Saturday, April 4, 2015

Nimerejea Salama Kutoka Leech Lake Tribal College

Nilirejea jana jioni kutoka Leech Lake Tribal College, kwenye mkutano kuhusu "Narratives of Identity." Nilikuwa mmoja wa wanajopo wanne waliotoa mada, na mada yangu ilikuwa "Being African in America."

Niliongelea uzoefu wangu katika miaka mingi ya kuishi na kufundisha hapa Marekani, nikielezea kazi kubwa isiyoisha ya kujitambulisha kama mu-Afrika, ambaye ni tofauti na mu-Amerika Mweusi. Nilielezea jinsi suala hilo linavyosabisha mikanganyiko na kutoelewana baina ya wa-Marekani Weusi na wa-Afrika tuishio Marekani.

Nilisema wazi kuwa namna wanavyojiita na kujitambulisha wa-Marekani Weusi ni tofauti na namna tunavyojiita na kujitambulisha sisi wa-Afrika. Nilimnukuu Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria ambaye katika mahojiano na katika riwaya yake maarufu ya Americanah, ameelezea vizuri suala hilo.

Nilimnukuu pia mwandishi Jamaica Kincaid wa Antigua, pande za Caribbean, ambaye pamoja na kuwa ni mweusi pia, hakuwahi kujiita kama wanavyojiita  wa-Marekani Weusi. Hayo mawazo yake niliyasoma katika mahojiano yaliyochapishwa mwaka 1991 katika jarida la Mississippi Review.

Nilisisitiza umuhimu wa kuheshimu haki ya kila jamii kujiita au kujitambulisha kwa majina wanayoyataka au yanayowaridhisha wenyewe. Watu wengine sherti wafuate njia hiyo badala ya kuwapachika watu majina ya utambulisho kama walivyofanya wakoloni.

Nilienda mbali zaidi na kuelezea suala la haki ya kila jamii kujieleza wenyewe, sio kuzimishwa kama walivyotuzimisha wakoloni, na wao wakawa wanaandika juu yetu.

Siwezi kuelezea hapa yote niliyosema. Nawazia kuendelea kutafakari suala hilo na kujisomea zaidi, na kuwasoma upya watu kama Frantz Fanon, Aime Cesaire, na Ngugi wa Thiong'o, ili hatimaye niandike makala kamili.

Hiyo jana, wakati nilipokuwa najitambulisha mkutanoni, nilisema kuwa nimeleta vitabu vyangu viwili kama zawadi kwa maktaba ya chuo cha Leech Lake Tribal College. Vitabu hivyo ni Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Vitabu hivi vilipokelewa kwa furaha na shukrani tele.

Nina hakika kuwa mkutano ule umesisimua watu. Jana hiyo hiyo, katika ukurasa wa Facebook wa Leech Lake Tribal College iliandikwa taarifa hii:

We had some great speakers on campus today for the Narratives of Identity presentations. One of the many memorable remarks from today's visit was by Joseph Mbele, St Olaf College- “I am not a person of color. I am Tanzanian which is a concept of colonization. Only when I came to America was I referred to as black. Naming yourself, knowing yourself, is a right…Construction of identities are not fixed and it’s our right to identify ourselves.”

(Picha ya juu kabisa na ya katikati ni kutoka Leech Lake Tribal College)

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...