Saturday, April 22, 2017

Yatokanayo na Ziara Ubalozi wa Tanzania Marekani

Wiki hii, tarehe 19, binti yangu Zawadi na mimi tulikwenda kwenye Ubalozi wa Tanzania mjini Washington DC kushughulikia pasposti mpya baada ya paspoti zetu kwisha muda wa matumizi yake. Nimeona niandike mambo yaliyoibuka mawazoni mwangu kutokana na ziara hiyo.

Kwanza tulijisikia vizuri kuingia katika jengo la Ubalozi, na kujisikia tumo katika ardhi ya Tanzania. Nilimweleza binti yangu jambo hilo, nikaongezea kwamba mtu wa taifa lolote akiingia humu kutafuta hifadhi na akapata, mamlaka ya nchi yake haiwezi kuingia na kumkamata. Itabidi wajaribu bahati yao kwa kufanya utaratibu wa kuiomba Tanzania ili wakabidhiwe huyu mtu wao. Tulitaja mfano wa Julian Assange wa WikiLeaks ambaye amejichimbia katika Ubalozi wa Ecuador, London.

Wazo jingine lililonijia tulipokuwa ndani ya Ubalozi ni jinsi wadhifa wa kuiwakilisha nchi ulivyo mkubwa na mzito nikilinganisha na uchache wa wawakilishi wetu katika Ubalozi. Ni wazi kuwa watu wachache tunaowapa wadhifa wa kuiwakilisha nchi yetu katika ofisi ya ubalozi hawawezi kufika kila mahali katika nchi kubwa kama hii ya Marekani. Kwa kuzingatia hilo, ni wazi kuwa sisi Wa-Tanzania wanadiaspora vote tunawajibika kuiwakilisha nchi yetu pale tulipo na tunapopata fursa ya kuwepo katika maeneo mengine.

Mimi ninakaa katika mji wa Northfield, jimbo la Minnesota, ambao ni mdogo sana lakini ni maarufu kwa kuwa na vyuo vikuu viwili: St. Olaf na Carleton. Katakana na wadhifa wangu kama mwalimu ninayeshughulika na watu kutoka sehemu zote za Marekani na sehemu mbali mbali duniani, nina fursa ya kufanya mengi pasipo kutegemea Ubalozi.

Ninashiriki matamasha, ninatoa mihadhara, na ninashiriki mikutano ya aina aina. Ninashiriki katika uendeshaji wa jumuia zinazowajumlisha watu wa mataifa mbali mbali hapa Minnesota, kama vile Afrifest Foundation. Wakati huu, baada ya kuteuliwa katika bodi ya Rochester International Association, nina wadhifa mwingine muhimu. Katika nafasi zote hizo, ninajiwakilisha mwenyewe lakini pia kama raia wa Tanzania.

Ingawa nilijua tangu zamani kuwa sisi wananchi tuna wajibu wa kuiwakilisha nchi yetu popote tulipo, ziara yangu Ubalozini imenipa hamasa zaidi katika mwelekeo huo. Nimesukumwa zaidi na ukweli kwamba wafanyakazi wa Ubalozini hawatoshi kabisa kwa majukumu yaliyopo ya kuiwakilisha na kuihudumia nchi huku ughaibuni.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...