Tuesday, November 25, 2014

Tuna Likizo Fupi ya "Thanksgiving"

Leo hapa chuoni tunaanza likizo fupi itakayokwisha mwisho wa wiki. Ni wakati wa sikukuu maarufu hapa Marekani iitwayyo "Thanksgiving." Kwa mwaka huu, "Thanksgiving" ni keshokutwa, tarehe 27.

Kwa upande wangu, nilianza hayo mapumziko jana mchana, baada ya kufanyisha mtihani katika somo langu la "South Asian Literature." Kwa hivi, kipindi hiki ambacho ni cha mapumziko sitapumzika, bali nitakuwa nasahihisha huo mtihani.

Vile vile, wakati huu ambapo hatufundishi, ninaendelea kujisomea maandishi mbali mbali, hasa tamthilia ya Macbeth. Ninangojea kwa hamu kuandika ripoti yake wiki hii hii katika blogu hii. Pamoja na jukumu la kusahihisha mtihani, naona akili yangu imetulia vizuri, kiasi cha kuniwezesha kuitafakari tamthilia ya Macbeth na kuifaidi vilivyo.

Nikirudi kwenye hii sikukuu ya "Thanksgiving," ningeweza kusema mengi kuhusu historia yake, pia malumbano na migogoro ya kiitikadi ambayo imeigubika sikukuu hii hasa miaka ya hivi karibuni.

Kifupi ni kuwa hii ni sikukuu ambayo ni kumbukumbu ya ujio wa wazungu katika nchi hii ya Marekani. Historia wanayoisimulia ni kuwa wale wazungu wa mwanzo waliwakuta wenyeji, tunaowaita Wahindi Wekundu, na hao wenyeji waliwakaribisha wageni hao, na ndio waliowawezesha hao wahamiaji kustawi katika mazingira ya nchi hii.

Kwa mujibu wa masimulizi hayo, hiyo "Thanksgiving" ni kumbukumbu na fursa ya kutoa shukrani. Batamzinga ndio chakula rasmi kwa siku hiyo, kiasi kwamba wa-Marekani wanapowazia sikukuu hii, wanaiunganisha moja kwa moja na mlo huo. Historia yake nayo ni ndefu.

Lakini, hasa miaka ya karibuni, wanaharakati wa hilo taifa la Wahindi Wekundu na wengine, wanaikosoa historia inayosimuliwa kuanzia katika vitabu vya watoto hadi katika media zingine, kwa msingi kuwa inapotosha ukweli kwamba wale wazungu waliingia nchi hii kwa mabavu, wakafanya maovu mengi dhidi ya wenyeji, yakiwemo mauaji na kupora ardhi. Wanaharakati wanaona hii sikukuu ya "Thanksgiving" kama ni tusi kwao. Wanaiona kama siku ya maombolezo.

Ni vema kwetu ambao hatukukulia nchi hii kujielimisha ili angalau tuelewe huu mgogoro wa kiitikadi. Tuelewe hisia za wenyeji wa asili wa nchi hii. Tusiwe watu wa kusherehekea tu, na kula batamzinga, kama wanavyosherehekea wengine hapa Marekani, bali angalau tufahamu utata wa suala zima la hii sikukuu.

Kwa upande mwingine, kila kabila au taifa hapa duniani lina wakati ambapo wanasherehekea na kutoa shukrani, hasa wakati wa mavuno. Dhana ya kutoa shukrani sio dhana ya Marekani pekee. Ingawa mimi si m-Marekani na hii si nchi yangu, ninaamini kuwa kinachotakiwa ni wao kutafuta njia za kutatua huu mgogoro wa kiitikadi niliouelezea.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...