama ambayo sikujiandaa kuimudu, nilimwuliza kwa utaratibu iwapo itakuwa gharama kiasi gani. Alinijibu kuwa hiyo "tire rotation" haitanigharimu. Nilimjibu kuwa nashukuru kwa huduma hiyo.

Dakika kama kumi tu baadaye. huyu jamaa aliiniita, kuniambia kuwa gari lilikuwa tayari. Alinikabidhi ufunguo na bili yangu, nikalipia, kisha nikashukuru na kuondoka zangu.

Huu ndio utamaduni niliouona hapa Marekani wa kuhudumia wateja. Nimewahi kuandika kuhusu huduma ya Car Time katika blogu hii,. Kila mahali nilipopita, hapa Marekani nimeona utamaduni huu wa kumjali mteja.

Sio mimi pekee mwenye uzoefu huo. Katika mahojiano yangu na Deus Gunza, m-Tanzania mwenzangu, tuliongelea suala hilo, tukakubaliana kuwa huu ndio utamaduni tunaouona hapa Marekani. Kwa upande wangu, nimejionea kuwa hata ukiingia baa, kama mhudumu yuko sehemu nyingine, ni kawaida kumwona meneja anakuja kwenye meza yako, kusafisha na kukuhudumia.

Katika baa za Tanzania, sijawahi kumwona meneja akifanya jambo kama hilo. Utamwona amekaa mahali anapiga gumzo na ulabu na marafiki zake, na akiona mteja umeingia na unangojea huduma, atakachofanya ni kuwaita wahudumu na kuwafokea kwa kukukalisha bila huduma. Sijawahi kumwona meneja akichukua kitambaa na kusafisha meza kwa ajili ya mteja na halafu kumletea kinywaji. Ni kama mwiko.

Kwa nini ninasimulia yote hayo? Ni kwa sababu nina nia ya dhati ya kuwasaidia wafanya biashara na watoa huduma wa Tanzania. Huduma bora kwa mteja ni msingi muhimu wa mafanikio. Hii imani kwamba mafanikio yanatokana na kwenda kwa mganga kusafisha nyota au kupata dawa ya mafanikio ni upuuzi.

Sijaona kampuni yoyote hapa Marekani inayoenda kwa waganga kutafuta dawa. Dawa muhimu ya uhakika ni kumridhisha au kumfurahisha mteja. Kama unauza bidhaa, uhakikishe bidhaa yako ni bora. Na kama biashara yako ni ya kutoa huduma, kama ile ushauri, uhakikishe huduma yako ni bora. Kwa vyovyote vile hakikisha mteja ameridhika au amefurahi. Huyu atakuwa mpiga debe wako. Ukimwudhi ataeneza habari kwa wengine na biashara yako itadhurika. Wataalam wanasema kuwa matangazo haya ya mdomo wanayofanya wateja ni msingi mkuu wa kufanikiwa au kuanguka kwa biashara.

Leo, niliporejea kutoka Car Time, nimemwelezea binti yangu Zawadi na mama watoto yote yaliyojiri, kwa furaha kubwa. Halafu jionee nilivyoandika hapa katika blogu. Nimekuwa mpiga debe wa Car Time bila wao kunilipa. Na ndivyo ilivyo katika maisha yetu. Utamsikia m-Tanzania anaisifia simu yake mpya ya "iPhone" au "smartphone" au "laptop" yake au kitu kingine, bila kutambua kuwa anaipigia debe kampuni ambayo haimlipi chochote, haimjui na wala haichangii uchumi wa Tanzania bali inajitajirisha. Tuna uwezo mkubwa sisi wateja. Laiti tungeutumia kuzitangaza bidhaa na huduma za ki-Tanzania.

Nimejifunza mengi katika kuishi hapa Marekani. Hili nililolieleza ni jambo moja. Ni elimu ambayo ninaitumia katika kuendeleza kampuni yangu ya ushauri ya Africonexion. Ninazingatia sana umuhimu wa kutoa huduma bora, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Friday, May 8, 2015

Going Visual: Kitabu Kuhusu Mawasiliano Kwa Taswira

Leo napenda kukiongelea kitabu kiitwacho Going Visual: Using Images to Enhance Productivity, Decision-Making and Profits, kilichoandikwa na Alexis Gerard na Bob Goldstein. Nilikinunua kitabu hiki miaka michache iliyopita. Kama ilivyo kawaid yangu ninaponunua kitabu, sikiweki katika maktaba yangu bila kukipitia angalau juu juu, ili nijue kinahusu nini.

Hivi ndivyo nilivyofanya niliponunua Going Visual. Niliona ni kitabu kinachoelezea maendeleo katika utumiaji wa taswira katika mawasiliano, kitabu kinachoelezea matokeo ya utafiti na uzoefu na mikakati ya matumizi ya taswira katika biashara na ujasiriamali. Kitabu kinaelezea jinsi tekinolojia ya kuzalisha, kuhifadhi, kuandaa, na kusambaza taswira, kuanzia za digitali hadi video, zinavyowezesha ufanisi katika biashara na ujasiriamali katika ulimwengu wa leo.

Wakati nilipokinunua kitabu hiki, nilikipitia juu juu, nikaelewa haya niliyoelezea. Lakini leo nimekitoa maktabani ili nikisome ipasavyo. Mada yake inanivutia, na ukweli kwamba sina ufahamu wa masuala yaliyomo umenipa shauku ya kufahamu.

Suala la mawasiliano tunalishughulikia katika usomaji na ufundishaji wa fasihi, kwani fasihi hutumia lugha, ambayo ni chombo mahsusi cha mawasiliano. Nadharia za lugha na fasihi zinatueleza mengi kuhusu mawasiliano. Mvuto wa kitabu cha Going Visual kwangu, na duku duku inayonisukuma kukisoma, ni hiyo mikakati na mbinu za kutumia taswira ambazo waandishi wa kitabu wanasema zinawanufaisha wafanya biashara na wajisiriamali wa leo.

Ninajiuliza: hizi mbinu ni zipi? Na hiyo mikakati ni ipi? Kwa hivi, ninaona ni muhimu nikisome kitabu hiki nielimike, ingawa siwezi kujiita mfanyabiashara au mjasiriamali. Elimu haina mwenyewe, haina mipaka, wala haina mwisho.

Friday, January 20, 2012

Kitabu cha m-Tanzania Kuhusu Usimamizi wa Fedha

Hatimaye, nimejipatia na kusoma nakala ya kitabu kiitwacho Taking Control of Your Money, kilichoandikwa na Juanita Puja Kilasara. Huyu ni binti m-Tanzania ambaye amejipambanua katika fani ya uhasibu na masuala ya fedha kwa ujumla. Habari za kitabu chake hiki niliziona kwanza katika tovuti ya wavuti, kwani kwenye ukurasa wa mbele pana sehemu inayotangaza vitabu vya wa-Tanzania.

Kitabu hiki kinaeleza kwa njia rahisi masuala mbali mbali ya kuzalisha fedha na matumizi ya fedha kwa namna ya kumsaidia mtu kuwa mwangalifu na kumfanya asonge mbele kimaisha. Kuna mawaidha mengi ya manufaa, hata katika masuala ya kuanzisha na kuendesha biashara na shughuli zingine za kujipatia kipato.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya dunia, hasa katika tekinolojia ya mawasiliano, kitabu hiki kinatoa dokezo mbali mbali za kumwezesha mtu kutumia fursa zilizopo mtandaoni. Ingekuwa vijana wa Tanzania wana mazoea ya kusoma vitabu, wakawa wanasoma vitabu kama hiki, hata suala la ajira wangeliangalia kwa upeo tofauti, kwani ni aina ya kitabu kinachofungua milango ya ujasiriamali. Nina jambo moja tu la kushauri, kwamba ingefaa kitafsiriwe pia katika ki-Swahili.

Unaweza kumsikiliza Juanita akiongelea kitabu chake hapa. Kitabu hiki kinapatikana sehemu mbali mbali, kama ilivyoelezwa hapa.

Monday, April 25, 2011

Msamvu, Morogoro

Blogu yangu hii ni sehemu ya mambo mengi binafsi, zikiwemo kumbukumbu. Leo najikumbusha kuhusu Msamvu, kitongoji cha mji wa Morogoro. Ni kumbukumbu ya ziara yangu ya mwaka jana, ambayo nilishaielezea kidogo katika blogu hii.

Morogoro ina vitongoji vingi, ambavyo sivijui kabisa au sivijui vizuri. Ila nimepata fursa ya kuifahamu Msamvu, maarufu kwa sababu ni kituo kikubwa cha mabasi.


Msamvu ni sehemu ya biashara. Kuna migahawa na vijiduka. Kwa wafanyabiashara ndogo ndogo, wasafiri ni wateja muhimu. Wageni kutoka ughaibuni wanapofika kwetu wanashangaa kuwa basi linaposimama, ghafla linavamiwa na wachuuzi wa kila aina ya bidhaa, ambazo hupitishwa madirishani, kuanzia matunda na biskuti hadi kadi za simu.

Kule mbele, kwenye miti, kuna hoteli na baa nzuri. Nimewahi kutua hapo mara mbili tatu, wakati nikingojea usafiri wa kwenda Dar es Salaam. Ni sehemu nzuri ya kupumzikia.

Friday, March 11, 2011

Mteja Nimefurahi

Juzi niliandika makala fupi, "Mteja ni Mfalme". Leo napenda kuendelea na mada hiyo, kutokana na jambo lililonitokea.

Nilipeleka kigari changu kwenye kampuni ya CarTime, kubadilisha "oil." Kama kawaida, wakati fundi anaendelea na shughuli, nilikuwa kwenye sehemu ya mapumziko ambako wateja hungojea magari yao. Baada ya muda, niliitwa na kuambiwa kuwa gari yangu tayari, nikalipia na kuchukua ufunguo. Kama kawaida, mhudumu wa hapo mapokezi alinishukuru.

Nilienda nje fundi alikopaki gari nikafungua mlango. Kwenye kiti cha mbele alikuwa ameweka karatasi ambayo picha yake nimeiweka hapa juu. Fundi makenika alikuwa ameiweka hapo. Ujumbe wake ni huu: Asante kwa kuchagua CarTime. Tumefurahi kuhudumia gari lako. Kama vile hii haitoshi, fundi ameshukuru tena na kuandika jina lake, Eric.

Katika makala yangu ya juzi niliongelea umuhimu wa kumridhisha mteja. Sasa leo hapa nimeweka mfano hai. Mimi kama mteja nimefurahi kwa huduma niliyopata. Lakini kwa hapa Marekani, hili si jambo la ajabu, kwani wenye biashara wanazingatia suala la huduma kwa mteja. Niliwahi kusema hivyo hata kwenye mahojiano niliyofanyiwa na Radio Mbao.

Kwa vile wanablogu tunafahamu kuwa blogu ni kama shule, na kwa kuzingatia kuwa watu wengi nchini wanasoma hizi blogu, nimeona niweke taarifa hii na mawazo mawili matatu yanayotakiwa kuzingatiwa na wafanyabiashara na watoa huduma wa Tanzania, ambao mara nyingi tunawalalamikia.

Niliwahi kuhudhuria semina ya biashara hapa Minnesota ambapo baadhi ya mambo yaliyosisitizwa ni kuwa unapokuwa na mteja, uwe makini sana. Ujue kuwa mteja huyu akiridhika na kufurahi, atakwenda kukutangazia biashara au huduma yako kwa marafiki na watu wengine.

Sisi wenyewe tunafanya hivyo kila siku. Tukiwa tumevaa nguo nzuri, halafu marafiki wakatuuliza tumenunua wapi, tunawatajia duka. Au watu wakituuliza hoteli nzuri iko wapi, tunawatajia. Waulize watu Dar es Salaam kitimoto safi kinapatikana wapi, watakutajia. Tukiona filamu nzuri, tunawaambia watu wengine na kuwahamasisha nao wakaione. Kwa maana hiyo, tunawapelekea wafanyabishara wateja bila wao kuingia gharama ya matangazo.

Katika semina hiyo hiyo tulionywa kwamba mteja akiudhika, atakwenda kutangaza habari mbaya kuhusu yaliyompata. Habari hiyo itaenea. Wale watakaosikia watawaambia wenzao, na inakuwa kama sumu ambayo itahujumu biashara au huduma yako.

Mimi mwenyewe mwaka jana nilikumbana na wahudumu wa ovyo katika hoteli moja mjini Arusha. Ni hoteli nzuri, na niliiipenda. Nililipia nikapelekwa chumbani. Baada ya muda kidogo nilihitaji msaada wa kurekebishiwa taa. Hapo ndipo nilipokumbana na uzembe usio kifani. Wahudumu walichelewa sana, na huenda hata walisahau. Nikawakumbusha. Bado hawakuja, nimi nikaendelea kuwangoja. Hatimaye nilienda chini walikokuweko nikaanza kuwafokea. Bosi wao naye akaja, nami nikamjumlisha katika mhadhara wangu wa jazba, nikaendelea kutema cheche na kuwapa vidonge wote. Hawakuwa na sababu kabisa ya kushindwa kutekeleza nilichokuwa nimewaambia.

Basi, kutokana na usumbufu walionipa, hata wakati huu ninapoandika sipendi hata kuiwazia hoteli ile. Inakuwa kama vile natonoshwa kidonda. Sina hamu ya kufikia tena katika hoteli ile. Bahati yao ni kuwa hapa sitataja jina lao. Wangenikoma.

Haya ndio mambo ambayo wenye biashara wanapaswa kuyaelewa na kuyazingatia. Inashangaza kwamba wengi nchini mwetu wanaamini kuwa jambo la kufanya ni kwenda kwa waganga wakapate dawa ya kuwavutia wateja. Inakuwaje sisi tuzingatie imani hizo wakati wenzetu kama hao CarTime hawatumii dawa?

Friday, February 25, 2011

SUPER MUHOGO: Unga Safi wa Muhogo

Katika pita pita zangu, nimeona tangazo kwenye blogu ya Lady JayDee la wajasiriamali wa Chanika, Dar es Salaam, wanaouza unga wa muhogo. Wamemwomba Lady JayDee awawekee tangazo hilo kwenye blogu yake, naye amefanya hivyo.

Nimevutiwa na jambo hili. Njia madhubuti ya kujenga uchumi wa nchi yetu ni kuzalisha bidhaa na kuziuza nje, ili tupate fedha za kigeni. Kuuza bidhaa zetu nje kunaleta ajira nchini.

Hili ni jambo rahisi kulielewa. Hata mimi ambaye sikusomea somo la uchumi nimeandika kuhusu suala hili katika kitabu changu cha CHANGAMOTO, nikielezea namna mbali mbali jinsi wa-Tanzania tunavyohujumu uchumi wa nchi yetu. Mfano moja ni jinsi tunavyozishabikia bidhaa za kutoka nchi za nje, bila kutambua kuwa tunawapa ajira watu wa nchi zingine. Wakati huo huo, wa-Tanzania wanalalamikia uhaba wa ajira nchini. Tunapaswa kuuza bidhaa na huduma kwa wengine.

Kutokana na yote hayo, nimevutiwa na hao wajasiriamali wanaouza unga wa muhogo. Nimeamua kusaidia kutangaza biashara yao hapa kwenye blogu yangu. Nawatakia mafanikio tele katika kuboresha maisha yao na kuinua uchumi wa nchi.

Sunday, March 28, 2010

Biashara Mtandaoni

Kadiri siku zinavyopita, neno tekinolojia linazidi kusikika miongoni mwa wa-Tanzania, kama ilivyo duniani kwa ujumla. Tekinolojia ya leo imetuletea mambo mengi, mojawapo likiwa ni mtandao. Ulimwengu unazidi kuunganishwa kwa tekinolojia ya mawasiliano ambayo kifupi tunaiita mtandao.

Lakini kuna hatari kuwa hizi dhana zinabaki kuwa dhana tu miongoni mwa wa-Tanzania wengi. Ukweli ni kuwa, ingawa una dosari za hapa na pale, na athari mbaya za hapa na pale, huu mtandao umekuja kama baraka. Mtandao umepunguza au kuondoa tofauti zilizokuwepo kabla katika uwezo wa watu mbali mbali kusambaza taarifa na maoni, au kutangaza shughuli zao kama vile biashara.

Kwa mfano, kwa kutumia nyenzo kama blogu, tovuti, au Facebook, mfanyabiashara mdogo, auzaye mahindi mjini Songea au Tunduma, au yule auzaye vinyago Mtwara, anaweza kutangaza biashara yake kwa ulimwengu.

Mtandao umeleta urahisi wa aia nyingine pia. Leo hii, umuhimu wa kujenga jengo linaloitwa duka, au kukodi chumba cha kukitumia kama duka, umepungua sana. Mtu unaweza ukawa na bidhaa zako nyumbani mwako au katika ghala yako, na ukafungua duka mtandaoni.

Mimi, kwa mfano, ni mwandishi wa vitabu. Ninauza hivi vitabu. Lakini sina nyumba au chumba kinachoitwa duka. Vitabu ninavichapisha mtandaoni. Bofya hapa. Au, kwa usahihi zaidi, niseme kuwa miswada ya vitabu hii nimeihifadhi mtandaoni, na mtu anapoagiza nakala, ndipo mitambo inachapisha nakala iliyoagizwa au nakala zilizoagizwa tu. Sivioni hivi vitabu wanavyoagiza wateja, lakini nimefungua duka huko huko mtandanoni. Bofya hapa. Wateja wananunua bila mimi kuwaona au kuwafahamu.

Katika maduka ya jadi, mwuzaji na mteja wanakutana, au wanasiliana kwa simu au barua. Mteja wa duka la mtandaoni kama hili langu, hahitaji kuwasiliana na mwenye duka. Yeye anafungua kompyuta, anaingia hapo dukani na kununua anachotaka, kwa kutumia "credit card" na kwenda zake. Wewe mwenye duka unapofungua kompyuta na kuangalia duka lako la mtandaoni, utaona kuwa bidhaa imenunuliwa, bila kumjua aliyenunua. Lakini malipo yako yanakuwa yameshaingia.

Siku hizi, watu wengi wenye maduka ya jadi au biashara za jadi wanaziweka mtandaoni pia. Ni njia ya kuwafikia wateja duniani kote. Mtu akiangalia duka hili la mtandaoni akapenda kununua kitu, anawasiliana na mwenye duka, kwa njia itakayokuwa imetajwa, iwe ni barua pepe, simu, au faksi. Au, kufuatana na utaratibu alioweka mwenye duka, mteja anatoa malipo hapo hapo anapoamua kununua kitu fulani. Jukumu la mwenye duka ni kumfungashia na kumpelekea mteja hicho alicholipia.

Kwa maana hiyo, biashara ya aina hii inahitaji uaminifu. Hili si jambo la kuongelewa. Ni ukweli usiopingika. Mwenye biashara makini anazingatia umuhimu wa kumridhisha mteja daima, kwani hii ndio siri ya mafanikio katika biashara. Mteja aliyeridhika na kufurahia huduma mahali fulani anawaambia wenzake. Huduma bora huzaa wapiga debe na kumneemesha mwenye biashara. Lakini mteja asiyeridhika naye atawaeleza wengine, na kusambaa kwa habari hii ni sumu kwa biashara. Wafanya biashara wetu wengi hawaelewi madhara ya kumnyanyasa mteja. Biashara yao inapoanguka, wanatoa visingizio kama vile kurogwa na washindani wao.

Ni muhimu sana wafanyabiashara wetu Tanzania waangalie suala hili la kuingia mtandaoni. Baadhi, kama vile kwenye sekta ya utalii, wanazo tovuti. Lakini kwa jinsi tekinolojia ya mtandao inavyozidi kupanuka na kusonga mbele, na kwa jinsi ilivyo na manufaa, ni vizuri wengine wajiunge na kuwa nayo sambamba.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...