Sunday, November 16, 2014

Mwandishi Unapoitwa Kuongelea Kitabu Chako

Siku hizi, mara kwa mara, nawazia jukumu linaloningoja, la kwenda mjini Zumbrota, Minnesota, kutoa mhadhara. Mada ni "Incorporating Immigrants into our Culture and Worship," kama nilivyoeleza katika blogu hii. Mwaliko wa kutoa mhadhara huu umetokana na kitabu nilichoandika, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sikualikwa nikaongelee kitabu hiki, lakini kwa hali yoyote, baadhi ya yaliyomo kitabuni yatajitokeza katika mhadhara na katika kipindi cha majibu na masuali. Napenda kusema machache kuhusu jukumu la kutoa mhadhara kuhusu kitabu ulichoandika.

Mara nyingi, hutokea kwamba watu utakaozungumza nao wanakuwa wameshakisoma kitabu. Ni lazima utafakari kabla kwamba utaongelea nini, na jambo hilo hutegemea aina ya kitabu.

Kama ni riwaya, watu hutegemea utawaeleza mambo kama vile nini kilikuwa chanzo cha wewe kuandika, yaani nini kilichokufanya uandike, njia uliyopitia katika kuandika, maandishi au waandishi waliokuathiri, matatizo uliyokumbana nayo, na mambo uliyojifunza.

Lakini, watu hutegemea pia, au labda zaidi, kuwa utasoma angalau kurasa kadhaa za riwaya yako, ili wasikie sauti yako na sauti ya wahusika katika hadithi yako kwa mujibu wako wewe kama mtunzi.

Hapa kushoto tunamwona mwandishi Nuruddin Farah wa Somalia, alipokuwa anaongelea riwaya yake mpya ya Crossbones, chuoni Carleton. Anaonekana akisoma kurasa kadhaa.

Wasikilizaji huvutiwa kumsikia mwandishi namna hiyo, kwani usomaji wake ni aina ya tafsiri sio tu ya kile alichoandika, bali kilichokuwa mawazoni mwake wakati anaandika. Watu huamini kuwa usomaji wa mwandishi una ukweli na uhalisi ambao msomaji mwingine hawezi kuufikia.


Hiyo ndiyo halisi inavyokuwa, iwapo kitabu ni riwaya au mashairi. Sauti na usomaji wa mwandishi vina mvuto huo niliouelezea, ingawaje kwa kifupi.

Lakini kuna pia vitabu vya aina tofauti, kama hiki changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Unapokuwa umealikwa kuongelea kitabu cha aina hiyo, ni lazima utafakari vizuri suala zima.

Iwapo watu hao wameshakisoma, nadhani jukumu lako sio kuwasomea kurasa za kitabu, bali ni kuongelea mambo yatokanayo na yale uliyoandika. Jukumu lako ni kufafanua baadhi ya yale uliyoandika, ambayo unaamini yanakidhi mahitaji ya watu watu wale, kufuatana na mwaliko wao.

Pengine, inawezekana uzungumze bila kufungua kitabu, ingawa unacho mbele yako. Kwa mfano, kwenye hii mada ya mhadhara wangu wa Zumbrota, siamini kama nitahitaji kuwasomea kurasa zozote kutoka kitabuni. Badala yake, ikibidi, nitajumlisha mafundisho yatokanayo, yenye kukidhi mategemeo ya mada.

Aina hii ya mhadhara nimeshatoa mara nyingi. Kwa mfano, hapa kushoto ninaonekana nikiongea na wanachuo waliokuwa wanajiandaa kwenda Afrika Kusini kwenye ziara ya kimasomo. Walishasoma kitabu changu, na profesa wao aliniita kuja kuongelea masuala ya aina niliyozungumzia kitabuni, kama sehemu ya maandilizi ya safari ya wanafunzi wale. Kwa vile wanafunzi walikuwa wameshasoma kitabu, mhadhara huu ulitawaliwa zaidi na masuali na majibu. Profesa wao aliandika kuhusu mhadhara wangu katika blogu yake.

Kwa ujumla, fursa hizi hunifurahisha, sio tu kwa sababu nakutana na wasomaji na wadau wengine ana kwa ana, bali pia napata wasaa wa kujipima ni kiasi gani naifahamu mada husika na vipengele vyake.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...