Showing posts with label Ufisadi. Show all posts
Showing posts with label Ufisadi. Show all posts

Tuesday, March 10, 2015

Mdau Anauliza Kama Ufisadi Utaisha Nchini

Mdau anonymous ameomba tusome makala ifuatayo na ameuliza iwapo ufisadi utaisha Tanzania.

Makala aliyoleta inamhusu Dr. Fulgence Mosha, anayeonekana pichani, daktari bingwa mstaafu wa hospitali ya KCMC, ambaye amekuwa akihangaikia mafao yake ya ustaafu kwa miaka kumi bila mafanikio. Makala aliyoileta mdau ni hii hapa.

Thursday, February 23, 2012

Dini Inayoenea kwa Kasi Kuliko Zote Tanzania

Mara kwa mara ninawasikia watu wakiongelea suala la dini inayoenea kwa kasi kuliko zote Tanzania, Afrika au duniani kwa ujumla. Kila mtu ana mtazamo wake. Wengine wanatoa pia takwimu, ambazo sijui kama ni za kweli au ndoto. Ni mchezo wa kuringiana nani zaidi kwa kutumia takwimu, wakati dini ni suala la mtu binafsi. Wala hutaingia ahera kwa msingi kuwa dini yako hapa duniani ilikuwa na wafuasi wengi kuliko dini nyingine.

Kwa mtazamo wangu, dini inayoenea kwa kasi kuliko zote Tanzania ni ufisadi na ushirikina. Ufisadi na ushirikina huo unaendelea kushamiri kiasi kwamba unajitokeza hata kwenye nyumba za ibada za dini mbali mbali. Hebu tutafakari hilo.

Saturday, January 29, 2011

Mikataba Bomu Itaendelea Kutumaliza

Wa-Tanzania wanalalamika sana kuhusu mikataba bomu ambayo inalisababishia Taifa hasara kubwa. Tafsiri yao, kwa ujumla, ni kwamba tunaingizwa katika janga hili na mafisadi ambao wanasaini kwa makusudi mikataba hii, kwamba hao ni wa-Tanzania wenye ubinafsi na uroho, na hawana uchungu na nchi, bali wanatafuta namna ya kunufaika wao. Mafisadi wetu hao wanashirikiana na mafisadi wa nje kuitafuna nchi yetu.

Kwa ujumla, nami nina hisia hizo. Kwanza kuna ukweli usiopingika kuwa maadili katika nchi yetu yanazidi kuporomoka. Vile vile nazingatia usemi wa wahenga kuwa lisemwalo lipo, na kama halipo laja. Pia tunaona taarifa kutoka sehemu mbali mbali za dunia kuhusu uozo wa rushwa katika masuala ya mikataba, zabuni, na kadhalika.

Lakini msimamo wangu hauishii hapa. Naamini kuwa hata kama tukiondoa kabisa rushwa na ufisadi, tukawa na watu wanaojali maslahi ya nchi na hao ndio wakawa wanaosaini mikataba yetu, bado tutaendelea kulizwa na mikataba bomu.

Kitakachosababisha janga hili ni kuanguka kwa elimu katika Tanzania. Kama ninavyosema daima katika blogu hii na sehemu zingine, wa-Tanzania tumejichimbia kaburi kwa kutothamini elimu ipasavyo. Ushahidi ni ufahamu wa lugha ulivyo duni, na utamaduni wa kununua na kusoma vitabu ulivyofifia au kutoweka miongoni mwetu.

Nikifafanua suala la lugha na kulihusisha na suala la mikataba, napenda kusema kuwa tupende tusipende, mikataba ya kimataifa itaendelea kuandikwa kwa ki-Ingereza, nasi tutajikuta tunasaini bila kuelewa vizuri kilichomo. Kuna matapeli wengi duniani, ikiwamo katika uwanja wa biashara na uwekezaji.

Wajanja, kwa kutambua umbumbumbu wetu, watachukulia mwanya huu kama mbinu ya kutukomoa. Laiti tungekumbuka msisitizo wa Mwalimu Nyerere pale tulipopata Uhuru, kuhusu maadui watatu tuliopaswa kupambana nao: umaskini, maradhi na ujinga.

Mwaka jana, serikali ya CCM ilitamka mara kwa mara kwamba imefanya marekebisho katika mikataba ya madini, ili kuziba mianya iliyokuwepo, iliyokuwa inatukosesha mapato tunayostahili. Sasa hapo nina suali. Ni nini kilichotufanya tusione hizo dosari tangu mwanzo? Kama si ufisadi, labda ni huu ujinga ninaoongelea. Binafsi, nakerwa kwamba serikali haijatuelezea undani wa suala hilo.

Monday, April 19, 2010

Fisadi Anapoingia Baa

Binafsi, siwaamini wa-Tanzania wanapojifanya kuwalalamikia mafisadi. Hapo nawaongelea wa-Tanzania kwa ujumla, ingawa bila shaka wako baadhi ambao kweli wanachukia ufisadi. Lakini jamii kwa ujumla, siamini kama inachukia.

Wa-Tanzania wanapenda sana starehe, au kwa maneno ya siku hizi, makamuzi na minuso. Shughuli muhimu katika maisha ya wa-Tanzania ni sherehe. Pamoja na kwamba yote hayo yanagharimu sana, michango ya sherehe haiishi.

Katika hali hii yeyote anayechangia sana sherehe hizi anaheshimiwa na kushangiliwa. Fisadi anayo nafasi kubwa ya kujijengea heshima katika jamii yetu, kama ni mchangiaji bora wa sherehe hizi.

Fisadi akiwa baa na kuwanunulia watu bia sana, anajijengea heshima kubwa. Wote wanamtetemekea na kumwita "mzee," na heshima yake inabaki juu.

Wa-Tanzania hawaulizi huyu mtu anapata wapi hela. Na hata wakijua, maadam anawanunulia bia na kuchangia sherehe kwa kiwango cha juu, wanafurahi na kumwenzi. Pamoja na kelele zote za kulalamikia ufisadi, sijawahi kuwasikia wa-Tanzania wakizisusia bia za fisadi. Kelele hizi kwa kiasi kikubwa ni usanii mtupu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...