Thursday, April 2, 2015

Mijadala Kuhusu Vitabu Katika Maktaba ya Bemidji, Minnesota

Ni usiku saa saba kasoro, nami nimo chumbani mwangu katika Hampton Inn hapa mjini Bemidji. Ninasoma gazeti la hapa liitwalo "The Bemidji Pioneer" la jana, yaani tarehe 2.

Nimevutiwa sana na habari kuhusu utaratibu walio nao katika mji huu wa kukusanyika katika maktaba yao na kufanya mijadala kuhusu vitabu. Nanukuu habari nzima, ambayo iko ukurasa wa 2:

Public Library book discussion set

BEMIDJI--The Bemidji Public Library offers a monthly book discussion program--the next session will take place at noon April  13. The program will run for approximately an hour.

The book for discussion will be "The Devil in the White City: Murder, Magic and Madness at the Fair that Changed America" by Eric Larson.

Nimejikuta nawazia mengi. Je, utaratibu wa aina unawezekana katika miji ya Tanzania? Kuna maktaba katika miji kama Dar es Salaam, Arusha, Tanga, Mwanza, Iringa, Songea, Lushoto, Mbinga, Karatu, na Mbulu. Hizo nimeziona mwenyewe, sio za kusikia.

Je utaratibu wa kuchagua na kujadili kitabu fulani kila mwezi unawezekana? Tusianze kutoa visingizio. Makampuni ya vitabu kama Mkuki na Nyota, Tanzania Publishing House, Dar es Salaam University Press, Ndanda Mission Press, na E&D Publishers yamechapisha na yanaendelea kuchapisha vitabu vingi sana.

Kampuni ya Mkuki na Nyota, kwa mfano imekuwa ikichapisha  vitabu vya Shaaban Robert kwa wingi, na kwa jamii yetu inayodai kuwa inakienzi ki-Swahili, mtu ungetegemea kuwa vitabu hivyo vinawindwa kama tunavyowinda kitimoto au bia za baridi.

Kuhusu gharama, wa-Tanzania kwa ujumla hawawezi kushindwa kuvinunua. Angalia jinsi wanavyochangia sherehe, jinsi wanavyofurika kwenye mechi za kabumbu, jinsi wanavyofurika kwenye burudani mbali mbali. Hela sio tatizo; ziko tele.

Nini kinazuia kuwepo katika jamii yetu kwa utamaduni kama huu wa jamii ya Bemidji wa kujadili vitabu?


No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...