Showing posts with label somo. Show all posts
Showing posts with label somo. Show all posts

Sunday, November 5, 2017

Hadithi Zetu za Jadi

Hadithi zetu za jadi ni hazina kubwa ya utamaduni wetu. Kila kabila lilikuwa na hadithi nyingi, pamoja na aina nyingine za fasihi simulizi, kama vile nyimbo, na methali. Hadithi zina tafakari juu ya maisha na tabia za binadamu ingawa mara nyingi wahusika wana taswira za wanyama, ndege au viumbe vingine. Zinaelezea masuala ya familia, malezi ya watoto, wajibu wa wazazi na watoto. Zinatoa tahadhari kuhusu tabia mbaya na maelekezo juu tabia njema. Zinafundisha huruma, maelewano, ushiriano na kusaidiana.

Hadith zinaelezea mahangaiko, mategemeo, mafanikio, ubora na udhaifu wa binadamu, Kuna hadithi za kusisimua hisia na fikra, zenye kuibua masuali kuhusu maana ya maisha, kama walivyoibua wanafalsafa wa mkondo uitwao "existentialism," kama nilivyogusia katika kitabu cha Matengo Folktales.

Kitabu hiki ni mkusanyo wa hadithi kumi za ki-Matengo, ambazo nilizitafsiri kwa ki-Ingereza. Niliandika uchambuzi wa kila hadithi na nikaandika pia insha ya jumla kuhusu hadithi, ili kuwapa wasomaji kianzio cha kuzichambua.

Nilipokuwa ninaandaa kitabu hiki, nilikuwa mhadhiri katika Chuo kikuu cha Dar es Salaam. Somo mojawapo nililokuwa ninafundisha ni "Oral Literature" (fasihi simulizi). Hapakuwa na kitabu cha kufaa kufundishia somo hilo kwa wanafunzi wa chuo kikuu. Hapakuwa na kitabu cha kufundishia hadithi za jadi, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Kwa hivyo, lengo langu lilikuwa ni kuziba pengo, kwa kuandika kitabu ambacho nilitaka kiwepo. Hii ni falsafa ambayo imekaa kichwani mwangu: kama hakuna kitabu ambacho ungetaka kiwepo, andika hicho kitabu. Au kama kitabu unachosoma hakikuridhishi, andika hicho ambacho kitakuridhisha.

Ingawa kitabu changu si kikamilifu, angalau kinakidhi mahitaji yangu ya kufundisha somo la hadith i za jadi kwa wanafunzi wa chuo kikuu. Ni faraja kwangu kuwa si mimi peke yangu mwenye wazo hilo. Kuna wengine ambao wanakitumia kama ilivyokuwa katika chuo kikuu cha Montana na chuo cha St. Benedict/St. John's.

Thursday, October 8, 2015

Wanafunzi Wangu wa Ki-Ingereza

Ni yapata mwezi sasa tangu tuanze muhula mpya wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Ninafundisha kozi mbili, South Asian Literature na "First Year Writing." Hii ya kwanza ni kozi ya fasihi ya ki-Ingereza kutoka India, Pakistan, na Sri Lanka. Ya pili ni kozi ya uandishi wa ki-Ingereza. Picha hii kushoto, ya darasa la ki-Ingereza (FYW), tulipiga leo. Mwanafunzi mmoja hayumo. Niliweka picha ya darasa kama hili katika blogu hii.

Nilipenda ualimu tangu utotoni. Ninawapenda wanafunzi. Ninawaambia hivyo tangu siku ya kwanza ya masomo, nao wanashuhudia hivyo siku zote. Wanajionea ninavyojituma kuwaelimisha kwa uwezo wangu wote na kwa moyo moja. Sina ubaguzi, dhulma, wala upendeleo. Hiyo imekuwa tabia yangu tangu nilipoanza kufundisha, mwaka 1976, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Ninajivunia jambo hilo.

Kwa miezi mingi, hasa mwaka jana, afya yangu haikuwa njema, na nilichukua likizo ya matibabu. Ingawa nimeanza tena kufundisha, inatokea mara moja moja kwamba sijisikii vizuri. Juzi ilitokea hivyo, ikabidi niwaambie wanafunzi hao waendelee kuandika insha niliyowaagiza kabla, nikawaaga.

Jana, nilipofika ofisini, nilikuta kadi mlangoni pangu, ambayo picha yake inaonekana hapa kushoto. Wanafunzi hao walikuwa wameniandikia hiyo kadi na ndani walikuwa wamesaini majina yao. Maneno yanayoonekana pichani yanatokana na michapo yangu darasani. Nilivyoipata kadi hii, niliguswa. Nimewaambia hivyo leo, tulipoanza kipindi.

Ualimu si kazi rahisi. Inahusu taaluma. Inahusu malezi. Inahusu kuwashauri na kuwasaidia wanafunzi katika hali mbali mbali za maisha. Lakini, hayo ndiyo mambo yanayonivutia katika ualimu. Mafanikio ya wanafunzi masomoni na maishani ndio mafanikio na furaha yangu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...