Saturday, April 29, 2017

Tamasha la Mataifa Limefana Rochester, Minnesota.

Leo tamasha la mataifa limefanyika mjini Rochester, Minnesota. Niliweka tangazo la tamasha hili katika blogu hii. Binti yangu Zawadi na mimi tulishiriki. Ni mwendo wa saa moja kutoka hapa Northfield ninapoishi.

Tulipanga vitabu vyangu na machapisho mengine mezani, tukatundika ukutani bendera ya Tanzania ambayo nilinunua siku zilizopita. Saa nne ilipotimia, ambayo ndiyo saa ya kufunguliwa tamasha, watu walianza kuja. Na hapo kwenye meza yetu tulianza kutembelewa na watu tangu dakika zile za mwanzo. Tuliongea nao, tukajibu masuali kuhusu vitabu hivyo na mambo mengine mengi, nao wakatueleza mambo mbali mbali.


Baada ya nusu saa hivi, ilianza shughuli ya kupeperusha bendera. Watu walielekezwa zilipowekwa bendera ili wachukue bendera ya nchi yao na kujiunga katika maandamano wakiwa wamebeba bendera. Nilikwenda nikaikuta bendera ya Tanzania, nikaibeba katika maandamano.

Tuliendelea kuongea na watu wa mataifa mbali mbali hapo kwenye meza yetu, tukapata pia fursa ya kuzunguka kwenye meza za wengine, na kupiga picha. Kwa namna ya pekee ninakumbuka tulivyozungumza na mama mmoja Mmarekani, kuhusu tofauti za tamaduni akatueleza yaliyomkuta Japani. Mila na desturi alizozizoea Marekani ziliwashangaza wenyeji. Nasi tulimweleza yanayotokea pale wa-Afrika wanapokuwa na wa-Marekani, kama nilivyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Ninakumbuka pia nilivyoongea na mama anayeonekana pichani hapa kushoto amevaa hijab. Nilikumbuka kuwa nilimwona katika tamasha mwaka jana, ila hatukufahamiana. Jana tulipata hiyo fursa, mezani pake, ambapo aliweka machapisho ya ki-Islam, kama vile The Message of the Qur'an cha Muhammad Asad, Who Speaks for Islam cha John L. Esposito na Dalia Mogahed, na Wisdom for Life & The Afterlife: A Selection of Prophet Mohammad's Sayings, ambavyo vyote ninavyo.

Nilimwambia kuwa mimi ni mwalimu katika chuo cha St. Olaf; nimetunga kozi, "Muslim Women Writers." na sababu za kuitunga. Naye alinielezea kuhusu kipindi anachoendesha kiitwacho Faith Talk Show, tukakubaliana nije kuhojiwa katika kipindi hicho siku zijazo.

Baada ya kurejea kutoka kwenye tamasha, nimeangalia mtandaoni, nikaona taarifa za mama huyu kama vile hii hapa. Ninawazia kumwalika darasani kwangu nitakapofundisha tena kozi yangu.

Muda wote wa tamasha kulikuwa na vikundi vya burudani jukwaani na pia vyakula vya nchi mbali mbali. Ninaleta hapa baadhi ya picha za tamasha.





No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...