
Namshukuru Mungu kwa kunipa akili na utashi nitafakari mambo na kujiamulia. Ninamshukuru kwa jinsi anavyotuneemesha, kwa kuwaumba wanadamu wa kila aina, wenye dini mbali mbali, tamaduni na lugha mbali mbali. Dunia inapendeza kwa tofauti hizo, sawa na maua yanavyopendeza, kwa uwingi wa tofauti za rangi.
Namshukuru Mungu kwa yote aliyoyaweka duniani: nchi kavu, bahari, milima, mabonde, mito, miti, majani na maua. Ametuwekea wanyama wa kila aina, ndege na wadudu, jua, mwezi na nyota, mvua na upepo, vitu vinavyoonekana na visivyoonekana.
Vyote ni mazao ya uumbaji wa Mungu. Ninaomba niwe na moyo wa kuwapenda wanadamu wote na vyote alivyoumba Mungu. Ninaomba niwe mtu mwema, mwenye kutambua na kuzingatia kila siku kuwa Mungu amenipa uhai, akili, na vipaji, si kwa ajili yangu, bali kwa manufaa ya walimwengu bila kujali tofauti zao, za taifa, kabila, dini, jinsia, umri, utamaduni, lugha, na kadhalika.
Kuwa kanisani, kujumuika na waumini wenzangu, ni fursa ya kujikumbusha imani ya dini yangu, kuwaombea walimwengu wote, wabarikiwe. Sasa, baada ya kutoka kanisani, ninajisikia mwenye faraja, moyo mkunjufu, na ari ya kuendelea na majukumu yangu.