Tuesday, February 23, 2016

"So Long a Letter" Katika Kozi ya "Muslim Women Writers"

Kozi yangu ya Muslim Women Writers inaendelea vizuri. Tulianzia India, na hadithi ya Sultana's Dream ya Rokeya Sakhawat Hossain. Baada ya hapo tunasoma So Long a Letter, utungo wa Mariama Ba wa Senegal, nchi mojawapo maarufu katika uwanja wa fasihi ya Afrika.

Senegal imetoa watunzi kama Leopold Sedar Senghor, Cheikh Hamidou Kane, Birago Diop, na Sembene Ousmane, kwa upande wa wanaume, na kwa upande wa wanawake kuna watunzi kama Aminata Sow Fall na Mariama Ba.

So Long a Letter ni utungo ulioandikwa kwa mtindo wa barua, ambayo mhusika mkuu anamwandikia mwanamke mwenzake, rafiki yake. Kwa hali hiyo, utungo huu unafuata jadi ambayo wanafasihi huiita "epistolary." Neno "epistolary" linatokana na neno la ki-Latini ambalo maana yake ni barua.

Suala moja muhimu linaloongelewa ni la wake wenza. Ni suala lenye chimbuko lake katika Qur'an, Sura iv aya 3:

     If ye fear that ye shall not
Bes able to deal justly
With the orphans,
Marry women of your choice,
Two, or three, or four;
But if ye fear that ye shall not
Be able to deal justly (with them),
Then only one, or (a captive)
That your right hand possess.
That will be more suitable,
To prevent you
From doing injustice.

Yusuf Ali, ambaye tafsiri yake ya Qur'an nimeinukuu hapa juu, anafafanua aya hii vizuri. Anakumbushia kwamba aya hii ilitokea katika mazingira maalum, ambamo kutokana na vita ya Uhud, jamii ya wa-Islam ilikuwa na wajane na yatima wengi, pamoja na mateka wa vita. Ilikuwa lazima watu hao watendewe kwa ubinadamu na haki kwa kiwango cha juu kabisa. Ruhusa ya kuwaoa wajane hao imewekewa masherti.

Kabla ya u-Islam, watu walikuwa wanaoa walivyopenda, lakini aya hii inaweka mipaka. Mtu anaweza kuoa hadi wake wanne, si zaidi, lakini kama Yusuf Ali anavyosema, "provided you could treat them with equality, in material things as well as in affection and immaterial things." Yaani masherti ni kwamba uweze kuwatendea wake hao kwa usawa katika mahitaji ya vitu, katika upendo, na mengine ya aina hiyo.

Kutokana na masherti hayo, Yusuf Ali anasema: "As this condition is most difficult to fulfill, I understand the recommendation to be towards monogamy." Yaani, kwa jinsi masherti yalivyo magumu kutekelezeka, nachukulia kwamba agizo hili linaegemea kwenye kuwa na mke moja.

Huu ndio msingi katika Qur'an wa suala la mitara. Wanawake wa-Islam wamekuwa wakilalamika kwamba fundisho la Qur'an limepotoshwa. Wanaume wamejitwalia mamlaka ya kupindisha mafundisho ya Qur'an na kuhalalisha mambo wanayoyapenda wao.  Hii ndio hali inayojitokeza katika So Long a Letter.

So Longer a Letter ni andiko linalohuzunisha kwa jinsi Ramatulaye anavyoelezea roho mbaya ya baadhi ya wanaume. Mume wake mwenyewe alijiolea binti kinyemela, na wanawake wengine wanakutana na adha za aina hiyo. Lakini, hasemi kuwa wanawake muda wote hawana dosari. Anakiri kuwa katika ndoa zingine, wanawake wanawatesa wanaume.

Hatimaye, So Long a Letter inaelezea matumaini ya kubadili mambo na kuwawezesha wanawake kushika nafasi wanazostahili katika jamii, wakitumia vipaji ambavyo wanavyo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...