Showing posts with label Masimulizi. Show all posts
Showing posts with label Masimulizi. Show all posts

Saturday, July 1, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Ninaamini kuwa kila mtu ana kitu anachokipenda sana. Kuna watu wanaopenda sana soka. Ni mashabiki ambao daima wanafuatilia mechi. Wako tayari kukopa hela ili waende uwanjani kuangalia mechi. Wengine wanapenda bia. Katika baa za Tanzania, nimeona watu wanaokunywa na kuandikiwa deni walipe baadaye. Kama huku kupenda kitu namna hii ni ugonjwa, basi vitabu ndio ugonjwa wangu. Ndio maana katika blogu hii ninaandika mara kwa mara habari za vitabu.

Mtu anaweza kuuliza, inakuwaje katika ulimwengu huu wa vitabu pepe, tuko watu ambao tunaendelea kung'ang'ania vitabu vya jadi? Je, hatuoni udhia wa kubeba vitabu hivyo, na pia udhia wa kuvitafutia sehemu ya kuviweka, badala ya kutumia kifaa cha kuhifadhia vitabu pepe, ambacho kinaweza kubeba mamia ya vitabu au zaidi? Ukweli ni kwamba, mazoea yana taabu. Sio rahisi kuachana na mazoea.

Leo nilikwenda Minneapolis, na wakati wa kurudi, nilipita katika duka la vitabu la Half Price Books, mjini Apple Valley. Kama kawaida, niliangalia kwanza sehemu vinapowekwa vitabu vya Ernest Hemingway au vitabu juu ya Hemingway. Sikuona kipya, nikaelekea sehemu vinapouzwa vitabu vya bei rahisi kabisa. Hapo nilichagua vitabu vinne.

Kitabu kimoja ni Gilgamesh: A Verse Narrative, cha Herbert Mason. Wafuatiliaji wa fasihi simulizi za kale wanafahamu juu ya Gilgamesh, mtu maarufu katika masimulizi ya watu wa himaya ya Sumer, katika nchi ambayo leo inaitwa Iraq, na pia nchi zingine za Mashariki ya Kati. Masimulizi haya hatimaye yaliandikwa, katika lugha kadhaa za wakati ule, kwa hati iitwayo "cuneiform," ambayo ni tofauti kabisa na hizi hati tunazotumia leo, kama vile ya ki-Rumi, au ki-Arabu. Ugunduzi wa maandishi yale ulitokana na juhudi za wana akiolojia.

Lakini baada ya ugunduzi, hakuna aliyeweza kusoma hati ya "cuneiform." Baadaye sana siri ya hati hii iligunduliwa na usomaji wake ukawezekana. Tafsiri za masimulizi ya Gilgamesh zikaanza. Kwa upande wangu, kwa miaka mingi nimefundisha masimulizi ya Gilgamesh kwa kutumia tafsiri ya N. K. Sandars. Nilifahamu, hata hivyo, kwamba ziko tafsiri zingine pia. Kwa hivyo, leo niliona ninunue hii tafsiri ya kishairi ya Herbert Mason.

Kitabu kingine nilichonunua leo ni A Play of Giants, ambayo ni tamthilia ya Wole Soyinka. Nimesoma na kufundisha maandishi ya Soyinka kwa miaka mingi, kuanzia tamthilia, riwaya, mashairi na insha. Ninavyo vitabu vyake kadhaa, lakini si A Play of Giants. Hata hivyo, nilifahamu tangu zamani kuwa tamthilia hii inawaumbua madikteta wa Afrika. Sasa nitaisoma.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni Theban Plays of Sophocles. Ni tafsiri ya David R. Slavitt ya tamthilia tatu za Sophocles. Huyu ni mwanatamthilia maarufu wa u-Griki ya kale. Ninazo tatsiri tofauti za tamthilia hizo, lakini niliamua kununua hii pia. Ni jambo bora kusoma tafsiri mbali mbali za kazi ya fasihi, kwani kila tafsiri inaleta ladha tofauti na hata tofauti za ujumbe.

Kitabu cha nne nilichonunua ni Speaking of Books: The Best Things Ever Said About Books and Book Collecting, kilichohaririwa na Rob Kaplan na Harold Rabinowitz. Hicho sikuwahi hata kukisikia, lakini nilivyoangalia ndani, nilivutiwa. Ni mkusanyiko wa kauli za watu mbali mbali kuhusu vitabu, usomaji, uandishi, waandishi, wasomaji, na kadhalika. Nilikuwa ninafahamu baadhi ya mambo ambayo yamewahi kusemwa kuhusu vitabu, kama vile kauli ya Ernest Hemingway, "There is no friend as loyal as a book," yaani hakuna rafiki wa kweli kama kitabu. Kutokana na kupendezwa kwangu na mambo hayo, niliona ninunue kitabu hiki.

Sunday, April 2, 2017

Mhadhara Chuo Kikuu cha Minnesota Juu ya Kitereza

Juzi tarehe 31, Dr. Charlotte (Shoonie) Hartwig na mimi tulitoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Minnesota, juu ya mwandishi Aniceti Kitereza. Huyu ni mwandishi muhimu ambaye, hata hivyo, hafahamiki sana. Mama Shoonie amekuwa akiandika kitabu ambacho nami nimechangia, na mhadhara wetu ulihusu kitabu hiki ambacho tunategemea kukichapisha.

Kitereza alizaliwa mwaka 1896 katika kisiwa cha Ukerewe kilichomo katika Ziwa Victoria, upande wa Tanzania. Alisomea katika shule za wamisheni, na alipomaliza aliajiriwa kazi kadhaa. Alivyozidi kukua alipata dhamira ya kuhifadhi mila na desturi za zamani za wa-Kerewe, ili zisipotee. Kama sehemu ya juhudi hiyo aliandika riwaya katika lugha ya ki-Kerewe, ambao aliukamilisha mwanzoni mwa mwaka 1945. Andiko hili ni hazina ya mila na destruĂ­ za wa-Kerewe wa zamani, ila Kitereza aliandika kwa mtindo wa hadithi ya kubuni, ili wasomaji wasichoke kusoma.

Baada ya juhudi na mahangaiko ya miaka mingi ya kutafuta mchapishaji, na kufuatia ushauri wa marafiki zake wa-Marekani, Kitereza aliutafsiri mswada wake kwa ki-Swahili. Hata hivyo, aliendelea kungoja kwa miaka mingi hadi mwaka 1980 ambapo mswada ulichapishwa kama kitabu, Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka na Ntulanalwo na Buliwhali.

Mama Shoonie ni mtu pekee aliyesalia mwenye taarifa za ndani za Kitereza, kwani yeye na mumewe, Dr. Gerald Hartwig, walimfahamu vizuri Kitereza baada ya kuonana naye kwa mara ya kwanza mwaka 1968 Ukerewe. Mbali ya kukutana naye mara kwa mara miaka ile ya mwanzo, waliendelea kuandikiana barua hadi miaka ya mwisho wa maisha yake. Kitereza alikuwa hodari wa kuandika barua; ananikumbusha waandishi kama Ernest Hemingway na Shaaban Robert.

Katika mhadhara wa juzi, Mama Shoonie alielezea maisha ya Kitereza na mambo aliyofanya kama mwandishi. Maelezo yake aliyaambatanisha na picha za Kitereza, mke wake, na familia nzima ya Hartwig. Watoto wa familia ya Hartwig walikuwa wadogo sana wakati huo. Mama Shoonie alielezea kuwa Kitereza alikuwa anajituma sana katika shughuli yake ya kuhifadhi mila na destruĂ­ za wahenga kwa kusukumwa na suali ambalo alilitunga mwenyewe, "Tunawajibika kuwafundisha nini watoto wetu?"

Ilipokuja zamu yangu, nilielezea kwa ufupi uandishi wa Kitereza kwa mujibu wa mtazamo wangu kama mwana fasihi. Nilisisitiza masuala kadhaa muhimu yanayojitokeza katika taaluma ya fasihi ya Afrika, hasa suala la uandishi katika lugha za ki-Afrika na suala la tafsiri. Niligusia jinsi riwaya ya Bwana Myombekere inavyoweza kutupa mtazamo mpya kuhusu historia ya riwaya ya ki-Afrika, na jinsi inavyoweza kuchambuliwa sambamba na kazi za waandishi kama Daniel O. Fagunwa na Amos Tutuola wa Nigeria, Gakaara wa Wanjau wa Kenya, na Shaaban Robert wa Tanzania. Huu utakuwa ni mtazamo wa fasihi linganishi.

Nimesoma tafsiri ya Kitereza ya riwaya yake. Ki-Swahili chake, ingawa kinatofautiana na ki-Swahili sanifu, kina ladha na mtiririko wa hadithi simulizi za lugha za ki-Bantu kama vile lugha yangu ya ki-Matengo. Kwa msingi huo, ninaipenda tafsiri ya Kitereza. Riwaya yake imetafsiriwa kwa ki-Faransa na ki-Jermani, lakini tafsiri hizo, kwa mujibu wa Profesa Gabriel Ruhumbika, zina walakini. Kauli ya Profesa Ruhumbika ina uzito sana, kwani lugha mama yake ni ki-Kerewe na pia yeye ni mashuhuri katika uwanja wa kutafsiri.

Profesa Ruhumbika mwenyewe ametafsiri kwa ki-Ingereza riwaya ya Kitereza kama ilivyoandikwa ki-Kikerewe, na tafsiri yake imechapishwa kama Mr. Myombekere and His Wife Bugonoka, Their Son Ntulanalwo and Daughter Buliwhali. Katika kuisoma tafsiri hii, nilivutiwa nayo, sawa na nilivyovutiwa na tafsiri ya ki-Swahili ya Kitereza mwenyewe. Ni tafsiri ambayo ninapendekeza isomwe na yeyote. Hivyo hivyo, ninakipendekeza kitabu cha Mama Shoonie kijacho. Ni kitabu chenye taarifa nyingi, zikiwemo barua na picha, ambazo ulimwengu haujaziona. 

Friday, December 9, 2016

The Rime of the Ancient Mariner: Samuel Taylor Coleridge

Jana na leo nimesoma The Rime of the Ancient Mariner, utenzi maarufu wa Samuel Taylor Coleridge, ambao ni moja ya tungo za ki-Ingereza nilizokuwa ninazipenda wakati wa ujana wangu, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nimefurahi kuusoma tena, baada ya miaka mingi, wakati ambapo akili yangu imepevuka zaidi kutokana na kusoma tungo nyingi za fasihi.

Katika kusema hivi, ninakumbuka kauli ya mshairi William Wordsworth, katika shairi lake maarufu, "Lines Written a Few Miles Above Tintern Abbey," anavyoongelea namna alivyotembelea, katika utu uzima wake, eneo ambalo alilizoea alipokuwa kijana. Matokeo ya kufanya hivyo ni kwamba, ingawa hawezi tena kuyaona mazingira yale kwa hisia za ujanani, sasa anayaona kwa kutumia akili ya kiutu uzima. Aina zote mbili za maono anazienzi, ingawa zinatofautiana.

Nami ninajisikia hivyo hivyo katika kusoma wakati huu The Rime of the Ancient Mariner. Nimeweza kuuweka utungo huu katika mkabala wa tungo nilizosoma kwa miaka ya baina ya ujana wangu na umri nilio nao sasa. Ninawazia hadithi ya kale ya Misri iitwayo, "The Tale of the Shipwrecked Sailor," utenzi wa Odyssey wa Homer, hadithi za baharia Sindbad, riwaya ya Daniel Defoe, Robinson Crusoe; riwaya ya Herman Melville, Moby Dick; na Utenzi wa Masaibu.

Papo hapo, kutokana na utafiti na ufundishaji wa somo la "Folklore," nimetilia maanani vipengele vya The Rime of the Ancient Mariner kama usimuliaji wa hadithi, imani mbali mbali ambazo tunaziita ushirikina. Kuna imani kama vile juu ya macho kuwa na nguvu ya kichawi. Dhana hiyo inajitokeza mara kadhaa katika utenzi huu. Kwa mfano, mwanzoni kabisa mwa utenzi tunasoma:

It is an ancient Mariner,
And he stoppeth one of three.
'By thy long grey beard and glittering eye,
Now wherefore stopp'st thou me?

'The Bridegroom's doors are opened wide,
And I am next of kin;
The guests are met, the feast is set:
May'st hear the merry din.'

He holds him with his skinny hand,
'There was a ship,' quoth he.
'Hold off! unhand me, grey-beard loon!'
Eftsoons his hand dropt he.

He holds him with his glittering eye--
The Wedding-Guest stood still,
And listens like a three years' child:
The Mariner hath his will.

Kuanzia hapo, huyu baharia mkongwe anamsimulia kijana yaliyomsibu katika safari baharini, yeye na mabaharia wenzake. Ni kisa cha mikosi, majanga na vifo vya wenzake wote akasalimika yeye, na tangu hapo katika maisha yake, hupatwa na maumivu fulani nafsini mwake ambayo suluhu yake ni kumnasa mtu wa kumsimulia kisa chake.

The Rime of the Ancient Mariner ni kisa cha kusisimua. Coleridge anazisukuma hisia zetu kupitia hali mbali mbali: mshangao, hofu, masikitiko, na huruma. Pamoja na kwamba hatimaye tunafarijika kwa jinsi mzee huyu alivyonusurika, tunabaki na majonzi kwa vifo vya mabaharia wenzake. Baada ya kuelewa kisa kizima, tunaelewa kwa nini mzee huyu anamteka kwa uchawi wa macho yake kijana anayekwenda arusini na kumfanya asikilize kisa chake hadi mwisho.


Sunday, November 8, 2015

Nimealikwa Kusimulia Hadithi

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mama mmoja m-Liberia aishiye hapa Minnesota. Amejitambulisha kwamba tulikutana katika tamasha la Afrifest, akauliza iwapo nitaweza kwenda kusimulia hadithi mjini Maple Grove tarehe 14 mwezi huu, katika sherehe ya kumbukumbu ya kuzaliwa mtoto.

Nilielezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza nilivyosimulia hadithi katika tamasha la Afrifest, hapa na hapa. Nilisimulia hadithi mbili kutoka katika kitabu cha Matengo Folktales. Mama aliyeniletea mwaliko wa tarehe 14 amenikumbusha kwamba mtoto wake na wengine walioshuhudia hadithi zangu katika Afrifest walivutiwa na wanataka nikasimulie tena.

Hii itakuwa mara yangu ya kwanza kusimulia hadithi katika mkusanyiko wa wanafamilia na marafiki zao, katika sherehe ya kifamilia. Nimezoea kusimulia katika vyuo. Nitatumia sehemu ya muda nitakaokuwa nao kuelezea dhima ya hadithi katika jadi za wa-Afrika na wanadamu kwa ujumla, halafu nitasimulia hadithi, na kisha nitawahimiza wasikilizaji kusaidia kuichambua hadithi nitakayosimulia. Ninawazia kusimulia hadithi kutoka Afrika Magharibi, labda Liberia, Senegal, au Burkina Faso, zilizomo katika kitabu cha West African Folktales.

Hadithi za jadi ni hazina yenye mambo mengi, kama vile falsafa, mafundisho kuhusu saikolojia na tabia za wanadamu, kuhusu mema na mabaya. Ziko zinazosikitisha, zinazofurahisha na kuburudisha, na zinazochemsha bongo, kama zile ziitwazo kwa ki-Ingereza "dilemma tales." Zote ni muhimu katika maisha ya wanadamu, kama nilivyojaribu kuelezea katika kitabu cha Matengo Folktales.

Tuesday, May 26, 2015

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Nimepata mwaliko kutoka Chuo Kikuu cha Winona, Minnesota, kwenda kutoa mhadhara tarehe 23 Juni. Huu utakuwa ni mchango wangu katika semina ya mafunzo kwa wanafunzi kutoka sehemu mbali mbali itakayofanyika Juni 17-27. Kama ilivyo kawaida yangu, nimeona niweke kumbukumbu hapa.

Mafunzo haya yatalenga kuwaandaa wanafunzi hao kwa masomo ya juu, waweze kuifahamu hali halisi ya maisha ya chuoni na taratibu za taaluma, waweze kujijengea hali ya kujitambua na uwezo wa uongozi.

Mratibu wa mafunzo, Alexander Hines, ambaye anafahamu kiasi shughuli zangu,  aliniambia tuangalie ni kipi kati ya vitabu vyangu viwili kitafaa zaidi kwa semina hii: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences au Matengo Folktales. Nilishauri kwamba hicho cha pili kingeendana vizuri zaidi na dhamira kuu ya semina.

Tumekubaliana. Tumekubaliana nikaelezee ni nini tunaweza kujifunza kutokana na tamaduni za jadi za Afrika katika masuala haya ya kujitambua, falsafa ya maisha, na uongozi katika dunia ya leo na kesho.

Kama ilivyo kawaida yangu, huwa napokea mialiko ya kutoa mchango wa mawazo kufuatana na mahitaji ya wale wanaonialika. Itabidi nitafakari na kuandaa mawazo yatakayotoa mchango unaohitajika katika semina. Wazo la kutumia kitabu cha Matengo Folktales kama msingi ni wazo muafaka, kwani masimulizi haya ya jadi yanathibitisha jinsi wahenga wetu walivyoyatafakari masuala muhimu ya maisha, mahusiano, na mengine yanatuhusu leo na yataendelea kuwa muhimu daima.
 

Tuesday, December 25, 2012

Milima Haikutani

Wa-Swahili husema, milima haikutani bali binadamu hukutana. Hayo yalinipata mjini Karatu mwaka 2008 nilipokutana na mzee ambaye anaonekana nami pichani.

Siku hiyo ilikuwa siku ya mnada mjini Karatu, siku ambayo hutokea mara moja kwa mwezi. Katika umati mkubwa wa watu, yeye na mimi tulijikuta uso kwa uso. Yeye alinitambua mara moja, akauliza: "Profesa Mbele?" Nilimwambia ndio mimi. Tulifurahi sana, tukaanza michapo.

Mzee huyu nilimfahamu mwaka 1996 wakati nafanya utafiti wa masimulizi ya jadi kuhusu shujaa wa wa-Iraqw aitwaye Saygilo Magena. Utafiti huu ulinipeleka kwenye miji na vijijini kama vile Mbulu, Mamaisara, na Karatu.

Kati ya watu walionisaidia sana ni huyu mzee ambaye jina lake ni John Qamlali. Baada ya kufahamiana kule Mbulu, tulikutana tena mjini Arusha, tukaongea sana. Anajua sana habari za wa-Iraqw na ameshawasaidia watafiti wengine wa mataifa mbali mbali. Ninazo kanda za maongezi yetu.

Kukutana tena mwaka 2008, miaka zaidi ya kumi tangu tulipokutana mara ya kwanza, ilikuwa ni ajabu na pia jambo la kushukuru.

Tuesday, November 13, 2012

Nimeenda Tena Chuo Cha Mazingira, Minnesota

Leo nilitembelea tena Chuo cha Mazingira, mjini Apple Valley. Kama alivyofanya mwaka hadi mwaka, Mwalimu Todd Carlson alinialika kwenda kuongea na wanafunzi wake kuhusu uwiano baina ya masimulizi ya jadi na mazingira. Mwalimu Todd Carlson, anaonekana pichani kushoto kabisa










Mwalimu Carlson huwaeleza wanafunzi kuhusu masimulizi ya jamii mbali mbali za asili, kama vile wa-Marekani Wekundu, wenyeji wa asili wa Australia, na pia wa-Khoisan wa pande za kusini mwa Afrika.

Anatumia pia kitabu changu cha Matengo Folktales. Kila ninapoenda kuongea na wanafunzi hao, nawakuta wamesoma angalau sehemu fulani muhimu za kitabu hicho.



 


Kutokana na maandalizi hayo anayofanya Mwalimu Carlson, mazungumzo yangu na wanafunzi pamoja na masuali yao huwa ya kiwango cha juu.


Kama ilivyokuwa safari zilizopita, sote tumefurahia ziara yangu ya leo.

Tuesday, May 31, 2011

Safari ya Bajaji: Lushoto Hadi Irente

Agosti 6, mwaka jana, nilisafiri kutoka Lushoto kwenda Irente. Nilishawahi kusafiri hadi Irente miaka michache kabla, nikitumia teksi. Lakini mwaka jana niligundua kuwa ningeweza kusafiri kwa bajaji. Bajaji yenyewe ndio hii inayoonekana katika picha, na dreva wake. Bajai hii ilikuwa maarufu mjini Lushoto.

Niliziona bajaji kwa mara ya kwanza nilipokuwa India, mwezi Aprili mwaka 1991. Wakati huo hapakuwa na bajaji Tanzania. Lakini kidogo kidogo, miaka iliyofuatia, bajaji zilianza kuonekana, na leo zimejaa katika miji mikubwa kama Dar es Salaam. Sasa zinaonekana hata kwenye miji midogo kama Lushoto. Ndio mambo ya ulimwengu katika utandawazi wa leo.

Safari ilikuwa murua. Bajaji ilikula milima na kukwepa mifereji na mashimo kama mchezo. Tulipofika Irente, nilianza kuwatafuta vijana wawili mapacha ambao niliwafahamu miaka iliyotangulia, wakati nafanya utafiti kuhusu masimulizi juu ya Osale Otango na Paulo Hamisi. Osale Otango na Paulo Hamisi ni maarufu katika historia ya miaka ya hamsini na kitu, walipokuwa wakisakwa na serikali ya wa-Ingereza kwa ujambazi. Walikuwa wakizunguka na kujificha maeneo hayo ya Irente.

Kwa bahati nzuri siku hiyo, hao mapacha walikuwa kijiji cha jirani wakati bajaji yangu ilipofika hapo. Tulifurahi kukutana, tukapandisha njia hadi nyumbani kwao.

Nilipiga picha hii wakati tunateremka kutoka kanisani. Hao marafiki zangu wametangulia. Bajaji ilikuwa imepaki kwenye nyumba zinazoonekana kule ng'ambo. Upande wa kulia, kule ukingoni, ndipo penye mwamba ambapo watalii na wageni wengine hufika kuangalia mandhari ya sehemu hizo na sehemu za mbali. Panaitwa Irente Viewpoint. Kuna picha nyingi za mahali hapo mtandaoni. Ni mahali maarufu kiasi kwamba kama hujafika hapo, inakuwa kama vile hujafika Lushoto.

Hapa ninaonekana nikiwa na hao marafiki zangu mapacha. Kule nyuma yetu ni miamba ambayo nayo imepigwa picha sana na watalii na wageni wanaofika hapa Irente. Kuna miteremko ya kutisha maeneo hayo. Hata mimi ambaye natoka sehemu za milimani, Umatengo, kwenye milima na miteremko, ninatishika na miteremko ya Irente.

Monday, November 15, 2010

Tumesoma Masimulizi ya "Popol Vuh"

Leo katika darasa langu mojawapo tumemaliza kuongelea masimulizi ya kale ya Popol Vuh. Ni masimulizi ya zamani sana ya taifa la wa-Maya wa Amerika ya Kati. Wa-Maya wa zamani waliishi maeneo ambayo leo yanahusisha nchi za Mexico, Guatemala, Belize na Honduras. Walikuwa maarufu kwa mafanikio waliyofikia katika nyanja mbali mbali, kama vile ujenzi wa miji, ugunduzi wa hati ya kuandikia lugha yao, utafiti wa sayari, na utengenezaji wa kalenda.

Nilisikia juu ya Popol Vuh kwa mara ya kwanza mnamo mwaka 1982 kutoka kwa Profesa Harold Scheub, nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu Cha Wisconsin-Madison. Hata hivi hatukusoma kitabu hiki. Sasa nimefurahi kuwa katika darasa langu tumefanikiwa kukisoma na kukijadili, ingawa mambo yake mengi si rahisi kueleweka kwetu watu wa leo, wa tamaduni tofauti kabisa na ule utamaduni wa wa-Maya wa zamani.

Popol Vuh ni masimulizi kuhusu mambo mengi yahusuyo jinsi dunia ilivyoumbwa, na matukio mbali mbali yaliyofuatia, yakiwahusisha miungu na mashujaa wa aina aina. Ni masimulizi yenye uzito, kwani yanabeba mambo ya imani, maadili, utabiri na falsafa. Baadhi ya masimulizi ya Popol Vuh yanatukumbusha masimulizi ya vitabu vya dini kama Biblia au Quran, na pia masimulizi mengine kama Gilgamesh, au hata masimulizi maarufu ya wa-Kerewe, alivyoyaandika Mzee Kitereza katika kitabu chake cha Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka na Ntulanalwo na Buliwhali.

Kusoma vitabu vya aina hii ni jambo jema sana, kwani linatupa mwanga kuhusu hali halisi ya yale waliyopitia na kuwazia wanadamu sehemu mbali mbali za dunia.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...