Sunday, November 9, 2014

Nimealikwa Kutoa Mhadhara

Siku chache zilizopita, nilipigiwa simu kutoka Faribault, kwenye Kanisa la First English Lutheran Church. Wananiuliza iwapo nitaweza kwenda kutoa mhadhara katika Cannon River Conferenc utakaofanyika mwezi Aprili mjini Zumbrota, Minnesota.

Mada ya mkutano itakuwa "Incorporating Immigrants Into our Culture and Worship," na mhadhara wangu unatarajiwa kuwa dira ya mkutano.

Miaka kama sita hivi iliyopita, nilialikwa First English Lutheran Church, Faribault, kutoa mihadhara kuhusu yale niliyoandika katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimefurahi kuwa mihadhara yangu ile inakumbukwa, tena mama aliyenipigia simu alinikumbusha kuwa anaikumbuka baadhi ya michapo yangu na pia kitabu changu. Hata hivi, kwenye mkutano kama huu wa Zumbrota, mada sio niliyoandika katika kitabu changu, ingawaje nitakitumia kama msingi mojawapo wa kuijadili mada niliyopewa. Patakuwepo pia na muda wa masuali na majibu. 

Huu mkutano wa Zumbrota utawaleta pamoja wanajumuia kutoka makanisa ya eneo hili la Minnesota ya Mashariki Kusini. Hapa Marekani, makanisa yako mstari wa mbele katika kuwapokea na kuwahudumia wakimbizi kutoka nchi mbali mbali.

Kwenye mji wa Faribault wenyewe, kwa mfano, makanisa ya kiLuteri na Katoliki yamekuwa yakifanya shughuli hiyo tangu pale wakimbizi na wahamiaji walipoanza kuja, kutoka sehemu kama Amerika ya Kati, Somalia, na Sudan. Hawana ubaguzi, iwe ni kwa msingi wa taifa, dini, au jinsia.

Nami, moja ya shughuli zangu katika mfumo huo imekuwa kuwasaidia wenyeji na wakimbizi na wahamiaji kuzitambua na kuzitafakari tofauti za tamaduni zao. Kuna ugumu kwa wageni kuelewa mambo ya Marekani, na kwa wa-Marekani kuna ugumu kuelewa mambo ya hao wageni. Msimamo wangu, kwenye mikutano ya aina hii, daima umekuwa kwamba sote tunawajibika kufanya juhudi kujielimisha. Hatuwezi kuuachia upande moja tu uwajibike. Wengi hawajazoea kusikia wazo kama hili.

Ninawaenzi hao waumini wa-Marekani  wanavyojitahidi kutatua tatizo hilo kwa namna yoyote iwezekananyo. Mikutano kama huu wa Aprili ni mfano mojawapo, kutoa changamoto ya kuwawezesha kuzitambua na kuzitafakari tofauti za tamaduni, kwa lengo la kuleta maelewano bali pia kuwezesha masuala kama hili suala la ibada za pamoja.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...