Friday, February 26, 2016

Jumuia ya Vyuo (ACM) Yakihitaji Kitabu

Leo nimeshinda hapa mjini Chicago nikihudhuria mkutano wa bodi ya programu ya Tanzania ya ACM. ACM ni jumuia ya vyuo vikuu 14 vya hapa Marekani ambayo inaendesha programu za masomo na utafiti sehemu mbali mbali za dunia. Kwa upande wa Afrika, kuna programu ya Tanzania na programu ya Botswana. Mimi ni mjumbe katika bodi za programu hizi mbili.

Mkutano kama wa leo tunafanya mara moja kwa mwaka kwa program ya Tanzania na vivyo hivyo kwa programu ya Botswana. Kila mwaka tunapeleka wanafunzi kwenye nchi hizi kwa muhula moja. Tunapokutana tunatathmini mwenendo wa masomo kwa mwaka husika. Tunapitia ripoti mbali mbali na kuzijadili, kubaini mapungufu na mafanikio na mapungufu, kutoa mapendekezo na kujiwekea malengo.

Leo, pamoja na yote hayo, limetokea jambo ambalo sikutegemea. Profesa Paul Overvoorde, aliyeambatana na wanafunzi Tanzania muhula uliopita, alianza hima kunieleza kuwa alikuwa ametumia kitabu changu cha Africans and Americans Embracing Cultural Differences na kilimsaidia sana katika kuendesha programu. Profesa huyu nilikuwa sijawahi kuonana naye, kwa sababu sikuwa nimehudhuria mikutano yetu kwa miaka mitatu. Alivyokuwa anaelezea kitabu hiki, nilijikuta nina hisia mchanganyiko: shukrani, furaha, na mshamgao.

Kama vile hii haikutosha, wakati wa mkutano, Profesa Karl Wirth naye akakitaja kitabu hiki. Huyu tumefahamiana tangu miaka ya mwanzo ya programu hizi. Wakati tulipokuwa tunahitimisha mkutano alitoa wazo kwa uongozi wa ACM kuwa kitabu hiki kifanywe msingi wa "webinar" itakayovihusisha vyuo vyetu vyote kwa ajili ya kufundishia mambo yiliyomo, na hii iwe ni mkakati wa kuwavutia wanafunzi kwenye programu.

Wazo hili limeshapita. Wakati wajumbe tulipokuwa tunaagana, mhusika wa tekinolojia za mawasiliano katika ACM aliniambia kuwa atanitafuta ili nichangie hiyo "webinar." Nami nilimwambia nangojea kwa hamu kushirikiana naye, kwani ninamini kuwa nitajifunza mambo mapya.

Nimeandika habari hii kwa sababu maalum. Kwanza ni kujiwekea kumbukumbu, kama ilivyo desturi yangu katika blogu hii. Pili ni kwa sababu ninawakumbuka watu kadhaa ambao wamejaribu kuzibeza juhudi zangu, nami nikawa siyumbishwi. Ninafanya shughuli zangu kwa bidii na umakini niwezavyo na baada ya hapo ninayathamini matokeo yake. Mtu lazima ujiamini na ujithamini. Ukithamini kile unachokifanya. Ukiwa na mtazamo huu, huwezi kuyumbishwa. Matokeo yanakuja kuonekana baadaye. Chambilecho wa-Swahili wa zamani mgaagaa na upwa, hali wali mkavu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...