Showing posts with label ELCA. Show all posts
Showing posts with label ELCA. Show all posts

Thursday, March 29, 2018

Kitabu Kinaendelea Kupigiwa Debe Nebraska

Mfanya biashara au mtoa huduma hufarijika anapoona wateja wakija tena kufuata kile walichokipata kabla. Imekuwa hivyo kwangu kama mwandishi. Mimi si mfanyabiashara, bali ni mwalimu. Uandishi ni sehemu ya ualimu. Ninafarijika na kufurahi ninapoona watu wakifaidika na maandishi yangu.

Ninaandika ujumbe huu kuelezea ujumbe juu ya kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kutoka Nebraska, jimbo mojawapo la Marekani. Waumini wa kanisa la ki-Luteri la Marekani, ELCA, wa sinodi ya Nebraska wana programu ya kuzuru Tanzania iitwayo vision trip, kujifunza masuala ya utamaduni na maisha ya wa-Tanzania na kubadilishana uzoefu, ili kujenga mahusiano na maelewano.

Mwaka hadi mwaka, waratibu wa programu wamekipendekeza kitabu changu hicho. Leo nimeona chapisho la mwongozo kwa ajili safari ya mwaka 2018. Humo, kama ilivyokuwa miaka iliyopita, kitabu changu kimeendelea kupendekezwa kwa wasafiri:

For those persons wanting to more deeply explore cultural differences between Africans and Americans, the book Africans and Americans by Joseph Mbele is recommended. This book is available at: www.africonexion.com

Tafsiri kwa ki-Swahili:

Kwa wale wanaotaka kufuatilia zaidi tofauti za tamaduni baina ya wa-Afrika na wa-Marekani, kitabu "Africans and Americans" cha Joseph Mbele kinapendekezwa. Kitabu hiki kinapatikana www.africonexion.com


Ninafurahi na kushukuru kwamba watu wanaona umuhimu wa kitabu hiki. Kingekuwa hakina manufaa, wangeacha kukipendekeza tangu zamani. Niliwahi kukutana na baadhi ya hao wasafiri wa Nebraska katika safari ya kwenda Tanzania wakiwa na kitabu changu, kama nilivyoandika katika blogu ya ki-Ingereza. Ninafurahi kuwa kitabu changu kinasaidia lengo la kujenga maelewano baina ya wa-Tanzania na wa-Marekani.

Thursday, September 8, 2016

Wasomaji Wangu Wa Nebraska Waendao Tanzania

Nina jadi ya kuwaongelea wasomaji wangu katika blogu hii, kama njia ya kuwaenzi. Ni jambo jema kwa mwandishi kufanya hivyo. Leo ninapenda kuwakumbuka wasomaji wangu wa sinodi ya Nebraska ya Kanisa la Kiluteri la Marekani, ambao tangu zamani wamekuwa na programu ya kupeleka watu Tanzania kuendeleza uhusiano baina yao na wa-Luteri wa Tanzania.

Hao wasafiri, sawa na wenzao wa sinodi zingine za Marekani, wamekuwa wakitumia kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika kujiandaa kwa safari, ili kuzielewa tofauti za tamaduni za Marekani na Afrika. Ni elimu muhimu katika ulimwengu wa utandawazi wa leo, ambayo nje ya ufundishaji wa darasani, ninashughulika nayo.


Wakati huu ninapoandika, waumini wa Nebraska wanajiandaa kwa safari ya Tanzania, ambayo itafanyika mwezi Februari mwaka 2017. Wameitangaza safari hii mtandaoni, na mratibu mojawapo wa safari, Martin Malley, ameniandikia ujumbe leo akisema, "We still recommend your book." Katika ukurasa wa 16 wa chapisho la maelezo na maandalizi ya safari, kitabu hicho kimetajwa.

Ninapowakumbuka wasomaji wangu wa Nebraska, ninakumbuka nilivyokutana katika uwanja wa ndege wa Amsterdam na kikundi cha watu wa Nebraska waliokuwa wanakwenda Tanzania, tukasafiri pamoja. Mimi sikuwajua, ila wao walinitambua, kama nilivyoelezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza.


Monday, November 19, 2012

Kwa wa-Luteri wa Tungamalenga, Iringa

Makanisa mengi ya ki-Luteri Marekani, ELCA, yana ushirikiano na makanisa ya ki-Luteri ya Tanzania na nchi zingine. Kanisa la Shepherd of the Valley, ambalo liko hapa Minnesota, lina uhusiano na kanisa la Tungamalenga, mkoani Iringa. Kwa taarifa zaidi, soma hapa.

Nimewahi kutembelea Shepherd of the Valley kuongea na wanafunzi wa Chuo cha Gustavus Adolphus ambao walikuwa hapo kufanya maandalizi ya safari ya Tanzania, kama nilivyoelezea hapa.

Kwa miaka mingi kiasi nilifahamu kuhusu uhusiano baina ya Shepherd of the Valley na Tungamalenga.  Kila ninapoliwazia kanisa la Shepherd of the Valley, au ninapoliona, naiwazia Tungamalenga, ingawa mimi si m-Luteri. Kwa vile liko pembeni mwa barabara, ninaliona kanisa hilo kila ninapoenda kutoa mihadhara katika Chuo cha Mazingira.

Sikuwahi kufika Tungamalenga, hadi mwaka jana, niliposafiri na wanafunzi wa ki-Marekani kutoka Iringa kwenda hifadhi ya Ruaha. Ghafla tulipita sehemu iitwayo Tungamalenga. Nilishtuka, kwa sababu sikuwa hata najua kama Tungamalenga iko katika njia hiyo, karibu kabisa na hifadhi ya Ruaha.

Picha inayoonekana hapa juu nilipiga tarehe 13 Novemba, nilipokuwa narudi kutoka kwenye Chuo cha Mazingira. Kwa miaka miwili au zaidi nilitaka niweke picha ya Shepherd of the Valley hapa katika blogu yangu, nikiwawazia wa-Luteri wa Tungamalenga.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...