Showing posts with label Askofu Owdenburg Mdegella. Show all posts
Showing posts with label Askofu Owdenburg Mdegella. Show all posts

Monday, October 26, 2015

Shukrani kwa Wa-Tanzania Wadau wa Kitabu Changu

Blogu yangu ni mahali ninapojiandikia mambo yoyote kwa namna nipendayo. Siwajibiki kwa mtu yeyote, wala sina mgeni rasmi. Leo nimewazia mafanikio ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nimejikumbusha kuwa mtu hufanikiwi kwa juhudi zako pekee, hata ungekuwa hodari namna gani. Kuna watu unaopaswa kuwashukuru.

Nami napenda kufanya hivyo, kama ilivyo jadi yangu. Nimewahi kuwaongelea na kuwashukuru wanablogu wa-Tanzania, na nimewahi kuwaongelea na kuwashukuru wa-Kenya. Ninapenda kuendelea kuwakumbuka wa-Tanzania.


Mwanzoni kabisa, nilipokuwa nimeandika mswada wa awali kabisa wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, rafiki yangu Profesa Joe Lugalla, wa Chuo Kikuu cha New Hampshire, alipata kuusoma, akapendezwa nao.

Yeye, kwa jinsi alivyoupokea mswada ule, alikuwa kati ya watu wa mwanzo kabisa kunitia hamasa ya kuuboresha. Tangu wakati ule hadi leo amekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha watu wakisome kitabu hiki. Kwangu hili ni jambo la kushukuru sana, nikizingatia kuwa Profesa Lugalla sio tu ni m-Tanzania mwenzangu anayefahamu ninachosema kitabuni, bali pia yeye ni mtaalam wa kimataifa wa soshiolojia na anthropolojia.


Mtu mwingine aliyenihamasisha tangu miaka ya mwanzo ya kuwepo kwa kitabu changu ni Mhashamu Askofu Owdenburg Mdegella wa dayasisi ya Iringa ya Kanisa la ki-Luteri Tanzania. Nakumbuka tulivyokutana katika eneo la shule ya Peace House, Arusha, na hapo hapo akaanza kuongelea kitabu changu, akisema kuwa ni muhimu wazungu wakisome ili watufahamu sisi wa-Afrika. Siwezi kusahau kauli yake hiyo na namna alivyoongea kwa msisimko. Nilimwelewa vizuri kwa nini aliongea hivyo, kwani yeye anahusika moja kwa moja na mipango ya ushirikiano baina ya wa-Marekani na wa-Tanzania, hasa wa Iringa.


Dada Subi, mwanablogu maarufu miongoni mwa wa-Tanzania, ni mtu mwingine ambaye namkumbuka kwa namna ya pekee, kwa yote aliyofanya katika kunihamasisha na kukipigia debe kitabu changu. Nakumbuka aliwahi kuwasiliana nami juu ya kitabu hiki, lakini cha zaidi ni kuwa alikipigia debe katika blogu yake.

Dada Subi alinisaidia sana katika shughuli zangu za kublogu. Ingawa hatujawahi kuonana, ninamfahamu ni mkarimu sana.




Napenda nichukue fursa hii kumtaja na kumshukuru Bwana Muhiddin Issa Michuzi, mwanablogu maarufu wetu wa-Tanzania. Ingawa tumewahi kukutana mara moja tu, Michuzi amekuwa mstari wa mbele kutangaza shughuli zangu katika blogu yake, ikiwemo kitabu changu. Kutokana na hayo tumekuwa kama watu tuliozoeana. Kwangu hilo ni jambo la kushukuru.

Sitachoka kuwashukuru wachangiaji wa mafanikio yangu. Kama nilivyosema, hakuna mtu anayefanikiwa kwa uwezo wake peke yake. Ule usemi wa ki-Ingereza, "No man is an island," yaani hakuna mtu ambaye ni kisiwa, una ukweli usiopingika.

Kwa wanaotaka, walioko Tanzania, Kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kinapatikana Burunge Visitor Centre, simu 0754 297 504.

Thursday, February 12, 2015

Kitabu Kimetimiza Miaka Kumi

Kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimetimiza miaka kumi tangu nilipokichapisha, tarehe 5 Februari, mwaka 2005. Siku hiyo niliuingiza muswada katika mtandao wa lulu nikalipia namba ya utambulisho wa kitabu, yaani ISBN. Siku hiyo hiyo niliagiza nakala ya kwanza, nikaipata baada ya wiki moja hivi. Wiki hii ni kumbukumbu ya miaka kumi ya kuwepo kwa kitabu hiki.

Mambo mengi yametokea katika miaka hii kumi kuhusiana na kitabu hiki. Nimepata fursa ya kusikia maoni ya wasomaji wengi. Baadhi wameandika maoni hayo na kuyachapisha, kama vile katika tovuti, blogu, na majarida. Wengine wameniandikia maoni yao katika barua pepe. Wengine wamenieleza maoni yao katika maongezi ya ana kwa ana.

Watu waliotoa maoni yao kuhusu kitabu hiki ni wa aina mbali mbali. Baadhi nawakumbuka vizuri, kama vile Mhashamu Askofu Owdenburg Mdegella wa dayosisi ya Iringa ya Kanisa la Kiluteri Tanzania, ambaye alisema kuwa kitabu kimemfurahisha sana na anataka wageni wakisome ili watuelewe wa-Tanzania. Aliniambia hayo siku tulipokutana kwenye chuo cha Peace House, Arusha, na alikuwa anaongea kutokana na uzoefu wake mkubwa wa kuwapokea na kushughulika na wa-Marekani wanaokuja Tanzania katika mpango wa ushirikiano baina ya waumini wa-Marekani na wa-Tanzania uitwao Bega kwa Bega.

Mwingine ninayemkumbuka vizuri ni Balozi Mstaafu Andrew Daraja. Alikisoma kitabu hiki wakati akiwa balozi wa Tanzania hapa Marekani, na alinipigia simu akaniambia jinsi alivyokipenda kitabu hiki kama nyenzo ya kuweka maelewano baina wa wa-Marekani na sisi wa-Afrika.

Mzee Patrick Hemingway, katika maongezi naye, amekuwa akikisifia kitabu hiki. Siku tulipomtembelea, alisema kuwa kitabu hiki ni "tool of survival." Mzee huyu m-Marekani anajua anachokisema, kwani aliishi Tanganyika (baadaye Tanzania) kwa miaka yapata 25. Ninaguswa na maoni ya watu kama yeye, ambao wanajua hali halisi ya tofauti baina ya utamaduni wao na wetu.

Katika miaka hii kumi, nimepata mialiko kadha wa kadha kutoka kwenye vyuo, taasisi, makampuni, na vikundi, kwenda kutoa mihadhara kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake. Ingawa kitabu hiki ni kifupi tu kilichoandikwa kwa lugha rahisi, wala si cha kitaaluma, kimenisaidia kuendesha mihadhara hiyo na pia warsha, na hata kutatua migogoro ya kutoelewana baina ya wa-Marekani na wahamiaji na wakimbizi kutoka Afrika.

Ninawashukuru kwa namna ya pekee watu waliochangia kwa namna moja au nyingine kwa kukisoma kitabu, kuwaelezea wengine, na kunipa maoni yao. Wiki hii nitawakumbuka kwa namna ya pekee.

Mambo ni mengi sana yaliyotokea katika miaka hii kumi, ambayo ningeweza kuyaandikia kitabu. Panapo majaliwa, nitafanya hivyo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...