Thursday, February 4, 2016

Ganesha: Mungu Maarufu

Ganesha ni mmoja wa miungu wa dini ya Hindu. Dini hii ilianzia India, miaka zaidi ya elfu tatu iliyopita. Leo ina waumini yapata bilioni sehemu zote za dunia, kuanzia India na nchi za jirani, hadi Afrika Mashariki, visiwa vya Caribbean, na visiwa vya Pacific.

Ganesha ni mtoto wa kiume wa Shiva na Parvati. Ni mungu maarufu katika dini zingine pia, kama vile u-Buddha na u-Jaini. Katika michoro na sanamu anatambulika kirahisi, kwa kuwa ana kichwa cha tembo. Kuna masimulizi mbali mbali juu ya asili ya hiki kichwa chake.

Ganesha anategemewa kama mungu anayeondoa vikwazo. Anasafisha njia ya mafanikio. Mtu anapoanza safari, biashara, au mradi wowote, huelekeza maombi kwa Ganesha. Lakini pia, Ganesha huwawekea vikwazo wenye kiburi.

Ganesha ni mungu mwenye akili sana. Ndiye mlezi wa wanataaluma. Ni mungu wa uandishi pia, na inasemekana alitumia pembe yake kuandika sehemu ya utungo maarufu wa Mahabharata. Washairi na watunzi wa vitabu humtegemea. Aghalabu, katika picha na sanamu, Ganesha anaonekana akicheza. Ni mlezi wa wanamuziki na wasanii wengine.

Ganesha ni mmoja wa miungu wanaotajwa sana katika fasihi, nami ninapofundisha kozi kama South Asian Literature, napata fursa ya kuwaeleza wanafunzi habari za miungu hao. Ninashukuru kwa bahati niliyo nayo ya kujifunza fasihi, tamaduni, na dini mbali mbali na kuwafundisha wengine. Ni njia bora ya kujenga maelewano duniani.

Imani za watu zinanivutia, kama zinavyonivutia fasihi na tamaduni. Niliwahi kuandika katika blogu hii jinsi nilivyozuru nyumba za ibada za wa-Hindu nchini India. Napenda kusema kuwa mimi ambaye ni mwanataaluma, mwandishi, na mwanablogu, kama ningekuwa m-Hindu, ningekuwa ninamtegemea Ganesha.

Jambo moja ambalo linaweza kuwa gumu kwa sisi ambao si wa-Hindu kulielewa ni kuwa ingawa kuna miungu wengi katika dini hiyo, kwa undani wake u-Hindu ni dini inayotambua kuwepo kwa "Supreme Being," na kwamba hao miungu wengi ni nafsi za "Supreme Being." Ni kitendawili kama kile wanachokumbana nacho watu wasio wa-Kristu wanapoambiwa kuwa sisi wa-Kristu tuna dhana ya Utatu Mtakatifu katika Mungu Mmoja.
 

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...