Showing posts with label wa-Marekani. Show all posts
Showing posts with label wa-Marekani. Show all posts

Thursday, March 29, 2018

Kitabu Kinaendelea Kupigiwa Debe Nebraska

Mfanya biashara au mtoa huduma hufarijika anapoona wateja wakija tena kufuata kile walichokipata kabla. Imekuwa hivyo kwangu kama mwandishi. Mimi si mfanyabiashara, bali ni mwalimu. Uandishi ni sehemu ya ualimu. Ninafarijika na kufurahi ninapoona watu wakifaidika na maandishi yangu.

Ninaandika ujumbe huu kuelezea ujumbe juu ya kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kutoka Nebraska, jimbo mojawapo la Marekani. Waumini wa kanisa la ki-Luteri la Marekani, ELCA, wa sinodi ya Nebraska wana programu ya kuzuru Tanzania iitwayo vision trip, kujifunza masuala ya utamaduni na maisha ya wa-Tanzania na kubadilishana uzoefu, ili kujenga mahusiano na maelewano.

Mwaka hadi mwaka, waratibu wa programu wamekipendekeza kitabu changu hicho. Leo nimeona chapisho la mwongozo kwa ajili safari ya mwaka 2018. Humo, kama ilivyokuwa miaka iliyopita, kitabu changu kimeendelea kupendekezwa kwa wasafiri:

For those persons wanting to more deeply explore cultural differences between Africans and Americans, the book Africans and Americans by Joseph Mbele is recommended. This book is available at: www.africonexion.com

Tafsiri kwa ki-Swahili:

Kwa wale wanaotaka kufuatilia zaidi tofauti za tamaduni baina ya wa-Afrika na wa-Marekani, kitabu "Africans and Americans" cha Joseph Mbele kinapendekezwa. Kitabu hiki kinapatikana www.africonexion.com


Ninafurahi na kushukuru kwamba watu wanaona umuhimu wa kitabu hiki. Kingekuwa hakina manufaa, wangeacha kukipendekeza tangu zamani. Niliwahi kukutana na baadhi ya hao wasafiri wa Nebraska katika safari ya kwenda Tanzania wakiwa na kitabu changu, kama nilivyoandika katika blogu ya ki-Ingereza. Ninafurahi kuwa kitabu changu kinasaidia lengo la kujenga maelewano baina ya wa-Tanzania na wa-Marekani.

Sunday, January 8, 2017

Msomaji Wangu Mpya

Jirani yangu mama Merri, mdau na mpiga debe mkubwa wa maandishi na shughuli zangu za uelimishaji, amenitambulisha kwa mwalimu Paul White anayeishi California. Alianza kuniambia habari za mwalimu huyu miezi kadhaa iliyopita, wakati aliponiambia kuwa anataka kumpelekea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Alinunua, nikasaini, akampelekea.

Baada ya hapo, nami nilianza kutafuta taarifa za mwalimu huyu mtandaoni. Niliguswa sana na juhudi na mafanikio yake katika kuwafundisha na kuwapa mwelekeo vijana walioshindikana, waliokata tamaa, wahalifu, na ambao jamii iliwaona hawafundishiki wala hawawezi kuokolewa.

Katika maisha yangu yote, sijawahi kusoma kuhusu mwalimu mwenye mtazamo na moyo kama alio nao mwalimu White. Mfano moja wa taarifa zake zilizonigusa ni mahojiano haya hapa. Nilivyosoma taarifa zake, nilifikiwa na wazo la kuanzisha mpango kama wa kwake nchini mwangu, kuwaokoa vijana waliotemwa na mfumo wa elimu, waliokata tamaa, wahalifu, ambao jamii inaamini wameshindikana.

Hatimaye, kwa kuhimizwa na mama Merri, jana nilimpigia simu mwalimu White. Mke wake aliitika akaniambia kuwa mwalimu alikuwa ameondoka kodogo,  nikaacha namba ya simu. Baada ya nusu saa hivi, mwalimu alinipigia simu, tukaongea kwa msisimko wa furaha. Aliniambia kuwa anakifurahia kitabu changu, akanukuu sehemu mbili tatu kusisitiza tofauti baina ya wa-Afrika na Wamarekani.

Ameongea kirefu, akanihimiza niandae mhadhara wa TED, na pia nifikirie kwenda California kutoa mihadhara kuhusu masuala yanayoikabili jamii ya wa-Marekani, kama vile tofauti za tamaduni. Tumefurahi kuwasiliana na tunafurahi zaidi kuwa tutaendelea na mawasiliano. Nimeona nijiwekee hizi kumbukumbu zangu, kwani ni lengo langu moja muhimu katika kublogu. 

Tuesday, February 3, 2015

Wa-Marekani na wa-Tanzania: Tofauti za Tamaduni

Leo, katika ukurasa wake wa "Facebook," Ndugu Maggid Mjengwa aliandika: "Leo Nimepokea Wafanyakazi Wa Kujitolea Kutoka Marekani..."

Wa-Marekani hao, ambao anaonekana nao katika picha hapa kushoto, wamefika Iringa kujitolea katika Kwanza Jamii, kampuni inayoendesha gazeti na redio. Maggid hakutuambia watakaa muda gani hapo Iringa, lakini nilijibu ujumbe wake "Facebook" namna hii:

"Safi sana. Ninapoona au kusikia mambo ya aina hii, wazo linalonijia akilini ni kuwa muhimu wageni wapate mtu wa kuwaelezea angalau yale ya msingi kuhusu tofauti kati ya utamaduni wa-Marekani na ule wa wa-Bongo, na wa-Bongo pia waelezwe kuhusu tofauti kati ya utamaduni wao na ule wa wa-Marekani. Hii ni kwa ajili ya kurahisisha shughuli na maisha kwa pande zote mbili. Kila la heri."

Suala hili nililoongelea ni muhimu hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Hao wageni wanapokuja kwetu na sisi tunapoenda kwenye nchi zao, ni mihumu kulizingatia, ili kufanikisha shughuli na mahusiano baina yetu. Nimeandika kuhusu tofauti baina ya utamaduni wa wa-Marekani na wa-Afrika katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho nashukuru kwa jinsi kinavyowasaidia watu wanaokisoma, kama ilivyoelezwa hapa na hapa.

Hilo ni suala ninalolishughulikia sana katika utafiti, mihadhara na warsha. Hiyo picha hapa juu tayari inanipa vidokezo muhimu. Ninaona jinsi hao wasichana walivyomwangalia Maggid usoni, na yeye ameangalia chini. Hapo Mjengwa anaonyesha heshima kwao, kwa mujibu wa utamaduni wetu wa ki-Tanzania na ki-Afrika kwa ujumla.

Nao hao wasichana, kwa mujibu wa utamaduni wa Marekani, wanaonysha heshima kwa kumwangalia Maggid usoni. Huenda wanashangaa kwa nini hawaangalii usoni. Hilo suala la kuangaliana usoni ni moja ya yale ninayoyaongelea katika kitabu changu:

Kama hii picha ingekuwa ni video, ingenipa fursa ya kusema mengi zaidi.

Tuesday, November 16, 2010

Mzee Kataraia Amekipenda Kitabu Hiki

Blogu yangu hii ni kama kisebule changu binafsi. Naamua nini cha kukiweka hapa, na sidhani kama ninasukumwa na ukweli kwamba watu wanasoma ninayoandika. Yeyote anayepita hapa na kuchungulia, ni hiari yake. Niliwahi kujieleza hivyo katika makala hii hapa.

Basi, leo napenda kuelezea nilivyokutana na Mzee Kataraia juzi, tarehe 14, mjini Minneapolis. Hatukuwa tumefahamiana. Lakini mara tulipotambulishwa, alianza kunielezea jinsi alivyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans.

Niliguswa, nikamsikiliza kwa unyenyekevu. Ingawa napenda kuandika makala na vitabu, na watu wengi wananielezea wanavyopendezwa na kufaidika na maandishi yangu, napata taabu kustahimili sifa. Ila huwa namshukuru Mungu kwa kunipa vipaji, niendelee kutekeleza wajibu wa kuwanufaisha viumbe wake. Hii ndio tafsiri yangu. Sifa zote na shukrani namrudishia Muumba.

Nikiwa namsikiliza, Mzee Kataraia aliendelea kunieleza jinsi alivyosafiri sehemu zingine hapa Marekani, akawaonyesha wa-Tanzania kadhaa kitabu hiki, nao wakakisoma. Aliniambia kuwa wiki hizi alizokuwa hapa Marekani, ameshafanya safari kadhaa kwa ndege. Wakati wa kungojea ndege, ameona watu wakisoma kwenye kompyuta zao, na ndege ikiwa hewani amewaona watu wakisoma vitabu. Hapo nami nikamwunga mkono, kuwa nami nimeona sana tabia hizo hapa Marekani.

Maongezi yetu yalikuwa mafupi sana, labda dakika tano tu, kwa sababu tulikuwa katika shughuli nyingine za kusalimiana na kuongea na watu. Lakini kwa dakika zile chache nilipata picha kuwa Mzee Kataraia ni m-Tanzania wa pekee.

Kwanza, kama ninavyoandika katika blogu hii mara kwa mara, si rahisi kumkuta m-Tanzania anayevutiwa na vitabu, labda vitabu vya udaku. Halafu niliguswa na moyo wa Mzee Kataraia wa kuwakumbuka wengine. Alivyoona amekuta kitu cha manufaa, ameenda kuwaonyesha wengine, wanufaike. Nimeguswa.

Sitamsahau Mzee huyu. Nitajiona nina bahati iwapo nitakutana naye tena. Nimegundua huyu ni Mzee aliyeelimika. Kwa mtazamo wangu, kama nilivyosema katika mahojiano Radio Mbao, ishara muhimu ya kuelimika ni kuwa daima na kiu ya kutafuta elimu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...