Monday, December 7, 2015

Nimesaini Vitabu Kwa Ajili ya Filamu ya "Papa's Shadow"

Wakati wa kampeni ya Ramble Pictures ya kuchangisha fedha kulipia gharama za filamu ya Papa's Shadow, nilichangia fedha kiasi na pia nakala za kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Walikuwa wameweka viwango mbali mbali vya michango ambavyo viliendana na vizawadi na vivutio kwa wachangiaji. Waliochangia dola 200 au zaidi waliahidiwa nakala ya kitabu changu kama zawadi.

Leo, Jimmy Gildea, mwanzilishi wa Ramble Pictures na mtengenezaji wa Papa's Shadow, ambaye alikuwa mwanafunzi katika kozi yangu ya Hemingway, alinifuata hapa chuoni St. Olaf, nikasaini nakala tano za kitabu changu, na kumkabidhi.

Tulipata fursa ya kuongelea habari za Ernest Hemingway, ziara yetu ya Montana, msisimko na mafanikio ya kampeni ya kuchangisha fedha, na kadhalika. Vile vile, Jimmy alinirekodi nikiwa nasoma kitabu cha Green Hills of Africa na pia nikiwa natembea katika sehemu iliyoonyesha vizuri mandhari ya chuo. Jimmy aliniuliza iwapo nina picha za ujana na utoto wangu. Anakusanya hayo ili kuyatafutia nafasi katika filamu ya Papa's Shadow, ingawa tayari ni nzuri sana, kwa jinsi nilivyoiona.

Papa's Shadow inategemewa kupatikana wiki chache kuanzia sasa, labda mwezi Februari. Si filamu ya kuigiza bali ni mazungumzo juu ya maisha, uandishi, na falsafa, ya Ernest Hemingway, hasa inavyohusiana na safari zake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye bado hai. Ni filamu inayoelimisha, si burudani.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...