Friday, February 19, 2016

"Tenzi Tatu za Kale:" Makala Inayosomwa Kuliko Zote

Mara kwa mara, ninaangalia takwimu zinazohusu blogu yangu hii: idadi ya watembeleaji, makala wanazozitembelea, na nchi walimo. Kuanzia wiki kadhaa zilizopita, makala inayotembelewa kuliko zote ni "Tenzi Tatu za Kale." Idadi ya watembeleaji iliongezeka ghafla pale Ndugu Michuzi alipoiweka makala hii katika blogu yake.

Ninajiuliza kwa nini makala hii inawavutia wasomaji namna hii. Je, hii ni ishara ya kupendwa kwa somo la fasihi ya ki-Swahili? Siamini kama ni hivyo, kwani ninaandika makala nyingi kuhusu fasihi, ambazo zinagusia tungo mbali mbali. Ingekuwa uwingi wa wasomaji unaonekana kwenye makala hizo pia, ningeamini kuwa kuna msisimko wa kupenda fasihi.

Ninapata hisia kwamba labda uhusiano na mahitaji ya shuleni au vyuoni. Ninahisi kuwa labda wanaosoma makala ya "Tenzi Tatu za Kale" ni wanafunzi ambao wanatakiwa kusoma Utenzi wa Al Inkishafi, au Utenzi wa Mwana Kupona, au Utenzi wa Fumo Liyongo: moja, mbili, au zote tatu.

Kama ni hivyo, si jambo la kuridhisha wala kufurahisha. Uwanja wa fasihi ya ki-Swahili ni mpana, na mwenye mapenzi na fasihi hii ninamtegemea awe anasoma tungo nyingi. Hata wanafunzi wa fasihi wanatakiwa kusoma tungo mbali mbali, si zile zilizomo katika mitaala tu.

Ningependa sana kuona mijadala ya fasihi ya ki-Swahili katika blogu hii. Ndio maana ninaweka taarifa mbali mbali kuhusu tungo za ki-Swahili. Tuienzi fasihi hii kwa kuisoma bila mipaka, kuichambua, na kuitangaza.
 

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...