Saturday, February 21, 2009

Nchi Zinazoendelea: Ni Zipi Hizo?

Dhana ya "nchi zinazoendelea" imejengeka vichwani mwa watu, tangu zamani. Pamoja na dhana hiyo, kuna pia dhana ya "nchi zilizoendelea." Je, dhana hizo zina mantiki yoyote?

Binafsi, ingawa zamani nilikuwa na mawazo kama wengine, kwamba kuna nchi zilizoendelea na zile zisizoendelea au zinazoendelea, miaka hii nimegundua kuwa dhana hizi hazina mantiki, na ni ushahidi wa kasumba vichwani mwa watu, au elimu duni.

Kwa mujibu wa dhana hizo, nchi kama Marekani, Uingereza, Sweden, Ujerumani, na Japani zinahesabiwa kuwa zimeendelea. Lakini nchi kama Tanzania, Kenya, na Uganda zinahesabiwa kuwa nchi zinazoendelea.

Kwa nini nasema dhana hizi ni duni? Kwanza, hakuna nchi duniani ambayo imesimama tu. Kila nchi iko katika mchakato na mabadiliko katika uchumi, siasa, utamaduni, na kadhalika. Marekani ya mwaka juzi ni tofauti na Marekani ya leo, na Marekani ya miaka mitano ijayo itakuwa tofauti na hii ya leo. Na ndivyo ilivyo kwa nchi zote. Kama ni tekinolojia, kwa mfano, tekinolojia inabadilika muda wote katika nchi kama Marekani. Kama ni utamaduni, ni hivyo hivyo. Na ndivyo ilivyo kwa nchi zote. Mabadiliko hayaishi, iwe ni katika Tanzania au Uingereza.

Kama huu mchakato na mabadiliko ndio maendeleo, basi kila nchi duniani ni nchi inayoendelea. Ni upuuzi kuziona baadhi ya nchi kama nchi zilizoendelea, wakati nazo ziko katika kubadilika muda wote.

Lakini, jambo la msingi zaidi ni dhana ya maendeleo. Maendeleo ni nini, na nani anayeweka vigezo vya kupima haya maendeleo? Hili ni suali la msingi.

Kwa ujumla, baadhi ya nchi, hasa zile ambazo zilikuwa zimetutawala wakati wa ukoloni, na zile zenye nguvu katika dunia ya leo, ndizo zinazoweka vigezo. Na wengi wamefundishwa kukubali hayo mawazo ya kikoloni na kikoloni mamboleo, bila kufikiri. Kwa vile Ulaya inajitapa kwamba imeendelea, Waafrika na wengine sehemu mbali mbali za dunia nao wanakubali hivyo na kuziona nchi zao kuwa ni nchi zinazoendelea au zisizoendelea. Hii ni kasumba.

Ingekuwa tunavyo vichwa timamu na tunavitumia ipasavyo, tungetafakari mambo sisi wenyewe, na tungetathmini dhana ya maendeleo. Tungejiuliza, maendeleo ni nini? Tungejiuliza iwapo dhana ya maendeleo ya watu wa Ulaya ni sherti tuipokee na kuikubali. Tungechukua jukumu na wajibu wa kujitungia vigezo vyetu na kuvitumia.

Kwa vile hatufanyi hivyo, tumebaki kuwa kasuku. Chochote kinachotoka Ulaya au Marekani tunakiona ni maendeleo. Papo hapo, watu wa Ulaya hawaoni chochote cha kwetu kuwa ni maendeleo. Ni pale tu tunapoiga mambo yao ndipo tunahesabiwa kuwa tunaendelea.

Hata kama jambo halina maana, maadam linatoka Ulaya au Marekani, watu katika nchi zetu wanaliona ni maendeleo. Hata kama ni mambo yasiyoendana na utu, maadam yametoka Ulaya, watu wetu wanayaona ni maendeleo. Kwa mfano, nchi zinazoitwa zimeendelea zimefanikiwa kuharibu mazingira kwa ujenzi wa viwanda na miundombinu mbali mbali, kiasi kwamba hewa katika nchi hizo sio safi, maji sio salama, mahusiano ya jamii ni ya wasi wasi.

Cha kushangaza ni kuwa watu wetu nao wanataka tufanye kama wanavyofanya Ulaya au Marekani, na miji yetu iwe kama ya huko Ulaya na Marekani, na viwanda na miundombino iwe kama ilivyo Ulaya na Marekani. Wanatamani nchi zetu ziwe na kila kitu ambacho kiko Ulaya na Marekani, ili tuonekane tumeendelea. Je, hayo ndio maendeleo?

Kwa hali ilivyo, hali ya nchi kadhaa kujiona kuwa zimeendelea, nchi zetu hazitafikia wakati wa kuwa sawa na hizo zingine. Mfumo huu uliopo hautaisha. Watu wa Ulaya na Marekani wataendelea kuyaona mabadiliko ya nchini kwao kuwa ndio maendeleo, na sisi tutakuwa daima watu wa kufuata hayo ya kwao. Kwa mtindo huu, hatutaweza kuwa mbele yao au sambamba nao.

Nchi zote ziko katika hali ya mabadiliko ya kila aina, katika nyanja mbali mbali. Hakuna nchi iliyomaliza mchakato huu na kuwa nchi ambayo imesimama na haibadiliki tena. Pasipo kuwa na vigezo vinavyozingatia haki ya kila watu duniani kuchangia katika kutunga tafsiri na viwango vya maendeleo, si sahihi kuendelea kutumia dhana ya nchi zilizoendelea na nchi zinazoendelea au zisizoendelea. Inatubidi tubadili fikra; tukatae huu mkondo uliopo sasa wa kuitwa au kujiita nchi zinazoendelea. Ni fikra tegemezi, za kikasuku, na kikoloni mamboleo, fikra zinazothibitisha kuwa tunahitaji elimu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...