Showing posts with label mafanikio ya biasArusha. Show all posts
Showing posts with label mafanikio ya biasArusha. Show all posts

Friday, March 11, 2011

Mteja Nimefurahi

Juzi niliandika makala fupi, "Mteja ni Mfalme". Leo napenda kuendelea na mada hiyo, kutokana na jambo lililonitokea.

Nilipeleka kigari changu kwenye kampuni ya CarTime, kubadilisha "oil." Kama kawaida, wakati fundi anaendelea na shughuli, nilikuwa kwenye sehemu ya mapumziko ambako wateja hungojea magari yao. Baada ya muda, niliitwa na kuambiwa kuwa gari yangu tayari, nikalipia na kuchukua ufunguo. Kama kawaida, mhudumu wa hapo mapokezi alinishukuru.

Nilienda nje fundi alikopaki gari nikafungua mlango. Kwenye kiti cha mbele alikuwa ameweka karatasi ambayo picha yake nimeiweka hapa juu. Fundi makenika alikuwa ameiweka hapo. Ujumbe wake ni huu: Asante kwa kuchagua CarTime. Tumefurahi kuhudumia gari lako. Kama vile hii haitoshi, fundi ameshukuru tena na kuandika jina lake, Eric.

Katika makala yangu ya juzi niliongelea umuhimu wa kumridhisha mteja. Sasa leo hapa nimeweka mfano hai. Mimi kama mteja nimefurahi kwa huduma niliyopata. Lakini kwa hapa Marekani, hili si jambo la ajabu, kwani wenye biashara wanazingatia suala la huduma kwa mteja. Niliwahi kusema hivyo hata kwenye mahojiano niliyofanyiwa na Radio Mbao.

Kwa vile wanablogu tunafahamu kuwa blogu ni kama shule, na kwa kuzingatia kuwa watu wengi nchini wanasoma hizi blogu, nimeona niweke taarifa hii na mawazo mawili matatu yanayotakiwa kuzingatiwa na wafanyabiashara na watoa huduma wa Tanzania, ambao mara nyingi tunawalalamikia.

Niliwahi kuhudhuria semina ya biashara hapa Minnesota ambapo baadhi ya mambo yaliyosisitizwa ni kuwa unapokuwa na mteja, uwe makini sana. Ujue kuwa mteja huyu akiridhika na kufurahi, atakwenda kukutangazia biashara au huduma yako kwa marafiki na watu wengine.

Sisi wenyewe tunafanya hivyo kila siku. Tukiwa tumevaa nguo nzuri, halafu marafiki wakatuuliza tumenunua wapi, tunawatajia duka. Au watu wakituuliza hoteli nzuri iko wapi, tunawatajia. Waulize watu Dar es Salaam kitimoto safi kinapatikana wapi, watakutajia. Tukiona filamu nzuri, tunawaambia watu wengine na kuwahamasisha nao wakaione. Kwa maana hiyo, tunawapelekea wafanyabishara wateja bila wao kuingia gharama ya matangazo.

Katika semina hiyo hiyo tulionywa kwamba mteja akiudhika, atakwenda kutangaza habari mbaya kuhusu yaliyompata. Habari hiyo itaenea. Wale watakaosikia watawaambia wenzao, na inakuwa kama sumu ambayo itahujumu biashara au huduma yako.

Mimi mwenyewe mwaka jana nilikumbana na wahudumu wa ovyo katika hoteli moja mjini Arusha. Ni hoteli nzuri, na niliiipenda. Nililipia nikapelekwa chumbani. Baada ya muda kidogo nilihitaji msaada wa kurekebishiwa taa. Hapo ndipo nilipokumbana na uzembe usio kifani. Wahudumu walichelewa sana, na huenda hata walisahau. Nikawakumbusha. Bado hawakuja, nimi nikaendelea kuwangoja. Hatimaye nilienda chini walikokuweko nikaanza kuwafokea. Bosi wao naye akaja, nami nikamjumlisha katika mhadhara wangu wa jazba, nikaendelea kutema cheche na kuwapa vidonge wote. Hawakuwa na sababu kabisa ya kushindwa kutekeleza nilichokuwa nimewaambia.

Basi, kutokana na usumbufu walionipa, hata wakati huu ninapoandika sipendi hata kuiwazia hoteli ile. Inakuwa kama vile natonoshwa kidonda. Sina hamu ya kufikia tena katika hoteli ile. Bahati yao ni kuwa hapa sitataja jina lao. Wangenikoma.

Haya ndio mambo ambayo wenye biashara wanapaswa kuyaelewa na kuyazingatia. Inashangaza kwamba wengi nchini mwetu wanaamini kuwa jambo la kufanya ni kwenda kwa waganga wakapate dawa ya kuwavutia wateja. Inakuwaje sisi tuzingatie imani hizo wakati wenzetu kama hao CarTime hawatumii dawa?

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...