Monday, February 1, 2016

Dini sio Misahafu Pekee

Leo ninapenda kuendelea kuongelea dini, kujenga hoja kwamba dini si misahafu pekee. Ninaongelea mada hii kwa kuwa ninaamini umuhimu wa mijadala ya dini, na kwa kuzingatia tabia ambayo imejengeka Tanzania ya baadhi ya wa-Islam na wa-Kristu kulumbana kuhusu dini zao. Wanaonekana viwanjani wakihubiri dhidi ya dini ya wapinzani wao. Wananukuu misahafu katika kujenga hoja kwamba dini yao ni bora zaidi au ndio dini ya kweli.

Binafsi, naona kuwa malumbano haya ni upuuzi mtupu. Dini haiko katika misahafu tu. Ni mfungamano wa nadharia na vitendo. Dini ni mfungamano wa mafundisho ya misahafu na maisha ya kila muumini. Bila mfungamano huo, dhana ya dini inapwaya.

Kuna maana gani kwa muumini wa dini kuringia msahafu wa dini yake iwapo maisha yake hayaendani na mafundisho yaliyomo katika msahafu? Badala ya kulumbana kuhusu misahafu, tuangalie maisha ya waumini. Je, tabia za mu-Islam ni bora kuliko za m-Kristu? M-Kristu ni bora kuliko mu-Islam? Jamii ya wa-Islam ni bora kuliko jamii ya wa-Kristu? Wa-Kristu ni bora kuliko wa-Islam? Tofauti za imani zina uzito gani? Je, wa-Kristu, ambao wanaamini kuwa Yesu ni mwana wa Mungu, ni watu waovu kuliko wa-Islam, ambao hawaamini kuwa Yesu ni mwana wa Mungu bali ni nabii?

Kama waumini wa dini fulani ni wema, waungwana, wakarimu, wastahimilivu, wenye huruma, wa amani kuliko wengine, ninaamini kuwa waumini hao watawavutia hata watu wasio na dini. Dini si misahafu tu; ni mfungamano wa nadharia na vitendo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...