Thursday, November 27, 2014

Kitabu Changu cha Ki-Swahili

Kitu kimoja ninachojivunia kama mwandishi ni juhudi niliyofanya kwa miaka mingi katika kuandika kwa ki-Swahili. Aliyenihamasisha na kunisukumia katika uandishi wa ki-Swahili ni rafiki yangu Mugyabuso Mulokozi, ambaye sasa ni profesa mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tangu tulipokuwa tunasoma wote "Mkwawa High School," aliona jinsi nilivyokuwa nimezama katika ki-Ingereza bila kujibidisha upande wa ki-Swahili.

Hatimaye, hasa tulipokuwa chuo kikuu, ambapo yeye nami tulikuwa tunafundisha, nilijitosa katika ulimwengu wa ki-Swahili. Kwanza nilisoma maandishi ya ki-Swahili, kisha nikaanza kufanya utafiti na kuandika makala magazetini. Kati ya maandishi niliyochapisha ni mapitio ya tamthilia ya Kijiji Chetu, iliyotungwa na Ngalimecha Ngahyoma.

Baadaye, nilianza utafiti kuhusu tungo za zamani za ki-Swahili, kama vile Utenzi wa Fumo Liongo, Al-Inkishafi na Utenzi wa Ras il Ghuli. Utafiti huu niliuendeleza nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, huku Marekani, miaka ya 1980-86.

Hatimaye, kwa kuombwa na Ndugu Maggid Mjengwa, mmiliki na mwendeshaji wa Mjengwablog, niliandika makala katika gazeti aliloanzisha, Kwanza Jamii. Baadaye, makala hizi nilizikusanya na kuzichapisha kama kitabu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Nilipochapisha kitabu hiki, niliandika taarifa katika blogu yangu ya ki-Ingereza.

Kuandika kwa ki-Swahili ni namna ya kuienzi lugha hii. Lugha ni utambulisho wa utaifa na ni kielelezo cha jinsi mtu unavyoheshimu utaifa wako na unavyojitambua na kujiheshimu wewe mwenyewe, kama alivyobainisha Frantz Fanon hasa katika vitabu vyake viwili: The Wretched of the Earth na Black Skin, White Masks.

Ninajivunia kitabu hiki kwa vile kimenipa fursa ya kupima uwezo wangu wa kuandika ki-Swahili sanifu. Ingawa bado naandika zaidi kwa ki-Ingereza, sijarudi nyuma katika uandishi wa ki-Swahili. Mbali na hili suala la kujitambua na kujitambulisha kwa kuienzi lugha yetu kwa vitendo, kitabu hiki kilitokana pia na msukumo wa watu waliokuwa wananiuliza kwa nini naandika kwa ki-Ingereza tu. Watu hao waliniambia kuwa ingekuwa bora niandike pia kwa ki-Swahili, ili wa-Tanzania walio wengi waweze kuyaelewa mawazo yangu. Nami niliona hii ni hoja nzuri.

Hata hivi, kitabu hiki hakijapata wasomaji wengi. Labda hii ni kwa sababu nilikichapisha huku Marekani, mtandaoni. Kama hili ndilo tatizo, napenda kusema kuwa kitabu hiki, sawa na vitabu vyangu vingine, kinapatikana kutoka kwangu, kwa anwani hii: africonexion@gmail.com au simu namba (507) 403 9756.

Lakini pia kuna suala la kukosekana kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu miongoni mwa wa-Tanzania, jambo ambalo limekuwa likisemwa na wahusika mbali mbali katika sekta ya vitabu. Tungekuwa na utamaduni huu, tungeona tahakiki na mijadala kuhusu vitabu, sio tu miongoni mwa wanafunzi na wasomi, bali katika jamii, kupitia vyombo vya habari, magazeti, na mitandao ya mawasiliano.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...